Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Visababishi na Madhara ya Mfadhaiko

Visababishi na Madhara ya Mfadhaiko

Visababishi na Madhara ya Mfadhaiko

MFADHAIKO ni nini? Kulingana na mtaalamu mmoja, mfadhaiko unaweza kufafanuliwa kuwa “hali yoyote ya kimwili, kikemikali, au kihisia ambayo hulemea mwili au akili.” Je, hilo linamaanisha kwamba nyakati zote mfadhaiko hutokeza madhara? La. Kama vile Dakt. Melissa C. Stöppler anavyosema, “nyakati nyingine kuwa na kiasi kidogo cha mfadhaiko na wasiwasi kunaweza kukufaidi. Mtu anapohisi kwamba amesongwa kidogo anapofanya kazi fulani anaweza kuchochewa kuifanya vizuri na kwa bidii.”

Hivyo, mfadhaiko husababisha madhara wakati gani? Stöppler anasema hivi: “Mfadhaiko husababisha madhara wakati mtu anapolemewa nao au anapoushughulikia vibaya.” Hebu tuchunguze visababishi fulani vya mfadhaiko.

Mfadhaiko Unaosababishwa na Kazi

Mfalme Sulemani alisema hivi: “Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kwamba ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.” (Mhubiri 2:24) Hata hivyo, wafanyakazi wengi hupaona mahali pa kazi kuwa mahali penye misongo mingi sana.

Ripoti ya Shirika la Ulaya la Usalama na Afya Kazini inasema kwamba mara nyingi wafanyakazi hukumbwa na mfadhaiko wanapokuwa kazini kwa sababu mbalimbali kama vile, mawasiliano yasiyofaa baina yao na wasimamizi, kukosa uhuru wa kutosha wa kufanya maamuzi yanayowahusu, kukosana na wafanyakazi wenzao, uwezekano wa kufutwa kazi au kwa sababu ya kulipwa mshahara mdogo. Hata sababu iwe nini, kushughulika na mfadhaiko unaosababishwa na kazi kunaweza kuwafanya wazazi washindwe kushughulikia mahitaji ya familia zao. Familia zinaweza kuwa na mahitaji mengi. Kwa mfano, katika kipindi cha mwaka mmoja huko Marekani, watu milioni 50 hivi waliwatunza washiriki wa familia waliokuwa wagonjwa au wazee. Matatizo ya kiuchumi yanaweza pia kusababisha mfadhaiko mwingi katika familia. Rita, ambaye ni mama ya watoto wawili, alikabili matatizo ya kiuchumi wakati mume wake anayeitwa Leandro alipopata msiba wa barabarani na kulazimika kutumia kiti cha magurudumu. Rita anasema hivi: “Matatizo ya kiuchumi husababisha mfadhaiko. Ikiwa huna pesa za kugharimia mahitaji yote ya nyumbani, mtazamo wako huathiriwa.”

Mfadhaiko Unaowakumba Wazazi Wasio na Mwenzi

Pia, wazazi wasio na mwenzi hukabili mfadhaiko mwingi wanapojitahidi kushughulikia familia zao. Kuamka mapema ili kutayarisha kiamshakinywa, kuwatayarisha watoto na kuwapeleka shuleni, kuharakisha ili kufika kazini kwa wakati, kisha kufanya kazi ngumu, humfanya mzazi asiye na mwenzi achoke sana kimwili na kihisia. Mama asiye na mwenzi anapotoka kazini, yeye huanza tena kukabili mfadhaiko anapoharakisha kuwachukua watoto shuleni, kutayarisha mlo wa jioni, na kufanya kazi nyingine za nyumbani. María, ambaye ni mzazi asiye na mwenzi mwenye mabinti wanne, anasema hivi: “Mfadhaiko huongezeka na kunifanya nihisi nitalipuka.”

Watoto Hukabili Mfadhaiko

Mwanasosholojia Ronald L. Pitzer anasema hivi: “Vijana wengi hukumbwa na mfadhaiko mwingi sana.” Lazima wakabiliane na mabadiliko ya kimwili na ya kihisia wanapobalehe. Pia wao husongwa sana na magumu wanayokabili shuleni. Kulingana na kitabu Childstress!, kwa kawaida mwanafunzi “hukabili matatizo mengi sana ambayo husababisha mfadhaiko, nayo yanatokana na masomo, michezo, marafiki, na kushughulika na walimu.”

Katika maeneo mengine wanafunzi hufadhaika kwa sababu ya kuogopa kushambuliwa shuleni. Vilevile vijana wengi huogopa mashambulizi ya kigaidi na misiba mingine. Msichana mmoja aliandika hivi: “Ikiwa kila mara wazazi wetu wanazungumzia jinsi ulimwengu unavyotisha, tutaogopa sana.”

Wazazi wanapaswa kuwaimarisha watoto wao. Lakini Pitzer anasema hivi: “Mara nyingi, watoto na vijana huzuiwa au kupuuzwa na wazazi wao wanapojitahidi kueleza jinsi wanavyohisi.” Nyakati nyingine wazazi hushindwa kuwashughulikia watoto kwa sababu wana matatizo ya ndoa. Mvulana anayeitwa Tito anasema hivi kuhusu wazazi wake ambao hatimaye walitalikiana: “Ni kana kwamba wazazi wangu walikuwa wakipigana kila mara.” Kitabu Childstress! kinasema kwamba “kupigana na kugombana sivyo visababishi pekee vya mfadhaiko wa kihisia. Chuki ya kichinichini huonekana hata inapofichwa kwa maneno matamu, nayo huwafadhaisha watoto.”

Madhara ya Mfadhaiko

Uwe kijana au mzee, au mfadhaiko wako unasababishwa na kazi au shule, afya yako inaweza kuathiriwa sana ukikabili mfadhaiko mwingi. Mwandishi mmoja wa masuala ya kitiba anaeleza hivi: “Tunaweza kulinganisha jinsi ambavyo mwili hutenda unapokabili mfadhaiko na ndege iliyo tayari kupaa.” Unapokabili mfadhaiko, mpigo wa moyo na shinikizo la damu hupanda. Kiwango cha sukari katika damu huongezeka. Homoni hutokezwa katika mfumo wa damu. Mwandishi huyo anaongeza hivi: “Mfadhaiko ukiendelea kwa muda mrefu, utendaji wa sehemu zote za mwili zinazohusiana na mfadhaiko (ubongo, moyo, mapafu, mishipa, na misuli) huongezeka au hupungua sana. Baada ya muda, hilo linaweza kusababisha madhara ya kimwili au ya kisaikolojia.” Magonjwa yanayoweza kusababishwa na mfadhaiko ni mengi sana. Baadhi ya magonjwa hayo ni kiharusi, ugonjwa wa moyo, kasoro za mfumo wa kinga, kansa, magonjwa yanayoathiri mifupa na misuli, na kisukari.

Watu wengi, hasa vijana, hutumia njia zisizofaa kukabiliana na mfadhaiko. Dakt. Bettie B. Youngs anasema hivi: “Inasikitisha sana kujua kwamba vijana hujaribu kuepuka huzuni kwa kunywa kileo, kutumia dawa za kulevya, kutoroka shule, kuwa watundu, kufanya ngono, kuwa wajeuri, na kutoroka nyumbani—mambo ambayo huwaletea matatizo makubwa kuliko yale wanayojaribu kuepuka.”

Mfadhaiko ni sehemu ya maisha ya leo na hauwezi kuepukwa kabisa. Hata hivyo, kama vile tutakavyoona katika makala inayofuata, kuna mengi tunayoweza kufanya ili kukabiliana na mfadhaiko!

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Mfadhaiko huongezeka na kunifanya nihisi nitalipuka”

[Picha katika ukurasa wa 5]

Mara nyingi wazazi wasio na mwenzi husongwa sana

[Picha katika ukurasa wa 6]

Vijana wanaweza kukabili msongo mwingi sana shuleni