Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vipi Akikataa?

Vipi Akikataa?

Vijana Huuliza . . .

Vipi Akikataa?

MWANZONI ulimwona kuwa rafiki tu. Lakini akaanza kukuvutia kwa njia ya pekee. Huenda ulivutiwa na mwenendo wake mzuri au jinsi alivyotabasamu alipokuwa akiongea nawe. Vyovyote vile, muda ulipita naye hakuonyesha kwamba anakupenda. Hivyo, uliamua kumuuliza ikiwa angetaka muanze uchumba. Huenda ulivunjika moyo sana alipokuambia kwa fadhili lakini kwa busara kwamba hataki. *

Bila shaka hilo litakuumiza. Hata hivyo, badala ya kuruhusu hali hiyo ikulemee, jitahidi kuwa na maoni yanayofaa. Ni kweli kwamba kijana fulani hataki kuanzisha uhusiano nawe. Hata hivyo, uamuzi wake hauathiri hadhi yako, wala haumaanishi kwamba wengine hawakupendi na kukuheshimu. Kwa hakika, huenda uamuzi wake unategemea hasa miradi na mapendezi yake ya kibinafsi wala si hali yako.

Ikiwa wewe ni Mkristo, yaelekea pia unakumbuka kwamba ‘Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’ (Waebrania 6:10) Sonja * anasema hivi: “Bado wewe ni mwenye thamani. Yehova anakuthamini hata ukiwa mseja.” Kwa kuwa Aliye Juu Zaidi, na vilevile watu wengine bado wanakuthamini, hupaswi kuacha kujistahi.

Huenda ukahisi hufai na kwamba huwezi kuwa mwenzi mzuri wa ndoa. Lakini hata kama kwa sasa ‘hustahili’ machoni pa kijana huyo, hilo halimaanishi kwamba ‘hustahili kabisa’ machoni pa mtu mwingine. (Waamuzi 14:3) Hivyo basi, badala ya kuhisi kuwa jitihada zako zimegonga mwamba, tambua kwamba umefanikiwa kutimiza jambo moja muhimu: Umejua kwamba kijana huyo hafai kuwa mume wako. Kwa nini tuseme hivyo?

Je, Kijana Huyo Anakufaa?

Biblia huwaamuru waume wawe “wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Waefeso 5:28) Pia huwaamuru waume wawe ‘wakiwapa heshima’ wake zao. (1 Petro 3:7) Katika kisa hiki, huenda kijana huyo anakuona kuwa rafiki. Lakini anapokataa kuanzisha uhusiano nawe, anaonyesha kwamba kwa sasa hayuko tayari kukupenda na kukuheshimu ukiwa mke wake. Alikuwa na haki ya kufanya uamuzi huo. Jiulize hivi: Ikiwa anahisi hivyo, je, kweli atafaa kuwa mume wako? Wazia jinsi ambavyo ungehuzunika kwa kuolewa na mume asiyekupenda na kukuthamini kama vile Biblia inavyotushauri!

Ingefaa pia umchunguze kijana huyo kwa uangalifu, hasa wakati huu ambapo hakuna uwezekano wa kuwa na uhusiano naye. Nyakati nyingine watu hupumbazwa na upendo usio wa kweli nao hukosa kuona kasoro za kibinafsi na za kiroho ambazo wengine huona kwa urahisi. Kwa mfano, je, alikwisha kutambua kwamba umeanza kupendezwa naye, au alichochea hisia zako kimakusudi kwa kuendeleza uhusiano wake pamoja nawe? Ikiwa alikuwa akichochea hisia zako kimakusudi, je hilo halionyeshi kwamba hayuko tayari kuwa mume Mkristo anayejali na mwenye fadhili? Ikiwa ndivyo, hata kama uamuzi wake unakuhuzunisha, ni vema kwamba umejua ukweli wa mambo.

Marcia alivutiwa wakati kijana fulani alipoanza kupendezwa naye. Alipomwuliza kuhusu nia yake, kijana huyo alimweleza kwamba hakutaka kuwa na uhusiano naye. Aliwezaje kukabiliana na hali hiyo yenye kuvunja moyo? Anasema hivi: “Niliweza kushughulikia hali hiyo vizuri kwa kutumia akili badala ya kuongozwa na hisia.” Kutafakari yale ambayo Biblia husema kuhusu waume, kulimsaidia kutambua kwamba kijana huyo hastahili kuwa mume wake. Hilo lilimsaidia Marcia kukabiliana na huzuni yake.

Andrea pia alitendewa vivyo hivyo na kijana fulani. Alichunguza jinsi kijana huyo alivyomtendea, na muda si muda akagundua kwamba hakuwa mkomavu. Alitambua kwamba kijana huyo hakuwa tayari kufunga ndoa, naye alimshukuru Yehova kwa kumsaidia kuona mambo waziwazi. Anasema hivi: “Ninaamini kwamba Yehova anaweza kukulinda dhidi ya mambo ambayo yanaweza kukudhuru, lakini ni lazima umtumaini.” Hata hivyo, kijana anaweza kuwa na maadili mazuri na bado awe na sababu nzuri ya kukataa kuanzisha uhusiano nawe. Vyovyote vile, utakabilianaje na huzuni ya kukataliwa?

Unachoweza Kufanya Kuhusu Huzuni Yako

Huenda ukahitaji muda ili kukubali jinsi hali ilivyo. Kwa kuwa ulichukua muda mrefu kukuza hisia zako kumwelekea, itachukua muda mrefu kubadili hisia hizo. Huwezi kuacha kumpenda mtu mara moja. Mara kwa mara, huenda hisia hizo zikakulemea! Uwe na subira. Baada ya muda utashinda hisia hizo. Hata hivyo, ukitaka kushinda hali hiyo haraka, epuka mambo ambayo huchochea hisia hizo.

Kwa mfano, epuka kuchanganua maneno uliyotumia na jinsi ulivyotenda wakati ulipokuwa ukimweleza jinsi unavyohisi. Usipodhibiti mawazo hayo, huenda ukaanza kufikiri kwamba kijana huyo hakumaanisha alichosema, au kwamba unaweza kufanikiwa ukijaribu mbinu tofauti. Kubali kwamba huwezi kubadili maoni yake. Hata kama ungetumia njia gani yaelekea jibu lake lingekuwa lilelile.

Kuwazia mambo yasiyowezekana ni mtego mwingine. Unaweza kuwazia maisha ya raha mustarehe ukiwa pamoja naye. Huenda ukahisi kwamba mawazo hayo yanafariji. Hata hivyo, tambua kuwa mawazo hayo si halisi. Yanapotoweka, wewe hurudia hali yako ya kawaida na huzuni yako hurejea. Usipojitahidi sana kukomesha mawazo hayo, hali hiyo inaweza kuendelea kwa muda mrefu.

Jitahidi uwezavyo kuepuka kuwazia mambo yasiyowezekana. Mawazo hayo yakianza kuingia akilini mwako, jaribu kutembea-tembea. Fanya kazi fulani ambayo itakusaidia kuondoa mawazo hayo akilini. Kazia akilini mambo yanayojenga badala ya yale yanayovunja moyo. (Wafilipi 4:8) Mwanzoni huenda ikawa vigumu kufanya hivyo, lakini hatimaye utafanikiwa na kuwa na utulivu.

Rafiki zako wa karibu wanaweza kukusaidia. (Methali 17:17) Hata hivyo, Sonja anatoa tahadhari hii: “Haifai kuwa tu na marafiki waseja wa rika lako, na ambao wana tamaa ya kufunga ndoa. Unahitaji marafiki wanaokuzidi umri, ambao watakusaidia kushughulikia mambo vizuri.” Isitoshe, kumbuka kwamba kuna mtu mwingine ambaye anaweza kukusaidia sana kukabili huzuni yako.

Yehova Ni Rafiki Anayeweza Kukutegemeza

Hapo kale, mtu mmoja mwaminifu alipokuwa amevunjika moyo, alimwomba Yehova msaada. Matokeo yalikuwaje? Yeye aliandika hivi: “Mahangaiko ya moyo wangu yanapozidi, wewe wanifariji na kunifurahisha.” (Zaburi 94:19, Biblia Habari Njema) Yehova atakufariji na kukutegemeza iwapo utamwomba na kumtumaini. Andrea alifanya hivyo. Anasema hivi: “Sala ni muhimu sana unapojitahidi kushinda huzuni yako na kuendelea na maisha kama kawaida.” Pia Sonja anasema hivi kuhusu sala: “Hukusaidia kujiheshimu hata kama wengine hawapendezwi nawe au wanakukataa.”

Hakuna mwanadamu anayeweza kufahamu kabisa jinsi unavyohisi. Hata hivyo, Yehova anakuelewa vizuri. Aliumba wanadamu wakiwa na tamaa ya kuonyeshana upendo ndani ya kifungo cha ndoa. Anafahamu jinsi hisia za mahaba zilivyo na nguvu, naye anajua jinsi ya kuzidhibiti. Anaweza kukusaidia kushinda huzuni kubwa unayokabili, kwani 1 Yohana 3:20 husema hivi: “Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua mambo yote.”

Dumisha Usawaziko

Ijapokuwa ndoa yaweza kuleta furaha, hiyo si njia pekee ya kupata furaha. Shangwe haipatikani tu kwa wale ambao wamefunga ndoa. Watumishi wote wa Yehova ni wenye shangwe. Useja una faida fulani ambazo wale waliofunga ndoa hawawezi kufurahia. Hawakabili ile “dhiki katika mwili wao” inayotajwa katika 1 Wakorintho 7:28. Dhiki hiyo humaanisha mfadhaiko ambao wenzi wote wa ndoa hukabili. Waseja wana uhuru zaidi na ni rahisi kwao kumtumikia Yehova. Ndiyo sababu Biblia husema hivi: “Yeye . . . anayeufungisha ndoa ubikira wake anafanya vema, lakini yeye asiyeufungisha ndoa atafanya vema zaidi.” (1 Wakorintho 7:38) Hata kama unatamani sana kufunga ndoa, kutafakari mafundisho hayo ya Biblia kutakuwezesha kudumisha usawaziko wako na kufurahia sana hali yako ya sasa.

Huenda rafiki zako wanaokujali wakasema hivi: “Usijali, siku moja utapata mwenzi mzuri sana.” Na ni kweli kwamba kukataliwa hakumaanishi kwamba hutapata mwenzi kamwe. Hata hivyo, mwanamke Mkristo anayeitwa Candace anasema hivi: “Mimi humtumaini Yehova. Sitazamii anipe mume ili niwe na furaha. Lakini najua kwamba atanisaidia kwa njia yoyote ile ili nifanikiwe kukabiliana na hali hiyo.” Maoni hayo yanayofaa yalimsaidia kukabiliana na hali wakati mwanamume mmoja alipokataa kumchumbia.

Katika ulimwengu tunamoishi, mara nyingi jitihada za kuanzisha uchumba hazifanikiwi. Lakini ndoa nyingi pia hazifanikiwi. Ukimtumaini Yehova na kufuata mashauri anayotoa, atakuwezesha kushinda huzuni yako na kupata shangwe. Unaweza kufurahia hali kama ile ya Mfalme Daudi aliyeandika hivi: “Ee Yehova, tamaa yangu yote iko mbele zako, wala kuugua kwangu hakujafichwa mbele zako. Kwa maana nilikungojea wewe, Ee Yehova; wewe mwenyewe ukanijibu, Ee Yehova Mungu wangu.”—Zaburi 38:9, 15.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Makala “Vijana Huuliza . . . Nitamwambiaje Jinsi Ninavyohisi?” (Oktoba 22, 2004) ilieleza kwamba katika jamii fulani huenda mwanamke asiruhusiwe kumweleza mwanamume kwamba anampenda. Ijapokuwa Biblia haimzuii mwanamke kufanya hivyo, inawahimiza Wakristo waepuke kuwakwaza wengine. Hivyo, mwanamke anayetaka kupata baraka za Mungu huzingatia shauri la Biblia anapofikiria kuanzisha uhusiano na mwanamume fulani.—Mathayo 18:6; Waroma 14:13; 1 Wakorintho 8:13.

^ fu. 5 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kubali msaada kutoka kwa Mungu