Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwapa Watoto Uangalifu Wanaohitaji

Kuwapa Watoto Uangalifu Wanaohitaji

Maoni ya Biblia

Kuwapa Watoto Uangalifu Wanaohitaji

JE, Mwana wa Mungu alikuwa na wakati wa kufanya mambo pamoja na watoto? Wanafunzi wake hawakufikiri hivyo. Pindi moja waliwazuia watoto wasimkaribie Yesu. Hata hivyo, yeye aliwaambia: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwazuia.” Kisha akawachukua watoto hao na kuzungumza nao. (Marko 10:13-16) Kwa kufanya hivyo, Yesu alionyesha kwamba alikuwa tayari kuwahangaikia watoto. Wazazi wanaweza kuigaje kielelezo chake? Wanaweza kufanya hivyo kwa kuwazoeza watoto wao kwa njia inayofaa na kwa kutumia wakati pamoja nao.

Bila shaka, wazazi wanaochukua madaraka yao kwa uzito huwajali watoto wao na huepuka kuwadhulumu. Pia ni jambo la “asili” kwa wazazi kuwaheshimu watoto na kuwaonyesha ufikirio. Hata hivyo, Biblia inasema kwamba katika siku zetu watu wengi hawatakuwa na “upendo wa asili.” (2 Timotheo 3:1-3) Wazazi wanaowapenda watoto wao hujitahidi kuboresha sifa zao ili wawashughulikie watoto wao vizuri zaidi. Wazazi wanaotaka kufanya hivyo watafurahia vikumbusho vya Biblia vinavyofuata.

Kuwazoeza Watoto Bila Kuwakasirisha

Dakt. Robert Coles, ambaye ni mwalimu na mtaalamu wa akili aliye maarufu, alisema hivi: “Mtoto anahitaji kanuni za kiadili. Ameumbwa akiwa na uhitaji huo, naye hutamani sana kuutosheleza.” Ni nani atakayetimiza uhitaji huo?

Biblia husema hivi katika Waefeso 6:4: “Akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” Je, unaona kwamba andiko hilo humtaka baba hasa awazoeze watoto wake kumpenda Mungu na kuheshimu viwango vyake? Katika Waefeso sura ya 6 mstari wa 1, mtume Paulo alipowaambia watoto ‘wawatii wazazi wao,’ alimaanisha wote wawili, yaani, baba na mama. *

Bila shaka, ikiwa baba hayupo, ni lazima mama achukue daraka hilo. Mama wengi wasio na wenzi wamefanikiwa kuwalea watoto wao katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova Mungu. Hata hivyo, mama hao wakiolewa na waume Wakristo, mume ndiye anayepaswa kuchukua daraka hilo. Mama anapaswa kufuata kwa hiari mwongozo wa baba Mkristo katika kuwazoeza na kuwatia watoto nidhamu.

Unaweza kuwazoezaje watoto wako bila ‘kuwakasirisha’? Hakuna njia moja hususa, hasa tunapotambua kwamba watoto wanatofautiana. Lakini ni lazima wazazi wafikirie kwa uzito jinsi wanavyotoa nidhamu, huku wakijitahidi kila mara kuwapenda na kuwaheshimu watoto wao. Andiko la Wakolosai 3:21 hurudia tena shauri hilo la kutowakasirisha watoto. Akina baba wanashauriwa hivi: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”

Wazazi fulani huwapigia watoto wao kelele. Bila shaka, jambo hilo huwakasirisha watoto. Lakini Biblia hutuhimiza hivi: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.” (Waefeso 4:31) Isitoshe, Biblia husema kwamba “mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.”—2 Timotheo 2:24.

Tumia Wakati Pamoja Nao

Kuwapa watoto wako uangalifu ambao wanahitaji kunatia ndani kuwa tayari kujinyima starehe na mambo mengine ili uwahangaikie watoto wako. Biblia husema hivi: “Maneno haya ninayokuamuru leo lazima yawe moyoni mwako; nawe uyakazie kwa mwana wako na kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.”—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

Kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi, ni vigumu kwa wazazi wengi kuwa pamoja na watoto wao tangu asubuhi hadi jioni. Hata hivyo, kitabu cha Kumbukumbu la Torati kinasema kwamba ni “lazima” wazazi watafute wakati wa kuwa pamoja na watoto wao. Ili waweze kufanya hivyo, wazazi wanapaswa kupanga mambo vizuri na kujitoa mhanga. Bila shaka, watoto wanahitaji kuhangaikiwa.

Fikiria kauli hii ya watafiti waliowachunguza vijana zaidi ya 12,000: “Uhusiano wa karibu pamoja na mzazi ndiyo njia bora zaidi ya kumwezesha kijana awe na afya njema na kuepuka mazoea yanayohatarisha uhai.” Naam, watoto hutaka sana uangalifu wa wazazi wao. Mama mmoja aliwauliza watoto wake hivi: “Ikiwa mngeahidiwa kupewa kitu chochote mnachotaka, mngechagua nini kwanza?” Watoto wote wanne walijibu hivi: “Kuwa pamoja na Baba na Mama kwa muda mrefu zaidi.”

Kwa hiyo, mzazi anayechukua daraka lake kwa uzito hujitahidi kutimiza mahitaji ya watoto wake, kama vile kuwa na urafiki wa karibu pamoja nao na kuwafundisha mambo ya kiroho. Hilo linahusisha kuwazoeza watoto wawe watu wazima wenye ustadi, wanaoheshimika, ambao huwatendea wanadamu wenzao kwa unyoofu na kumletea Muumba wao utukufu. (1 Samweli 2:26) Bila shaka, kwa kuwazoeza watoto na kuwatia nidhamu kupatana na mwongozo wa Mungu, wazazi huonyesha kwamba wanachukua daraka lao kwa uzito.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Katika mstari wa kwanza, Paulo alitumia neno la Kigiriki go·neuʹsin, linalotokana na neno go·neusʹ, ambalo humaanisha “mzazi.” Lakini katika mstari wa 4 anatumia neno la Kigiriki pa·teʹres, linalomaanisha “akina baba.”

[Picha katika ukurasa wa 13]

Watoto hufadhaika wazazi wanapowapigia kelele

[Picha katika ukurasa wa 13]

Tumia wakati mwingi pamoja na watoto wako