Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Marafiki Wazuri na Wabaya

Marafiki Wazuri na Wabaya

Marafiki Wazuri na Wabaya

MSICHANA mmoja tutakayemwita Sarah alieleza yaliyo moyoni mwake kwa huzuni. Aligundua kwamba mwanamume aliyekuwa rafiki yake ni muuaji. Sarah aliuliza hivi: ‘Ikiwa mtu ninayemtumaini anaweza kufanya jambo kama hilo, ninawezaje kumtumaini mtu yeyote?’ Mtu aliyekuwa akimsikiliza Sarah alimuuliza ikiwa anajua maadili ya mwanamume huyo aliyekuwa rafiki yake. Sarah akajibu hivi, “Unamaanisha nini?” Sarah hakujua “maadili” ni nini. Vipi wewe? Je, unajua maadili ya marafiki wako?

Kama vile kisa cha Sarah kinavyoonyesha, jibu la swali hilo linaweza kumaanisha uhai au kifo. Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” (Methali 13:20) Hata hivyo, kama vile Sarah, watu wengi huchagua marafiki kwa kutegemea jinsi wanavyohisi wanapokuwa pamoja nao. Tunapenda kushirikiana na watu wanaotufurahisha. Lakini ikiwa sisi huchagua marafiki kwa njia hiyo, bila kufikiria sifa zao, tunaweza kukatishwa tamaa sana. Unaweza kujuaje ikiwa mtu ana maadili bora?

Uhitaji wa Kuwa na Maadili Bora

Kwanza, tunapaswa kuwa na maadili bora. Tunahitaji kutofautisha mema na mabaya na kuwa na maadili bora nyakati zote. Methali nyingine ya Biblia inasema: “Chuma hunolewa kwa chuma. Ndivyo mtu anavyounoa uso wa mwingine.” (Methali 27:17) Watu wawili ambao ni marafiki wanapokuwa na maadili bora, wanaweza kusaidiana kukomaa, na hilo litaimarisha urafiki wao.

Pacôme, anayeishi Ufaransa, anasema: “Kwa maoni yangu, rafiki wa kweli ni yule ambaye hunisikiliza, huzungumza nami kwa fadhili, na kunikemea ninapotenda upumbavu.” Bila shaka, marafiki bora zaidi, wawe vijana au wazee, ni wale ambao hutusaidia kufuata njia inayofaa na kutusahihisha tunapoelekea kutenda kipumbavu. Biblia inasema: “Makaripio ya rafiki yaonyesha uaminifu.” (Methali 27:6, Biblia Habari Njema) Ili tujiimarishe kiadili na kiroho, tunahitaji kushirikiana na wale wanaompenda Mungu na kanuni zake. Céline, anayeishi Ufaransa, anakumbuka hivi: “Kwa kuwa hakukuwa na mwanafunzi yeyote shuleni aliyefuata maadili na mafundisho yetu ya Kikristo, niliona umuhimu wa kuwa na marafiki wa kweli katika kutaniko la Kikristo. Wamenisaidia sana kutenda kwa busara.”

Kuwachunguza Watu Tunaotaka Wawe Marafiki Wetu

Ikiwa unataka kufanya urafiki na mtu fulani ambaye umekutana naye karibuni, jiulize hivi, ‘Marafiki wake ni nani?’ Unaweza kufahamu mengi kumhusu mtu kwa kuchunguza marafiki wake wa karibu. Isitoshe, watu wakomavu na wanaoheshimika katika jamii wanamwonaje mtu huyo? Kwa kuongezea, ni jambo la busara kuchunguza jinsi watu tunaotaka wawe marafiki wetu wanavyowatendea wengine, hasa jinsi wanavyowatendea watu ambao hawawezi kuwafaidi kwa njia yoyote. Ikiwa kwa kawaida mtu huyo si mnyoofu, si mwaminifu, hana subira, na hawajali wengine, je, kweli atakutendea vizuri nyakati zote?

Ili ufahamu utu wa mtu unahitaji subira, ustadi, na wakati kumchunguza katika hali za kawaida. Biblia inasema hivi: “Shauri moyoni mwa mtu ni kama kilindi cha maji, lakini mtu mwenye utambuzi ataliteka.” (Methali 20:5) Tunahitaji kuzungumza na watu tunaotaka kufanya urafiki nao kuhusu mambo mazito, yaani, mambo yanayofunua nyutu zao, nia zao, na maadili yao. Wao ni watu wa aina gani? Je, ni wenye fadhili au ni wenye ubaridi? Je, wao ni wachangamfu na wenye mtazamo mzuri au ni wenye kuchambua-chambua na wenye mtazamo mbaya? Je, wana ubinafsi? Je, ni waaminifu au si waaminifu? Ikiwa mtu huwachambua wengine mnapokuwa pamoja, je, hatakuchambua usipokuwepo? Yesu alisema hivi: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.” (Mathayo 12:34) Hivyo, tunapaswa kuzingatia yale ambayo watu husema kwa kuwa yanatufunulia utu wao.

Mapendezi Muhimu

Watu fulani hufikiri kwamba marafiki wao wanapaswa kuwa na mapendezi kama yao. Mvulana mmoja alisema kwamba hawezi kuwa rafiki ya mtu asiyependa keki anayoipenda sana. Ni kweli kwamba ili marafiki waelewane, wanahitaji kuwa na mapendezi mengi yanayofanana, na ni muhimu sana wafuate kanuni zilezile za kiadili na kiroho. Lakini si lazima wawe na utu na malezi yaleyale. Kwa kweli, mambo tofauti-tofauti ambayo watu wamejionea maishani yanaweza kuboresha urafiki.

Katika Biblia tunasoma kuhusu urafiki kati ya Yonathani na Daudi na kati ya Ruthu na Naomi, ambao ulitegemea kujitoa kwao kwa Mungu na kwa kanuni zake. * Inapendeza kwamba katika visa vyote viwili, marafiki hao walitofautiana sana kwa umri na malezi. Tunajifunza jambo jingine kuhusu urafiki kutokana na mifano hiyo: Vijana na wazee wanaweza kusaidiana sana wanapokuwa marafiki.

Kufaidika Kutokana na Marafiki Wenye Umri Mbalimbali

Tunaweza kufaidika sana tunapokuwa na marafiki wenye umri mkubwa au mdogo kuliko wetu. Fikiria maelezo haya ya vijana yanayotegemea mambo waliyojionea maishani.

Manuela (Italia): “Muda fulani uliopita nilifanya urafiki na wenzi fulani wa ndoa. Niliwaeleza yaliyokuwa moyoni mwangu, na ninafurahi kwamba hata wao walifanya hivyo. Hawakunipuuza eti kwa sababu mimi ni kijana. Hilo lilinifanya nivutiwe nao. Urafiki wao ni muhimu hasa ninapokabili matatizo. Ninapowaeleza wasichana wa rika langu matatizo yangu, nyakati nyingine wao hunipa mashauri yasiyofaa. Lakini marafiki wangu wenye umri mkubwa wana uzoefu, ufahamu, na busara ambayo sisi vijana hatuna. Wamenisaidia kufanya maamuzi yanayofaa.”

Zuleica (Italia): “Tunapofanya karamu sisi huwaalika vijana na vilevile watu kadhaa wanaotuzidi umri. Nimetambua kwamba watu wenye umri mkubwa na vijana wanapochangamana katika karamu, sote hutiwa moyo. Sisi hufurahi kwa sababu tunafaidika kutokana na maoni tofauti-tofauti.”

Nyinyi wenye umri mkubwa mnaweza pia kupendezwa na vijana. Kama maelezo hayo yanavyoonyesha, vijana wengi huthamini sana ujuzi wenu mwingi na hufurahia ushirika wenu. Amelia, mjane aliye na umri wa miaka 80 na kitu, anasema: “Mimi huwajulia hali vijana. Bidii yao na nguvu zao hunichangamsha!” Tunaweza kufaidika sana tunapotiana moyo kwa njia hiyo. Vijana wengi wenye furaha husema kwamba wamefanikiwa hasa kwa sababu walipokuwa wachanga walikuwa na marafiki wenye umri mkubwa ambao waliwawekea mfano mzuri na kuwapa mashauri yanayofaa.

Kuboresha Urafiki

Si lazima utafute marafiki wapya ili uwe na marafiki wazuri. Ikiwa tayari una marafiki wazuri, kwa nini usijaribu kuimarisha urafiki wenu? Marafiki wetu wa muda mrefu ni wenye thamani sana, na tunapaswa kuwaona hivyo. Kamwe usipuuze uaminifu wao.

Zaidi ya yote, kumbuka kwamba furaha ya kweli na urafiki wa kweli hutegemea kujitoa na kutumia wakati na mali zako. Utapata faida nyingi sana ukijitahidi na kujidhabihu. Hata hivyo, hutafanikiwa ukijifikiria mwenyewe tu unapochagua marafiki. Kwa hiyo, unapotaka kuanzisha urafiki, usifikirie tu watu unaovutiwa nao au wale ambao wanaweza kukufaidi. Fanya urafiki na wale ambao hupuuzwa na wengine au wale wanaoona ni vigumu kupata marafiki. Gaëlle, anayeishi Ufaransa, anasema: “Tunapopanga kufanya jambo fulani pamoja na wengine sisi huwakaribisha vijana wapweke. Sisi huwaambia hivi: ‘Tunajua hamngependa kubaki nyumbani peke yenu. Mnaweza kuandamana nasi. Acheni tufahamiane vizuri.’”—Luka 14:12-14.

Kwa upande mwingine, watu wazuri wanapotaka kuwa marafiki wako, usiwazuie. Elisa, anayeishi Italia, anasema: “Huenda ukaudhika unapokumbuka kwamba ulipuuzwa zamani. Huenda ukafikiri hivi, ‘Si lazima niwe na marafiki.’ Kwa hiyo unaamua kujitenga na wengine, na hilo linakufanya uhisi upweke, na kujifikiria tu. Badala ya kutafuta marafiki, unafanya iwe vigumu zaidi kuwapata.” Badala ya kuruhusu maoni yasiyofaa au ubinafsi ukuzuie kuanzisha urafiki, jitahidi kufahamiana na wengine. Tunapaswa kufurahi sana watu wanapotujali na wanapotaka kuwa marafiki wetu.

Unaweza Kupata Marafiki wa Kweli

Ili kupata marafiki wa kweli unahitaji kufanya mengi zaidi ya kutamani, kungoja, na kusoma makala kama hizi. Kujifunza jinsi ya kuanzisha urafiki ni sawa na kujifunza kuendesha baiskeli. Hatuwezi kujifunza mambo hayo kwa kusoma vitabu tu. Tunahitaji kujizoeza, hata ikiwa tutakosa kufaulu mara kwa mara. Biblia huonyesha kwamba urafiki ulio imara zaidi hutegemea sana kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. Lakini Mungu hawezi kutubariki na marafiki tusipojitahidi kuwapata. Je, ungependa kupata marafiki wa kweli? Usikate tamaa! Sali upate msaada wa Mungu, tafuta marafiki bila ubinafsi, na ujitahidi kuwa rafiki.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Unaweza kusoma kuhusu urafiki huo katika vitabu vya Biblia vya Ruthu, Samweli cha Kwanza, na Samweli cha Pili.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

Madokezo kwa Ajili ya Wazazi

Sawa na masomo mengine mengi, mtu hujifunza kuhusu urafiki anapokuwa nyumbani. Maisha ya familia humwezesha mtoto mdogo kuwa na marafiki. Hata hali za familia zikiwa nzuri, mawazo, hisia, na tabia za mtoto hutegemea sana watu anaoshirikiana nao. Kwa mfano, watoto wengi wachanga wa watu waliohamia nchi nyingine hujifunza lugha mpya haraka kwa kushirikiana na watoto wengine.

Mkiwa wazazi, mna pendeleo la kuwasaidia watoto kuchagua marafiki kwa hekima. Watoto wachanga na vijana wanaobalehe hawana ujuzi wa kutosha kufanya maamuzi hayo bila mwongozo wa wazazi. Hata hivyo, kuna tatizo. Vijana wengi huhisi wakiwa karibu na vijana wenzao kuliko wazazi wao au watu wengine wenye umri mkubwa.

Wataalamu fulani wanaamini kwamba jambo moja linalowafanya vijana watafute mwongozo kutoka kwa marika wao badala ya kutoka kwa wazazi ni kwamba wazazi wengi hawasadiki kwamba wana uwezo wa kuwapa watoto wao mwongozo unaofaa. Wazazi wanapaswa kutimiza daraka lao walilopewa na Mungu la kuwaongoza na kuwahangaikia watoto wao. (Waefeso 6:1-4) Watafanyaje hivyo? Dakt. Ron Taffel, ambaye ni mtaalamu wa mambo ya familia, hukutana na wazazi wengi ambao hawajui jinsi ya kushughulika na watoto wao wanaobalehe. Anaandika kwamba wazazi wengi “hufuata mashauri ya kuwalea watoto ambayo yanatolewa na vyombo vya habari” badala ya kutimiza madaraka yao. Kwa nini wao hutegemea mashauri hayo? “Kwa kuwa hawana uhusiano wa karibu na watoto wao, hawajui jinsi ya kuwasaidia.”

Hata hivyo, wazazi wanaweza kuwa na uhusiano mzuri na watoto wao wanaobalehe. Wazazi wanapaswa kufahamu kwamba watoto wao watawaendea marafiki wao ikiwa mahitaji yao hayatimizwi nyumbani. Watoto wanahitaji nini? Taffel anasema: “Wanahitaji kile ambacho vijana wamekuwa wakihitaji sikuzote: kuzoezwa, kuthaminiwa, kulindwa, kuelezwa waziwazi sheria na mambo wanayotarajiwa wafanye, na kuonyeshwa kwamba wanahitajiwa katika familia. Tatizo lililopo leo ni kwamba mahitaji ya vijana wengi wanaobalehe hayatoshelezwi na watu wazima, nao hawaonyeshwi upendo katika familia zao.”

Utawasaidiaje watoto wako kupata marafiki wazuri? Hatua ya kwanza ni kuchunguza maisha yako na marafiki wako. Je, wewe na marafiki wako mna miradi mizuri na maisha mazuri yasiyo na ubinafsi? Je, miradi na maisha yenu ni ya kiroho au ya kimwili? Douglas, mzee Mkristo ambaye pia ni baba, anasema: “Kwa kuwa muungwana ni kitendo, bila shaka watoto wako wataiga mitazamo na matendo yako, ya marafiki wako, na ya watoto wa marafiki wako.”

Wanyama wengi huongozwa na silika kupigana ili kuwalinda watoto wao kutokana na wanyama wengine hatari. Mtaalamu anayeshughulikia dubu anaripoti hivi: “Madubu-jike wanajulikana sana kwa kuwalinda watoto wao kutokana na chochote wanachoona kuwa hatari.” Je, haingefaa wazazi wanadamu wafanye vivyo hivyo? Ruben, anayeishi Italia, anasema: “Wazazi wangu walinisaidia kufikiri kwa kutumia Maandiko. Walinionyesha kwamba inafaa kuepuka kushirikiana na watu fulani. Mwanzoni, nilihisi hivi: ‘Eti nini? Eti siwezi kuwa na marafiki wowote?’ Lakini baada ya muda kupita nimeona kwamba hawakukosea, nami nimelindwa kwa sababu ya subira yao.”

Pia, wasaidie watoto wako washirikiane kwa ukawaida na watu ambao ni mifano mizuri ambao watawasaidia kujiwekea miradi inayofaa. Kijana mmoja mwenye furaha anayeitwa Francis ambaye amefanikiwa maishani, anakumbuka hivi: “Mama yangu alitambua kwamba mimi na ndugu zangu tulipenda kuwa peke yetu, kwa hiyo alitusaidia kwa kuwakaribisha marafiki waliokuwa na bidii katika huduma ya Kikristo ya wakati wote. Hilo lilituwezesha kuwafahamu na kuanzisha urafiki nao, papo hapo nyumbani.” Ukifanya hivyo, watoto wako wanaweza kupata marafiki wazuri hata wakiwa nyumbani.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Chunguza tabia za watu unaotaka kufanya urafiki nao

[Picha katika ukurasa wa 10]

Urafiki usio na ubinafsi huimarika licha ya umri na malezi tofauti