Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutosheleza Tamaa Yetu ya Kuwa na Marafiki

Kutosheleza Tamaa Yetu ya Kuwa na Marafiki

Kutosheleza Tamaa Yetu ya Kuwa na Marafiki

“UPWEKE si ugonjwa,” chasema kitabu In Search of Intimacy. “Upweke ni hisia inayofaa . . . , ni ishara ya kawaida inayoonyesha kwamba tunahitaji marafiki.” Kama vile njaa inavyotuchochea kula chakula kinachofaidi mwili, ndivyo upweke unavyopaswa kutuchochea kutafuta marafiki wa kweli.

Hata hivyo, kulingana na msichana Mfaransa anayeitwa Yaël, “kuna watu ambao hujitenga kabisa na wengine.” Lakini hata sababu yetu ya kujitenga iwe nini, hatuwezi kusuluhisha matatizo yetu kwa njia hiyo, kwani tunapojitenga na wengine tunakuwa wapweke hata zaidi. Methali moja ya Biblia husema hivi: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” (Methali 18:1) Kwa hiyo, tunahitaji kwanza kutambua uhitaji wetu wa kuwa na marafiki, kisha tujitahidi kuutosheleza.

Chukua Hatua Zinazofaa Ili Upate Marafiki

Badala ya kujisikitikia au kuwaonea wivu wale walio na marafiki wengi au marafiki wazuri, jitahidi kusitawisha mtazamo unaofaa kama Manuela anayeishi nchini Italia. Anasema hivi: “Nilipokuwa kijana, nilihisi upweke. Ili kukabiliana na hali hiyo, niliwachunguza watu waliokuwa na marafiki wazuri. Kisha nikajaribu kuiga sifa zao nzuri ili niwe mtu mwenye kupendeza.”

Hatua moja muhimu ni kujitunza kimwili na kiakili. Ukila chakula kinachoboresha afya, kupumzika vya kutosha, na kufanya mazoezi ya kutosha, utajihisi vizuri na utapendeza. Ukiwa nadhifu, safi, na ukivalia vizuri, wengine watafurahia kushirikiana nawe, na utajiheshimu. Hata hivyo, usihangaikie sura yako kupita kiasi. Gaëlle, anayeishi Ufaransa, anasema: “Si lazima uvalie mitindo ya kisasa ya mavazi ili upate marafiki wa kweli.” Pia anasema: “Watu wenye kuheshimika hupendezwa hasa na sifa nzuri za mtu.”

Hata mawazo na hisia zetu huathiri yale tunayosema na jinsi tunavyoonekana. Je, una mtazamo mzuri kuhusu maisha? Hilo litakusaidia uwe na uso mchangamfu. Tabasamu ya kweli huvutia sana. Roger E. Axtell, ambaye ni mtaalamu anayechunguza ishara za mwili ambazo watu hutumia kuwasiliana na wengine, anasema kwamba mtu anaweza kutabasamu “mahali popote na katika hali zozote zile” na “mara nyingi hataeleweka vibaya.” * Isitoshe, ukifurahia ucheshi watu watavutiwa nawe.

Kumbuka kwamba sifa hizo nzuri ni za ndani. Kwa hiyo, jitahidi kujaza mawazo yanayofaa katika akili na moyo wako. Soma habari za maana na zenye kupendeza kama vile kuhusu matukio ya karibuni, utamaduni mbalimbali, na maumbile. Sikiliza muziki unaoburudisha. Lakini usiruhusu televisheni, sinema, na riwaya zichochee hisia na akili zako kuwazia mambo yasiyowezekana. Mahusiano yanayoonyeshwa kwenye sinema si halisi, si urafiki wa kweli, bali ni mawazo ya mtu fulani.

Eleza Yaliyo Moyoni!

Zuleica, anayeishi Italia, anakumbuka hivi: “Nilipokuwa mchanga, nilikuwa mwenye haya, na ilikuwa vigumu kupata marafiki. Lakini nilijua kwamba ikiwa tunataka kupata marafiki, tunapaswa kuchukua hatua ya kwanza ya kujitambulisha na kuwajua wengine.” Naam, ili uwe na marafiki wa kweli ni lazima uwaeleze wengine yaliyo moyoni mwako—acha wakujue vizuri. Mawasiliano ya aina hiyo ni muhimu ili kuwa na marafiki wa kweli kuliko kuwa na sura yenye kupendeza na vipawa vya pekee. Dakt. Alan Loy McGinnis, ambaye ni mshauri, anasema: “Watu walio na marafiki wazuri wanaweza kuwa watu wenye haya, watu wasio na haya, vijana, wazee, watu wasio wachangamfu, watu wenye akili, watu wenye sura isiyovutia, au watu wenye sura ya kuvutia; lakini wote wana sifa moja, yaani, wao hueleza yaliyo moyoni mwao. Wao huwaruhusu watu wajue vizuri yaliyo moyoni mwao.”

Hiyo haimaanishi uwafunulie watu wote hisia zako wala kuwaambia watu usiowatumaini siri zako. Lakini inamaanisha kuwa mteuzi na kuwafunulia watu fulani hatua kwa hatua mawazo na hisia zako. Michela, anayeishi Italia, anasema: “Mwanzoni, nilikuwa na tatizo la kuficha hisia zangu. Nilihitaji kufanya mabadiliko kwa kujitahidi kuonyesha hisia zangu zaidi ili marafiki wangu waelewe jinsi ninavyohisi na wavutiwe nami.”

Hata ikiwa unapenda kushirikiana na watu kiasili, unahitaji wakati na kufanya mambo pamoja na wengine ili mwe marafiki wanaotumainiana. Usihangaikie sana maoni ya watu kukuhusu. Elisa, anayeishi Italia, anakumbuka hivi: “Tatizo langu lilikuwa kwamba kila mara nilipotaka kusema jambo fulani, niliogopa kukosea. Basi nikawaza hivi, ‘Ikiwa wao ni marafiki wa kweli, watanielewa.’ Hivyo nilijicheka nilipokosea, nao wengine wakacheka pia.”

Basi, usiwe na wasiwasi! Usijifanye. Kujifanya hakusaidii. Mshauri mmoja wa familia anayeitwa F. Alexander Magoun aliandika hivi: “Tunavutia zaidi tunapokuwa wanyoofu na kutenda kama kawaida yetu.” Watu wenye furaha ya kweli hawahitaji kujifanya ili kuwafurahisha wengine. Tutapata marafiki wa kweli ikiwa tu tutakuwa wanyoofu. Vivyo hivyo, tunahitaji kuwaruhusu wengine watende kama kawaida yao. Watu wenye furaha huwapenda wengine jinsi walivyo, bila kulalamika kuhusu makosa yao madogo-madogo. Hawahisi kwamba wanahitaji kubadili tabia za marafiki wao ili zipatane na mapendezi yao. Jitahidi kuwa mtu mwenye furaha, asiyewachambua-chambua wengine.

Uwe Mwenye Urafiki Ili Uwe na Marafiki

Kuna jambo jingine lililo muhimu zaidi. Miaka 2,000 hivi iliyopita, Yesu alionyesha kwamba siri ya kufanikisha mahusiano ya wanadamu ni upendo usio na ubinafsi. Alifundisha hivi: “Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo.” (Luka 6:31) Naam, ili upate marafiki wa kweli, hupaswi kuwa na ubinafsi. Kwa ufupi, ili uwe na rafiki lazima uwe mwenye urafiki. Ili urafiki udumu, mtu anahitaji kutoa si kupokea tu. Tunapaswa kuwa tayari kuhangaikia mahitaji ya marafiki wetu kabla ya kuhangaikia mapendezi yetu.

Manuela, aliyenukuliwa mapema, anasema: “Kama vile Yesu alivyosema, furaha ya kweli inatokana na kutoa. Yule anayepokea hufurahi, lakini yule anayetoa hufurahi zaidi. Njia moja ya kutoa ni kuwajulia hali marafiki wetu, kujitahidi kuelewa matatizo yao, na kufanya yote tuwezayo kuwasaidia hata kabla hawajatuomba.” Kwa hiyo, pendezwa na wengine, kutia ndani marafiki ulio nao tayari. Imarisha urafiki wenu. Usipoteze marafiki kwa sababu ya kushughulikia mambo yasiyo na maana. Tunapaswa kutumia wakati pamoja na marafiki na kuwahangaikia. Ruben, anayeishi Italia, anasema: “Unahitaji kutumia wakati ili kupata na kudumisha marafiki. Kwanza kabisa, unahitaji wakati ili kusikiliza kwa makini. Sote tunaweza kuboresha jinsi tunavyosikiliza na kupendezwa na mambo ambayo wengine wanasema kwa kutowakatiza wanapozungumza.”

Waheshimu Wengine

Jambo jingine muhimu ili kudumisha urafiki wenye furaha ni kuwaheshimu wengine. Hiyo inatia ndani kujali hisia za wengine. Bila shaka, ungependa marafiki wako watumie busara wakati maoni na mapendezi yenu yanapotofautiana. Je, haingefaa uwatendee vivyo hivyo?—Waroma 12:10.

Njia nyingine ya kuonyesha heshima ni kuepuka kuwalemea marafiki wetu kwa hisia nyingi kiasi cha kuwafanya wahisi kwamba wamebanwa. Rafiki wa kweli hana wivu wala hamnyimi rafiki yake uhuru. Biblia husema hivi kwenye 1 Wakorintho 13:4: “Upendo hauna wivu.” Kwa hiyo, epuka mwelekeo wa kutotaka marafiki wako wawe na marafiki wengine. Wanapowafunulia wengine hisia zao, usikasirike na kuwaepuka. Tambua kwamba sote tunapaswa kupanuka. Waruhusu marafiki wako wapate marafiki wengine.

Pia, tambua kwamba marafiki wako wanahitaji kuwa na faragha. Watu mmoja-mmoja, na vilevile wenzi wa ndoa, wanahitaji kufanya mambo fulani wakiwa peke yao. Ingawa unapaswa kujihisi huru kuwafikia wengine, uwe na usawaziko na mwenye ufikirio, na unapowatembelea marafiki wako usiwachoshe kwa kukaa sana. Biblia inaonya hivi: “Fanya mguu wako uwe haba nyumbani kwa mwenzako, asije akakuchoka.”—Methali 25:17.

Usidai Ukamilifu

Bila shaka, watu wanapojuana vizuri, wao hufahamu udhaifu na sifa nzuri za wenzao. Hata hivyo, hilo halipaswi kutuzuia kufanya urafiki. Pacôme, anayeishi Ufaransa, anasema: “Wengine huwatazamia watu wafanye mengi sana ili wawe marafiki wao. Wao hutaka wawe na sifa nzuri tu, lakini hilo haliwezekani.” Kwa kuwa sisi si wakamilifu, hatupaswi kuwadai wengine ukamilifu. Ingawa hatujakamilika, sisi hutaka marafiki wetu watukubali na wavumilie udhaifu wetu. Basi, je, hatupaswi kujaribu kuvumilia udhaifu wa marafiki wetu kwa kuepuka kuufikiria na kuukazia kupita kiasi? Mwandishi Dennis Prager anatukumbusha hivi: “Wanyama-vipenzi tu ndio marafiki wasio na kasoro (yaani, wale wasiolalamika, ambao hutupenda nyakati zote, ambao hawakasiriki kamwe, ambao hutukazia fikira nyakati zote, na wasioweza kutukatisha tamaa kamwe).” Ikiwa hatutaki marafiki wetu wa karibu zaidi wawe wanyama-vipenzi, tunahitaji kutii shauri la mtume Petro la kuacha ‘upendo ufunike dhambi nyingi.’—1 Petro 4:8.

Inasemekana kwamba urafiki huongeza shangwe yetu na kupunguza huzuni yetu. Hata hivyo, hatupaswi kuwatarajia marafiki wetu watutimizie mahitaji yetu yote wala kututatulia matatizo yetu yote. Huo ni ubinafsi.

Marafiki wa Kufa Kuzikana

Tukiisha kupata rafiki, hatupaswi kumpuuza. Marafiki wasipoonana kwa muda mrefu kwa sababu ya kuishi mbali, wao huendelea kufikiriana na kusali kwa ajili ya mmoja na mwenzake. Hata wakionana mara chache tu, ni rahisi kwao kuelewana haraka na kufurahia kuwa pamoja. Ni muhimu kuwategemeza marafiki wetu hasa wanapokabili hali ngumu. Hatupaswi kuwahepa marafiki wetu wanapopata matatizo. Huo ndio wakati wanapotuhitaji zaidi. “Rafiki wa kweli anapenda nyakati zote, naye ni ndugu aliyezaliwa kwa ajili ya wakati wa taabu.” (Methali 17:17) Marafiki wa kweli wanapokosana, wao hupatana haraka na kusameheana. Marafiki wa kweli hawavunji urafiki wao eti kwa sababu mambo yamekwenda mrama.

Ukiepuka ubinafsi na ukisitawisha maoni mazuri kuwahusu wengine unaweza kupata marafiki. Hata hivyo, ni muhimu kufikiria aina ya watu unaochagua wawe marafiki wako. Unaweza kuchaguaje marafiki wazuri? Makala inayofuata inazungumzia jambo hilo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona makala “Tabasamu Ni Yenye Manufaa Kwako!” katika gazeti la Amkeni! la Julai 8, 2000.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6, 7]

Je, Mwanamume na Mwanamke Wanaweza Kuwa “Marafiki Tu”?

Je, mwanamume na mwanamke ambao si wenzi wa ndoa wanaweza kuwa marafiki? Hilo linategemea jinsi tunavyolitumia neno “rafiki.” Yesu alikuwa rafiki wa karibu wa Maria na Martha walioishi Bethania, na wote walikuwa wanawake waseja. (Yohana 11:1, 5) Mtume Paulo alikuwa rafiki ya Prisila na mume wake, Akila. (Matendo 18:2, 3) Bila shaka, watu hao walipendana sana. Hata hivyo, hatuwezi kuwazia kwamba Yesu na Paulo waliruhusu uhusiano huo uwe wa kimahaba.

Maisha ya kisasa huwafanya wanaume na wanawake kushirikiana sana kuliko wakati mwingine wowote, hivyo inakuwa lazima hata zaidi kwa watu wa jinsia zote kujua jinsi ya kufanya urafiki unaofaa kati yao. Pia, wenzi wa ndoa hufaidika wanapofanya urafiki na wenzi wengine wa ndoa na waseja.

Gazeti Psychology Today linaonya hivi: “Inaweza kuwa vigumu sana kutofautisha hisia za kimahaba, za kingono, na za kirafiki.” Pia linaongeza hivi: “Kuna uwezekano wa mwanamume na mwanamke ambao ni marafiki kuvutiana kingono bila kukusudia. Kumbatio la kawaida linaweza kuamsha hamu ya ngono haraka.”

Ni muhimu kwa wenzi wa ndoa kuona mambo kihalisi. Katika kitabu chake Happiness Is a Serious Problem, Dennis Prager, anaandika hivi: “Uhusiano wowote wa karibu pamoja na wengine unaweza kuhatarisha ndoa.” Kisha anaongeza: “Uhusiano wa karibu hautegemei ngono tu, na mwenzi wako wa ndoa ana haki ya kuwa rafiki yako wa karibu zaidi wa jinsia tofauti.” Yesu alisema kwamba kudumisha usafi wa kiadili hutegemea moyo. (Mathayo 5:28) Basi, uwe mwenye urafiki, lakini linda moyo wako na ujitahidi sana kuepuka hali zinazoweza kukufanya uwaze, uhisi, au utende kwa njia isiyofaa kumwelekea mtu wa jinsia tofauti.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Kutunza akili na mwili wako hufanya upendeze

[Picha katika ukurasa wa 8]

Marafiki huelezana yaliyo moyoni