Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nifanyeje Mtu Akinieleza Matatizo Yake?

Nifanyeje Mtu Akinieleza Matatizo Yake?

Vijana Huuliza . . .

Nifanyeje Mtu Akinieleza Matatizo Yake?

“Kuna msichana fulani shuleni ambaye wazazi wake wanataka kutalikiana. Maksi zake zinashuka. Mara kwa mara yeye hunieleza kuhusu matatizo ya familia yao.”—Jan, ana miaka 14.

“Msichana fulani shuleni amenieleza kwamba alifanya ngono na mvulana fulani. Alipata mimba na kuitoa bila wazazi wake kujua.”—Mira, ana miaka 15.

WAZIA kwamba unazungumza na rafiki yako au mwanafunzi mwenzako. Kwa ghafula, anaanza kukueleza kuhusu tatizo fulani linalomhangaisha. Huenda anahangaikia mambo yanayowahangaisha vijana wengi kama vile mavazi, pesa, sura, marafiki, na maksi za shule. Au huenda ana matatizo mazito sana.

Hali huko Marekani huonyesha jinsi vijana walivyo na matatizo mazito. Gazeti Newsweek linasema hivi: “Taasisi za Kitaifa za Ugonjwa wa Akili zinakadiria kwamba asilimia 8 ya vijana waliobalehe na asilimia 2 ya watoto (baadhi yao wakiwa na umri wa miaka 4) wana dalili za mshuko wa moyo.” Uchunguzi mwingine ulionyesha kwamba “wasichana 97 hivi kati ya kila wasichana 1,000 walio na umri wa miaka 15 hadi 19—idadi hiyo inawakilisha wasichana milioni moja huko Marekani—hupata mimba kila mwaka. Wasichana wengi, yaani asilimia 78, hupata mimba bila kukusudia.” Isitoshe vijana wengi sana wanatoka katika familia zilizo na matatizo. Vijana wengi hudhulumiwa kimwili au kingono. Zaidi ya asilimia 50 ya wanafunzi wa shule za sekondari huko Marekani wamewahi kulewa. Vijana wengi sana wana matatizo ya kula.

Basi, haishangazi kwamba vijana wengi hutaka sana kuwaeleza wengine matatizo yao. Mara nyingi wao huwaendea vijana wenzao kwanza. Unapaswa kufanya nini kijana mwenzako akikueleza matatizo yake? Ikiwa wewe ni Mkristo, usishangae vijana wenzako wakikueleza matatizo yao. Biblia huwahimiza Wakristo wawe ‘vielelezo’ katika mwenendo na wawe na usawaziko. (1 Timotheo 4:12; Wafilipi 4:5) Hivyo, huenda vijana wenzako, kutia ndani wale ambao si Wakristo, wakakueleza matatizo yao. Unapaswa kutendaje? Vipi ukihisi kwamba matatizo hayo yanakulemea na huwezi kuyatatua?

Sikiliza kwa Makini

Biblia husema kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema.” (Mhubiri 3:7) Mara nyingi mtu aliye na matatizo anaposema nawe, inafaa kumsikiliza. Biblia hushutumu yeyote anayeziba sikio lake asisikie “kilio cha kulalamika cha mtu wa hali ya chini.” (Methali 21:13) Huenda ilimchukua rafiki yako muda mrefu kupata ujasiri wa kutosha kukueleza tatizo lake. Atazungumza nawe kwa urahisi iwapo utakuwa tayari kumsikiliza. Kijana Mkristo anayeitwa Hiram anasema hivi: “Mimi humwacha mwenzangu azungumze. Mimi humruhusu afunue moyo wake, nami humhurumia.” Vincent pia anasema hivi: “Nyakati nyingine watu hutaka tu kuongea.”

Hivyo, huenda rafiki yako hatazamii utatue matatizo yake. Labda anataka tu kusikilizwa kwa makini. Kwa hiyo, msikilize! Epuka kukengeushwa na mambo mengine au kumkatiza anapozungumza. Unaweza kumsaidia sana kwa kumsikiliza tu. Ukifanya hivyo utaonyesha kwamba unamjali.

Je, hilo linamaanisha kwamba unapaswa kukaa kimya? Hilo litategemea sana tatizo lenyewe. Kwa kawaida, unahitaji tu kusema jambo linalofaa kwa fadhili. (Methali 25:11) Kwa mfano, ikiwa rafiki yako amepatwa na msiba fulani, inafaa kuonyesha kwamba unamhurumia. (Waroma 12:15) Methali 12:25 husema hivi: “Hangaiko katika moyo wa mtu huufanya uiname, lakini neno jema huufanya ushangilie.” Huenda ukahitaji tu kumtia moyo. Mwonyeshe kwamba unatumaini atashinda tatizo lake. Kwa kusema, “Naelewa sababu inayokufanya uhisi hivyo” au “Ninahuzunika kukuona ukikabili tatizo hili” utamfanya mwenzako atambue kwamba unamjali kikweli na unataka kumsaidia.

Hata hivyo, Methali 12:18 huonya hivi: “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma.” Epuka kusema mambo kama vile, “Hilo ni tatizo dogo tu,” “Achana nalo,” au “Hilo lisikuhangaishe.” Zaidi ya hilo, epuka kupunguza uzito wa tatizo lake kwa kulifanyia utani. Ukifanya hivyo huenda mwenzako akafikiri kwamba unapuuza hisia zake.—Methali 25:20.

Vipi ikiwa huna la kusema? Uwe mnyoofu. Mweleze mwenzako kwamba hujui usemeje lakini uko tayari kumsaidia kwa njia yoyote ile. Muulize, “Ninaweza kukusaidiaje?” Bila shaka, kuna mambo unayoweza kufanya ili kumsaidia kukabili tatizo lake.—Wagalatia 6:2.

Mshauri Kama Rafiki

Utatendaje ukihisi kwamba rafiki yako anahitaji shauri? Kwa kuwa wewe ni kijana, ni wazi kwamba huna ujuzi mwingi. (Methali 1:4) Hivyo, huenda usiweze kutoa shauri linalofaa hali mbalimbali. Hata hivyo, Zaburi 19:7 husema hivi: “Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, humfanya asiye na uzoefu awe na hekima.” Ijapokuwa huna “uzoefu,” huenda unafahamu kanuni za Biblia zinazoweza kumsaidia rafiki yako. (Methali 27:9) Kwa busara, mwonyeshe baadhi ya kanuni hizo za Biblia. Ikiwa hujui kanuni za Biblia unazoweza kutumia, fanya utafiti. Kwa miaka mingi makala “Vijana Huuliza . . . ” zinazochapishwa katika gazeti hili zimetoa mashauri mengi yanayotegemea Biblia kuhusu masuala mbalimbali. Pia unaweza kupata habari zaidi katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. *

Labda itafaa kumweleza kisa chako mwenyewe. Unaweza kumpa madokezo fulani. Unaweza kumweleza jinsi ulivyotatua tatizo fulani bila kumlazimisha afuate maoni yako. (Methali 27:17) Hata hivyo, kumbuka kwamba matatizo hutofautiana. Huenda njia yako ya kutatua tatizo fulani isimfae mwenzako.

Tahadhari

Usitumie wakati mwingi sana kusikiliza matatizo ya vijana wasiomcha Yehova na wasioheshimu viwango vya Kikristo. Huenda wanakabili matatizo mengi kwa sababu ya mazoea yanayopingana na kanuni za Biblia. Ukijaribu kumsaidia mtu anayedharau shauri la Biblia, nyote wawili mnaweza kuvunjika moyo. (Methali 9:7) Isitoshe, huenda akakueleza mambo ya kipuuzi au habari chafu. (Waefeso 5:3) Hivyo, iwapo hufurahii mazungumzo hayo, mweleze rafiki yako kwa ujasiri kwamba huwezi kumsaidia au kwamba hupendezwi na mazungumzo hayo.

Uwe mwangalifu ikiwa mtu wa jinsia tofauti anataka kukueleza jinsi anavyohisi. Biblia husema kwamba moyo unaweza kuwa mdanganyifu. (Yeremia 17:9) Uhusiano wa karibu unaweza kuamsha hisia za mahaba na kuwachochea mfanye ngono.

Zaidi ya hilo, usiahidi kwamba hutamwambia mtu mwingine yeyote mambo ambayo rafiki yako anakueleza. Tambua kwamba huenda mtu anayekueleza matatizo yake anahitaji msaada zaidi ya ule unaoweza kumpa.—Methali 11:2.

Msaada wa Wengine Unapohitajika

Kwa kawaida inafaa wewe mwenyewe umtafutie rafiki yako msaada kutoka kwa wengine. Mira, aliyenukuliwa mwanzoni, alisema hivi: “Kwa kweli, sikujua jinsi ya kumsaidia mwanafunzi mwenzangu. Hivyo, nikamweleza mzee fulani kutanikoni kuhusu jambo hilo naye akanipa mashauri mazuri ili kumsaidia.” Naam, katika kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova, kuna watu wenye ujuzi wanaoweza kukusaidia. (Waefeso 4:11, 12) Mira alihimizwa na mzee huyo amtie moyo rafiki yake kuwaeleza wazazi wake kuhusu tatizo lake. Msichana huyo alifuata shauri hilo. Mira anasema hivi: “Hali yake imekuwa afadhali naye anataka kujifunza Biblia.”

Vipi Mkristo mwenzako akikueleza matatizo yake? Bila shaka, utafanya yote uwezayo kumsaidia. (Wagalatia 6:10) Ukihisi kwamba anapuuza kanuni za Yehova za adili, usisite kumwambia ‘ukweli.’ (Waefeso 4:25) Uwe mnyoofu, lakini usijione kuwa mwadilifu kupita kiasi. Kumweleza mambo waziwazi kunaonyesha kwamba wewe ni rafiki wa kweli.—Zaburi 141:5; Methali 27:6.

Katika hali kama hiyo, ni lazima umtie moyo rafiki yako kutafuta msaada kutoka kwa wazazi wake, wazee, au Wakristo wengine wakomavu. Akikawia kufanya hivyo, huenda ukalazimika kumweleza mtu mwingine ili amsaidie. (Yakobo 5:13-15) Unahitaji kuwa na ujasiri ili kufanya hivyo, lakini hatua hiyo itaonyesha kwamba unamjali rafiki yako.

Bila shaka, Yehova hakutazamii utatue matatizo ya kila mtu. Hata hivyo, usivunjike moyo mtu fulani akikueleza matatizo yake. Tumia ujuzi wako wa Kikristo kumsaidia, na kuthibitisha kwamba wewe ni “rafiki wa kweli.”—Methali 17:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nyakati nyingine huenda ukahitaji kutafuta msaada kwa ajili ya rafiki yako aliye na tatizo