Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sote Tunahitaji Marafiki

Sote Tunahitaji Marafiki

Sote Tunahitaji Marafiki

“Rafiki ni mtu ambaye unaweza kuzungumza naye kwa uhuru kuhusu jambo lolote, unayeweza kumpigia simu wakati wowote.”—Yaël, Ufaransa

“Rafiki hufahamu unapohuzunika, naye hujiweka katika hali yako.”—Gaëlle, Ufaransa

“YUKO rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu zaidi kuliko ndugu.” (Methali 18:24) Utu wa mwanadamu haujabadilika tangu maneno hayo yalipoandikwa katika Biblia yapata miaka 3,000 iliyopita. Urafiki ni muhimu kwa mwanadamu kama vile chakula na maji yalivyo muhimu kwa mwili. Hata hivyo, si rahisi kwa wengi kupata marafiki. Watu wengi ni wapweke. Katika kitabu chao In Search of Intimacy, Carin Rubenstein na Phillip Shaver wanasema hivi: “Si vigumu kutambua baadhi ya visababishi.” Wanasema kwamba visababishi vya upweke vinatia ndani, “kuhamahama mara nyingi,” kuishi katika “majiji yenye uhalifu mwingi na yenye watu wasiojali,” na “kutazama televisheni na video badala ya kuchangamana na watu.”

Vilevile, maisha ya leo humaliza wakati na nguvu zetu. Katika kitabu chake Among Friends, Letty Pogrebin anaandika hivi: “Leo, watu ambao mkaaji wa jijini hukutana nao kwa juma moja ni wengi kuliko watu ambao mkaaji wa kijijini wa karne ya kumi na saba alikutana nao kwa mwaka mmoja au hata maishani mwake.” Kwa kuwa mtu anaweza kufahamiana na watu wengi sana, huenda ikawa vigumu kuwakazia fikira watu fulani hususa kwa muda mrefu ili kusitawisha na kudumisha urafiki wa karibu.

Hali za kijamii zinabadilika haraka hata mahali ambapo watu hawakuwa na shughuli nyingi. Ulla, anayeishi Ulaya Mashariki, anasema: “Zamani, tulikuwa na uhusiano wa karibu sana na marafiki wetu. Lakini sasa wengi wao wanajishughulisha sana na kazi zao au mambo yao. Kila mtu ana shughuli nyingi nyakati zote, nasi tunahisi kwamba urafiki wetu unavunjika pole kwa pole.” Kwa kuwa kuna shughuli nyingi sana leo, ni rahisi kupuuza marafiki wetu.

Ingawa hivyo, bado tunahitaji sana marafiki. Vijana hasa wana uhitaji huo. Yaël, aliyetajwa juu, anasema hivi: “Unapokuwa kijana, unahitaji kuhisi kwamba unahitajiwa na kukubaliwa na wengine, unahitaji kuwa na uhusiano wa karibu na mtu fulani.” Tuwe vijana au wazee, sote tunahitaji kuwa na urafiki wa karibu na wenye kufurahisha. Ijapokuwa hilo si rahisi, kuna mengi tunayoweza kufanya ili kupata na kudumisha marafiki wa kweli. Makala zinazofuata zinazungumzia jambo hilo.