Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Upole Ni Udhaifu?

Je, Upole Ni Udhaifu?

Maoni ya Biblia

Je, Upole Ni Udhaifu?

“Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.”—2 TIMOTHEO 2:24.

HISI yetu ya kugusa husitawi muda mrefu kabla hatujazaliwa. Tunapozaliwa sisi hutamani sana kupapaswa kwa wororo na mama zetu. Tukiwa wachanga, tamaa yetu ya kutabasamu, uwezo wa kusitawisha hisia zetu, na tamaa yetu ya kujifunza kuwasiliana, hutegemea sana upendo ambao wazazi wetu hutuonyesha.

Hata hivyo, Biblia ilitabiri kwamba katika siku za mwisho watu watakuwa “wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili.” Sifa zinazohusiana na upole kama vile fadhili na huruma zingekosekana sana kwa kuwa watu wangekuwa “wenye kujipenda wenyewe,” na vilevile “wakali, wasiopenda wema.”—2 Timotheo 3:1-3.

Watu wengi leo huona inafaa kuwa mkali na kutokuwa na huruma. Wanasema kwamba upole ni udhaifu. Je, ndivyo ilivyo?

Watu Wapole Lakini Wenye Nguvu

Yehova Mungu hufafanuliwa kuwa “mtu wa vita anayetenda kiume.” (Kutoka 15:3) Yeye ndiye Chanzo cha nguvu zote. (Zaburi 62:11; Waroma 1:20) Hata hivyo, nguvu za Yehova hazikumzuia kuwa “mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema,” alipokuwa akimbariki yule mtu mwaminifu Ayubu. (Yakobo 5:11) Yehova alipokuwa akieleza kuhusu uhusiano mwororo kati yake na taifa la Israeli, alilinganisha hisia zake na za mama anayenyonyesha ambaye humhurumia “mwana wa tumbo lake.”—Isaya 49:15.

Yesu pia alikuwa mwenye nguvu na mpole. Aliwashutumu vikali viongozi wa kidini wanafiki wa wakati huo. (Mathayo 23:1-33) Hata aliwafukuza watu wenye pupa waliokuwa wakibadilisha pesa hekaluni. (Mathayo 21:12, 13) Lakini je, Yesu alikosa kuwaonyesha watu huruma kwa sababu alichukia ufisadi na pupa? La hasha! Yesu alikuwa mpole. Hata alijilinganisha na kuku ambaye “hukusanya vifaranga chini ya mabawa yake.”—Luka 13:34.

Tuwe Wakali au Wapole?

Wakristo wa kweli wanahimizwa kumwiga Kristo kwa kuvaa “utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu.” (Waefeso 4:20-24) Sawa tu na nyoka ambaye huondoa ngozi yake, tunashauriwa ‘tuvue utu wa zamani pamoja na mazoea yake.’ (Wakolosai 3:9) Hata hivyo, nyoka akiisha kuondoa ngozi yake, ngozi yake mpya huzeeka na inambidi aiondoe tena. Lakini sisi tunaambiwa daima tujivike “upendo mwororo wenye huruma, fadhili, . . . na ustahimilivu.” (Wakolosai 3:12) Hivyo, tunapaswa kuwa wapole daima.

Kuwa na sifa nyororo hakumaanishi kwamba sisi ni dhaifu. Badala yake, ili tuwe na sifa hizo tunahitaji kuwa na “uwezo katika mtu [tuliye] kwa ndani [tukiwa] na nguvu kupitia roho [ya Yehova].” (Waefeso 3:16) Kwa mfano, Lee anasema hivi: “Muda fulani uliopita nilikuwa mjeuri na mwovu. Hata sura yangu iliwashtua watu kwani nilikuwa nimetoboa mwili wangu na kuvaa vito. Nilitaka kupata pesa nyingi sana na nilitumia usemi mchafu na kufanya ujeuri ili kutimiza lengo langu. Sikuwa na huruma.” Hata hivyo, Lee alianza kujifunza Biblia na mfanyakazi mwenzake naye akamjua na kumpenda Yehova Mungu. Amevua utu wake wa kale na amesitawisha sifa ya kujizuia. Sasa yeye anawapenda watu na huonyesha hilo kwa kujitolea kuwasaidia kujifunza Biblia.

Wakati mmoja Paulo alikuwa “mtu mwenye dharau,” aliyefanya ujeuri ili kutimiza lengo lake. (1 Timotheo 1:13; Matendo 9:1, 2) Hata hivyo, Paulo alipofahamu na kuanza kuthamini rehema na upendo ambao Yehova Mungu na Yesu Kristo walimwonyesha, alijitahidi kuiga sifa hizo. (1 Wakorintho 11:1) Ijapokuwa Paulo alishikilia kwa uthabiti kanuni za Kikristo, alijitahidi kuwatendea wengine kwa upole. Bila shaka, Paulo aliwaonyesha ndugu zake upendo mwororo waziwazi.—Matendo 20:31, 36-38; Filemoni 12.

Kusitawisha Upole

Kisa cha Lee na cha mtume Paulo huonyesha kwamba mtu hahitaji kuwa dhaifu ili awatendee wengine kwa upole. Badala yake, mtu anahitaji nguvu nyingi ili ageuze akili na matendo yake na kupambana na tamaa ya kimwili ya ‘kulipa uovu kwa uovu.’—Waroma 12:2, 17.

Tukijifunza Neno la Mungu kwa ukawaida na kutafakari kuhusu upendo na rehema ambazo Yehova Mungu na Mwana wake, Yesu Kristo wametuonyesha, sisi pia tunaweza kuwa na huruma nyororo. Tukifanya hivyo, nguvu za Neno la Mungu zitafanya moyo wetu uwe mwororo. (2 Mambo ya Nyakati 34:26, 27; Waebrania 4:12) Hata kama tulikuwa na malezi au maisha magumu, tunaweza kujizoeza kuwa ‘wapole kwa wote.’—2 Timotheo 2:24.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Baba mzuri huwatendea watoto wake kwa upole