Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kazi ya Udaktari Itakuwaje Wakati Ujao?

Kazi ya Udaktari Itakuwaje Wakati Ujao?

Kazi ya Udaktari Itakuwaje Wakati Ujao?

WATU wanapochanganua wakati ujao wa madaktari, wao hufikiria ikiwa maendeleo ya kiteknolojia yatapunguza kazi fulani za madaktari na kuwawezesha kutumia muda mwingi zaidi kuwashughulikia wagonjwa. Bila shaka, hali ya wakati ujao ya madaktari inahusiana sana na wakati ujao wa wanadamu kwa jumla. Vitabu viwili vya Biblia vinavyozungumzia jambo hilo vinaeleza kuhusu maisha ya Yesu na mitume wake. Vitabu hivyo viwili viliandikwa na daktari.

Kwa nini tupendezwe na maelezo ya daktari kuhusu maisha ya Yesu na mitume wake? Maisha ya Yesu na mitume wake yanahusianaje na hali ya wakati ujao ya madaktari na wagonjwa? Kwa nini madaktari fulani wanatazamia kwa hamu wakati ambapo kazi yao haitahitajiwa tena?

Madaktari wengi huchunguza mambo kwa uangalifu sana. Luka, ambaye huitwa “tabibu mpendwa,” ndiye aliyeandika vitabu hivyo viwili vya Biblia na kueleza mambo mengi kuhusu wagonjwa fulani walioponywa na Yesu na mitume wake. (Wakolosai 4:14) Basi, Luka anatusaidia kujibu maswali haya: Je, kweli watu hao waliponywa? Ikiwa ndivyo, hilo linawahusuje madaktari na wagonjwa?

Uchunguzi wa Tabibu

Luka angeweza kuhakikisha kwamba maponyo hayo ya kimuujiza yalitukia kwa kuwahoji watu walioshuhudia matukio hayo. Isitoshe, alisafiri sana na mtume Paulo. Inaonekana Luka alimwona Paulo akiwaponya watu kadhaa. Tunapochunguza masimulizi ya tabibu huyo kuhusu maponyo mawili kati ya hayo, ona jinsi alivyoeleza mambo mengi.

Luka anataja wakati, tarehe, na mahali pa tukio hili: Ilikuwa katikati ya usiku, katika siku ya kwanza ya juma. Wakristo fulani walikuwa wamekusanyika katika chumba cha ghorofa ya tatu huko Troa, katika mkoa wa Roma wa Asia. (Matendo 20:4-8) Simulizi hilo linasema hivi: “Kijana fulani anayeitwa Eutiko, . . . akalala usingizi mzito huku Paulo akiendelea kuongea, naye akalemewa na usingizi, akaanguka chini kutoka ghorofa ya tatu akaokotwa akiwa amekufa.” Kisha kwa nguvu za Mungu, Paulo akaponya majeraha ya kijana huyo na kumfufua. Baada ya kula, “wakamchukua huyo mvulana akiwa hai wakafarijiwa kupita kiasi.”—Matendo 20:9-12.

Pia Luka anaripoti kwamba alikuwa na Paulo huko Malta. Walikuwa wamekaribishwa nyumbani kwa Publio aliyekuwa “mkuu” wa kisiwa hicho, wakati Paulo alipofanya muujiza mwingine. Alimponya mtu ambaye alikuwa na ugonjwa hatari sana, hasa wakati huo ambapo hakukuwa na dawa za kuua viini. Luka anaripoti hivi: “Baba ya Publio alikuwa amelala akitaabishwa na homa na ugonjwa wa kuhara damu, na Paulo akaingia alimokuwa na kusali, akaweka mikono yake juu yake akamponya. Baada ya jambo hilo kutukia, watu wale wengine kisiwani waliokuwa na magonjwa wakaanza pia kuja kwake na kuponywa.”—Matendo 28:7-9.

Kilichomsadikisha Tabibu Huyo

Luka aliandika masimulizi hayo ya kitabu cha Matendo wakati ambapo wasomaji wa habari hizo wangeweza kuchunguza maponyo hayo kwa kuzungumza na wahusika. Luka aliandika hivi kuhusu masimulizi yanayopatikana katika kitabu cha Luka: “Nimefuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi . . . ili upate kujua kabisa uhakika wa mambo.” (Luka 1:3, 4) Mambo ambayo tabibu huyo aliona na kuchunguza yalimsadikisha kwamba Yesu alifundisha kweli. Miujiza yake ilikuwa sehemu ya mafundisho hayo, na ilitoa msingi wa kuamini unabii wa Biblia unaosema kwamba Mungu atamaliza magonjwa. (Isaya 35:5, 6) Kwa kuwa Luka alikuwa daktari aliyezoea kushughulika na watu wanaoteseka, hapana shaka alitazamia kwa hamu wakati ambapo kazi yake ya udaktari haingehitajiwa tena. Je, tumaini hilo linakuvutia?

Watu wote wanaompenda Mungu wana tumaini hilo, hata iwe wanaishi wapi. Biblia inaahidi kwamba chini ya Ufalme wa Mungu “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) Leo, madaktari wengi wamekata kauli kwamba kuna sababu nzuri za kuamini ahadi za Biblia.

‘Nilivutiwa Sana’

Dakt. Jon Schiller, wa Amerika Kaskazini, anasema hivi: “Sawa na watu wengine, nilisomea udaktari ili niwasaidie wagonjwa. Tumaini la kuwa na ulimwengu usio na magonjwa lilinivutia sana. Nilianza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova baada ya kumaliza masomo ya chuoni kuhusu historia ya ustaarabu wa Magharibi. Masomo hayo yalinionyesha kwamba dini zimesababisha matatizo mengi sana na niliona kwamba wanadini walikuwa wakitumia Biblia kwa unafiki. Hivyo nilijiuliza, ‘Biblia inasema nini hasa?’

“Nilipoenda kwenye Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova, nilivutiwa kwanza na watu wenye urafiki waliotofautiana sana na wengi wa marafiki wangu. Shahidi mmoja alinijia na kujitolea kunitembelea ili kuzungumza Biblia pamoja nami. Kilichonivutia hasa ni kwamba alinijibu maswali yangu akitumia Biblia.

“Kadiri umri wangu unavyozidi, ndivyo ninavyothamini kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova. Mtu anapoanza kufanya kazi ya udaktari yeye hutarajia kutimiza mengi. Lakini mimi huwaona watu wengi ambao wamekata tamaa kwa kutotimiza mengi maishani. Nafikiri jambo bora zaidi katika maisha ya Shahidi wa Yehova ni lile tumaini tulilo nalo la wakati ujao na kuwa na kusudi maishani. Tuwe madaktari, mafundi wa mitambo, au mabawabu, tunajua kwamba tunapomtumikia Mungu sisi hutimiza jambo muhimu sana, kwani sisi humfanyia Yehova kazi fulani. Hilo hutupa uradhi.”

“Kutumia Kanuni za Biblia Kuliboresha Familia Yetu”

Dakt. Krister Renvall, ni daktari huko Ufini, naye hufurahia kuzungumza na watoto. Anasema hivi: “Wakati mmoja nilizungumza na msichana mwenye umri wa miaka 12, ambaye alikuwa akikaribia kufa kutokana na kansa. Msichana huyo alinipa kitabu Amani ya Kweli na Usalama wa Kweli—Kutoka Chanzo Gani? * Nilivutiwa na maelezo yake kuhusu imani yake alipokuwa akikaribia kufa kutokana na ugonjwa huo, lakini sikupata nafasi ya kusoma kitabu alichonipa. Wakati huo nilikuwa na kazi nyingi sana katika kliniki moja huko Helsinki hivi kwamba familia yangu iliathiriwa.

“Hata hivyo, baada ya muda fulani kupita, mke wangu alianza kusoma kitabu hicho. Alisadikishwa mara moja kwamba yale aliyokuwa akisoma ni kweli. Shahidi mmoja wa Yehova alimtembelea na kuanza kujifunza naye Biblia. Mwanzoni, mke wangu aliogopa kunieleza jambo hilo. Lakini aliponieleza, nilimwambia hivi, ‘Ikiwa itasaidia familia yetu, basi ni sawa.’ Nilianza kushiriki katika funzo hilo. Kutumia kanuni za Biblia kuliboresha familia yetu na kubadili maoni yetu kuhusu maisha. Nilifurahi sana kujifunza kuhusu tumaini la ulimwengu usio na magonjwa; sikushangaa kujua kwamba Mungu anakusudia jambo hilo kwa ajili ya wanadamu. Muda mfupi baadaye, mimi na mke wangu tulibatizwa, kisha washiriki wengine wote wa familia wakabatizwa. Ijapokuwa yule msichana mdogo niliyezungumza naye alikufa, imani yake ingalipo.”

Kwa kuwa madaktari wanazidi kukabili mfadhaiko katika ulimwengu huu unaobadilika haraka, wanastahili pongezi kwa kujitahidi sana kuwasaidia wagonjwa. Lakini, hivi karibuni wanadamu watakabili mabadiliko makubwa zaidi. Leo madaktari wengi wanatazamia kwa hamu ulimwengu usio na magonjwa unaoahidiwa na Neno la Mungu! (Ufunuo 21:1-4) Hilo ni jambo unalopaswa kujichunguzia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 17 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10, 11]

“NILITAMBUA KWAMBA MAISHA YANA KUSUDI”

“Nilipokuwa nikiwahudumia wanafunzi walemavu, nilitambua kwamba wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova ni tofauti. Ilionekana kwamba waliwashughulikia vizuri zaidi watoto wao walemavu kuliko wazazi wengine. Pia nilitambua kwamba wana elimu bora ikilinganishwa na kazi wanazofanya. Imani yao ilinivutia. Imani yangu ilikuwa imedhoofishwa sana na walimu wa nadharia ya mageuzi. Hata hivyo, masomo yangu ya tiba yalikuwa yamenifanya nistaajabie sana maajabu ya uhai.

“Wakati huohuo, nilitambua kwamba sijui kuwalea watoto wangu. Sikujua mipaka ninayopaswa kuwawekea, mambo ninayopaswa kuwachochea wafanye, au jinsi ya kufanya maisha yao yawe na kusudi. Pia, maisha yangu hayakuwa na kusudi. Nilisali ili kupata msaada.

“Wakati huo, Mashahidi wa Yehova waliniletea gazeti linalozungumzia jinsi ya kuwarekebisha na kuwatia watoto nidhamu kwa upendo. Kanuni za Biblia zilizoelezwa katika gazeti hilo zilinisaidia sana, kwa hiyo nilikubali kujifunza Biblia pamoja nao. Nilipojifunza sababu iliyomfanya Yehova aanzishe uhai na umuhimu wa kifo cha Yesu, nilitambua kwamba maisha yana kusudi. (Yohana 3:16; Waroma 5:12, 18, 19) Nilikuwa nimepotoshwa na nadharia ya mageuzi. Nilifarijika nilipojifunza kwamba Mungu hakukusudia wanadamu wawe wagonjwa na wafe! Sasa ninapata uradhi ninapowafundisha watu wanyoofu jinsi Mungu atakavyoponya magonjwa yote hivi karibuni.”

[Picha]

Helena Bouwhuis alikuwa akiwatibu wanafunzi wa shule huko Uholanzi

[Picha katika ukurasa wa 9]

Luka, ambaye alikuwa tabibu na mwandishi wa Biblia, aliandamana na Paulo wakati mtume huyo alipomponya baba ya Publio na kumfufua Eutiko

[Picha katika ukurasa wa 10]

Dakt. Jon Schiller, Marekani

[Picha katika ukurasa wa 10]

Dakt. Krister Renvall, Ufini