Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kuteseka Asanteni sana kwa makala yenye kichwa “Vijana Huuliza . . . Kwa Nini Mungu Anaruhusu Tuteseke?” (Machi 22, 2004) Nina umri wa miaka 14, na hivi majuzi babu na shangazi yangu niliowapenda sana walikufa. Ninajua Mungu hapaswi kulaumiwa kwa vifo vyao. Shetani ndiye wa kulaumiwa, naye ana kipindi kifupi sana kilichobaki. Makala hiyo ilinifariji sana. Tafadhali endeleeni kuandika makala kama hizo. Ninawashukuru tena kutoka moyoni.

B. B., Marekani

Hivi majuzi msichana niliyetaka kuoa alikufa katika msiba wa barabarani. Huo ulikuwa msiba mbaya sana kwangu, kwa kutaniko, na hasa kwa wazazi wake. Ninamshukuru sana Yehova kwa kunisaidia kuvumilia huzuni yangu. Nami ninawashukuru sana kwa makala yenye kichwa “Kwa Nini Mungu Anaruhusu Tuteseke?” Niliipata kwa wakati unaofaa.

I. D., Ujerumani

Kwanza sikutaka kusoma makala hiyo. Nilifikiri ilihusu tu mambo yenye kuhuzunisha. Miaka miwili iliyopita ndugu yangu mkubwa alikufa kutokana na ugonjwa fulani, na bado ninahuzunika. Lakini makala hiyo ilinikumbusha kwamba Yehova ndiye chanzo cha vitu vyema. Maumivu yangu yalipungua haraka, nami nilitiwa moyo sana kuendelea kuishi katika ulimwengu huu wenye msukosuko.

S. H., Japani

Sukari Watu kadhaa wameniambia kwamba ile makala yenye kichwa “Sukari Ni Muhimu kwa Uhai” (Machi 22, 2004) ilipendekeza watu watumie dawa fulani kutibu magonjwa mbalimbali kutia ndani ugonjwa wa kansa. Sichambui makala yenu, hata hivyo sielewi kinachowafanya watu fulani waitumie kujifaidi kifedha au kupendekeza maoni yao.

P. K., Australia

“Amkeni!” linajibu: Makala yenye kichwa “Sukari Ni Muhimu kwa Uhai” iliripoti tu mambo ambayo wanabiolojia wamegundua kuhusu umuhimu wa sukari katika afya. Makala hiyo haikukusudiwa kupendekeza dawa yoyote. Gazeti la “Amkeni!” linapozungumzia mambo ya afya, halipendekezi wasomaji watumie matibabu fulani. Kila Mkristo anapaswa kuhakikisha matibabu anayopata yanaonyesha kwamba ana utimamu wa akili na hayapingani na kanuni za Biblia.

Magonjwa Yanayosababishwa na Maziwa Kwa miaka kadhaa nimekuwa na dalili za ugonjwa uliotajwa katika makala yenye kichwa “Magonjwa Yanayosababishwa na Maziwa.” (Machi 22, 2004) Kwa hiyo nilipochunguzwa iligunduliwa kwamba nina ugonjwa unaosababishwa na maziwa. Nilipomwonyesha daktari makala hiyo, alisema kwamba ilikuwa imefanyiwa utafiti sana, naye akaniambia niwashukuru kwa kuandika makala nzuri sana. Alisema kwamba hafikiri amewahi kusoma Amkeni!

E. S., Ujerumani

Kunywa Kupita Kiasi Asanteni sana kwa makala yenye kichwa “Maoni ya Biblia: Je, Ni Kosa Kunywa Kupita Kiasi?” (Machi 8, 2004) Sasa ninatambua kwamba matatizo yangu na mke wangu yalisababishwa na kunywa kileo, na kwamba nimepoteza pesa nyingi sana kutokana na zoea hilo. Siku hizi mimi hunywa mara chache sana.

G. K., Tanzania

Fumbo la Kujaza Maneno Mimi hufurahia sana kujibu maswali katika fumbo la kujaza maneno ambalo huchapishwa katika Amkeni! Sehemu hiyo huelimisha. Mwanzoni nilihitaji kutafuta jibu sahihi katika Biblia. Siku hizi mimi hufanya hivyo mara chache sana. Kujifunza Biblia kumenisaidia kufanya hivyo. Mafumbo hayo yalinichochea niwe na funzo la kibinafsi la Biblia!

W. K., Poland

“Amkeni!” linajibu: Mafumbo ya kujaza maneno ambayo hupatikana katika “Amkeni!” la Kiingereza hubadilishwa katika lugha nyingine na maswali ya Biblia yenye kichwa “Je, Wajua?”