Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Musa Nimetoka tu kusoma mfululizo wenye kichwa “Musa—Mtu Halisi au wa Hadithi?” (Aprili 8, 2004) Sikutazamia kupata habari nyingi sana zinazokanusha madai ya wasomi kwamba Musa alikuwa mtu wa hadithi tu! Nina hakika kwamba watu wanyoofu wakisoma sehemu moja tu ya mfululizo huu wataimarisha imani yao katika Yehova.

Y. M., Urusi

Wakati Asanteni sana kwa makala yenye kichwa “Usichelewe!” (Aprili 8, 2004) Kutumikia kutaniko, kuwa kichwa cha familia, na kufanya kazi ya kimwili, huhitaji wakati mwingi sana. Nimetumia madokezo mengi yaliyotokea katika magazeti, lakini inapendeza kuona makala nyingine kama hiyo. Nilipendezwa hasa na sentensi iliyosema, “Muumba wetu alikusudia tutunze wakati.” Hilo liliweka mambo wazi. Tafadhali endeleeni kuandika makala kama hizo zilizo na habari zenye kunufaisha.

J. S., Marekani

Mara nyingi mimi huahirisha mambo hadi dakika ya mwisho, na ingawa huwa sichelewi, mimi hulala kupita kiasi. Nimejihatarisha mara nyingi kwa sababu ya kuharakisha. Makala hiyo ilinisaidia kutopangia kufanya mambo mengi sana kwa wakati mfupi.

Y. W., Japani

Nina miaka 18. Kwa kuwa mimi ni mtumishi wa wakati wote na bado niko shuleni, mimi huwa na shughuli nyingi kila wakati. Ninahitaji wakati wa kuhubiri, wa kufanya kazi za shule, na wa kuwa na funzo la kibinafsi. Makala hiyo ilinisaidia kupanga mambo vizuri ili nifike kwenye mikutano ya Kikristo, shuleni, na katika shughuli nyingine kwa wakati. Sitaki kuchelewa tena. Asanteni sana!

J. H., Marekani

Ilikuwa kawaida kwangu kuchelewa kufika kwenye mikutano. Nilisali kuhusu jambo hilo na Yehova amejibu sala yangu. Nilijaribu kutumia madokezo yaliyo katika makala hiyo na kufaulu. Sasa sichelewi. Ninatambua kwamba upendo ndio humfanya mtu afike kwa wakati.

J. A., Nigeria

Mazoea Mabaya Ilinibidi kuandika ili niwashukuru kwa ajili ya makala yenye kichwa “Maoni ya Biblia: Je, Mtu Anaweza Kuacha Mazoea Mabaya?” (Aprili 8, 2004) Kwa muda fulani nimekuwa nikikabiliana na tatizo la kuongeza uzito. Nimekuwa nikijaribu kupunguza uzito lakini baada ya muda ningeongeza tena. Ingawa makala hiyo haikuzungumzia kuhusu kupunguza uzito, kanuni zilizotolewa zilifaa hali yangu. Ilinisaidia kuchunguza mazoea yangu mabaya na kuona jinsi yalivyochangia kuongeza uzito. Asanteni kwa kutukumbusha kwamba Yehova anajua na anatambua matatizo tunayokabiliana nayo.

M. S., Marekani

Marundo ya Mchanga Asanteni sana kwa makala yenye kichwa “Marundo ya Mchanga Yenye Kustaajabisha Huko Poland.” (Machi 22, 2004) Kwa kuwa nimetembelea Mbuga ya Kitaifa ya Słowiński mara nyingi na kuvutiwa sana nayo, makala hiyo ilinipendeza sana. Yehova anastahili kusifiwa sana kwa kuumba vitu ambavyo hutuvutia. Makala hiyo ilinipendeza hasa kwa sababu mama yangu alizaliwa kilometa chache tu kutoka katika mbuga hiyo.

I. L., Ujerumani

Makala hiyo ilinisaidia kutambua jinsi ninavyotamani sana hali zitakazokuwa katika ulimwengu mpya wa Mungu. Ninaweza kuwazia nikiwa katika Mbuga ya Kitaifa ya Słowiński na ‘kufurahia utulivu mbali na hekaheka za jijini,’ kama makala hiyo ilivyoeleza. Sote tutaburudishwa wakati Ufalme wa Mungu utakapoitawala dunia! Asanteni sana kwa habari hiyo iliyoandikwa vizuri sana!

J. G., Poland