Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Daraka la Mama Linaloheshimika

Daraka la Mama Linaloheshimika

Daraka la Mama Linaloheshimika

MARA nyingi watu hawathamini daraka la mama na nyakati nyingine wao hulidharau. Makumi ya miaka iliyopita, watu fulani walianza kudharau kazi ya kuwatunza watoto. Waliona kwamba kazi hiyo haikuwa muhimu kama kazi ya kuajiriwa na kwamba ni aina fulani ya mateso. Huenda watu wengi wakaona maoni hayo kuwa ya kupita kiasi, lakini mara nyingi akina mama hufanywa wahisi kwamba kazi ya kutunza nyumba na kuwalea watoto si muhimu sana. Baadhi yao hufikiri kwamba mwanamke anapaswa kufanya kazi nyingine ili kusitawisha vipawa vyake.

Hata hivyo, waume na watoto wengi wameanza kuthamini daraka la mama katika familia. Carlo, anayetumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Ufilipino, anaeleza hivi: “Nipo hapa leo kwa sababu ya mazoezi niliyopewa na mama yangu. Baba yangu alitoa nidhamu haraka, lakini Mama alijadiliana nasi na kutushauri alipokuwa akitusahihisha. Ninathamini sana jinsi alivyotufundisha.”

Peter, anayeishi Afrika Kusini, ni mmoja kati ya watoto sita waliolelewa na mama ambaye hakuwa amesoma sana. Baba yake alikuwa amewaacha. Peter anasema hivi: “Mama hakupata mshahara mkubwa kwani alikuwa yaya na alifanya kazi ya kusafisha nyumba. Ilikuwa vigumu kwake kutulipia sisi sote karo ya shule. Mara nyingi tulilala njaa. Ilikuwa vigumu kwake kulipa kodi ya nyumba. Licha ya matatizo hayo yote, Mama hakukata tamaa. Alitufundisha tusijilinganishe kamwe na wengine. Tumefanikiwa maishani kwa sababu ya jitihada na ujasiri wake.”

Mume mmoja wa Nigeria anayeitwa Ahmed anaeleza jinsi anavyohisi kuhusu msaada wa mke wake katika kulea watoto: “Ninathamini kazi ambayo mke wangu hufanya. Nisipokuwepo nyumbani, nina uhakika kwamba anawatunza watoto vizuri. Badala ya kuhisi kwamba mke wangu anashindana nami, mimi humshukuru na kuwaonyesha watoto kwamba lazima wamheshimu kama wanavyoniheshimu.”

Mwanamume mmoja Mpalestina anasifu kazi ya mke wake ambaye pia ni mama: “Lina amefanikiwa sana kumlea binti yetu naye ameboresha sana hali ya kiroho ya familia yetu. Kwa maoni yangu, amefanikiwa kwa sababu ya mambo anayoamini.” Lina ni Shahidi wa Yehova naye hutumia kanuni za Biblia kumfundisha binti yake.

Kanuni hizo ni gani? Biblia ina maoni gani kuhusu akina mama? Je, zamani akina mama waliheshimiwa kwa kupewa daraka la kuwafundisha watoto wao?

Maoni Yanayofaa Kuhusu Akina Mama

Mwanamke alipoumbwa alipewa daraka linaloheshimika katika familia. Kitabu cha kwanza cha Biblia kinasema: “Yehova Mungu akaendelea kusema: ‘Si vema huyo mwanamume aendelee kuwa peke yake. Nitamfanyia msaidizi, awe kikamilisho chake.’” (Mwanzo 2:18) Hivyo, mwanamke wa kwanza, Hawa, aliumbwa ili awe kikamilisho cha Adamu. Alikuwa msaidizi aliyemfaa kabisa. Alikuwa sehemu ya kusudi la Mungu la kuzaa watoto, kuwatunza, na kuitunza dunia na wanyama. Angemchochea Adamu kufikiri huku akimtegemeza akiwa rafiki yake wa kweli. Adamu alifurahi sana kupokea zawadi hiyo maridadi kutoka kwa Muumba!—Mwanzo 1:26-28; 2:23.

Baadaye, Mungu alieleza jinsi alivyotaka wanawake watendewe. Kwa mfano, akina mama Waisraeli walipaswa kuheshimiwa wala si kudharauliwa. Mtoto ‘aliyemlaani baba yake na mama yake’ alipaswa kuuawa. Vijana Wakristo walihimizwa ‘wawatii wazazi wao.’—Mambo ya Walawi 19:3; 20:9; Waefeso 6:1; Kumbukumbu la Torati 5:16; 27:16; Methali 30:17.

Mama alipaswa kufuata mwongozo wa mume wake katika kuwafundisha wana na mabinti. Mwana aliamuriwa ‘asiiache sheria ya mama yake.’ (Methali 6:20) Vivyo hivyo, sura ya 31 ya Methali ina “ujumbe mzito ambao mama [ya Mfalme Lemueli] alimwambia ili kumrekebisha.” Alimshauri mwana wake kwa hekima aepuke kutumia kileo vibaya, aliposema: “Haifai wafalme kunywa divai wala maofisa wakuu kuuliza: ‘Kileo kiko wapi?’ ili mtu asinywe na kusahau jambo lililoagizwa na kupotosha haki ya yeyote wa wana wa mateso.”—Methali 31:1, 4, 5.

Isitoshe, kijana yeyote anayefikiria kufunga ndoa anapaswa kufikiria ufafanuzi wa “mke mwenye uwezo” uliotolewa na mama ya Mfalme Lemueli, aliyesema: “Thamani yake inapita sana ile ya marijani.” Kisha, baada ya kueleza daraka muhimu ambalo mke huyo hutimiza katika familia, mama ya mfalme huyo alisema: “Uvutio unaweza kudanganya, nayo sura yenye kupendeza inaweza kuwa ubatili; lakini mwanamke anayemwogopa Yehova ndiye anayejiletea sifa.” (Methali 31:10-31) Ni wazi kwamba Muumba wetu aliwapa wanawake cheo kinachoheshimika na daraka muhimu katika familia.

Hata katika kutaniko la Kikristo, wake na akina mama wanaheshimiwa na kuthaminiwa sana. Waefeso 5:25 inasema: “Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu.” Kijana Timotheo, aliyezoezwa na mama yake na nyanya yake kuheshimu “maandishi matakatifu,” alipewa shauri hili lililoongozwa kwa roho: ‘Wasihi wanawake wazee kama mama.’ (2 Timotheo 3:15; 1 Timotheo 5:1, 2) Kwa hiyo, mwanamume anapaswa kumheshimu mwanamke mzee kama anavyomheshimu mama yake. Kwa kweli, Mungu anawathamini wanawake naye huwapa daraka linaloheshimika.

Onyesha Uthamini Wako

Mwanamume mmoja aliyelelewa katika utamaduni unaowapuuza wanawake anasema: “Nilifundishwa kwamba mwanamume ndiye wa maana zaidi, nami niliwaona wanawake wakitendewa vibaya na kudharauliwa. Hivyo imenibidi nijitahidi sana kumwona mwanamke sawa na Muumba anavyomwona, yaani, akiwa kikamilisho, au msaidizi nyumbani, na kwamba ana daraka la kunisaidia kuwafundisha watoto. Ingawa ni vigumu kumsifu mke wangu, ninajua kwamba watoto wangu wana sifa nzuri kwa sababu ya jitihada zake.”

Bila shaka, akina mama ambao hutimiza daraka lao la kufundisha watoto, wanaweza kujivunia jambo hilo. Kazi yao ni muhimu sana. Wanastahili kupongezwa na kuthaminiwa sana. Akina mama hutufundisha mengi, kama vile mazoea muhimu maishani, tabia njema zinazohitajiwa sana ili kuwa na mahusiano mazuri, na mara nyingi wanafundisha kanuni za adili na za kiroho zinazoweza kuwasaidia vijana. Je, umempongeza mama yako hivi karibuni kwa sababu ya mambo ambayo amekufanyia?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mama ya Peter alimfundisha kutokata tamaa

[Picha katika ukurasa wa 10]

Ahmed huthamini sana msaada wa mke wake katika kuwalea watoto wao

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mume wa Lina anasema kwamba binti yao ana tabia njema kwa sababu ya imani ya mke wake