Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Akina Mama Wanavyoshinda Magumu

Jinsi Akina Mama Wanavyoshinda Magumu

Jinsi Akina Mama Wanavyoshinda Magumu

TATIZO kubwa ambalo mama wengi hukabili leo ni kufanya kazi ili kuruzuku familia. Isitoshe, wengine hulazimika kuwalea watoto wakiwa peke yao kwa sababu mbalimbali.

Margarita, ambaye anaishi Mexico, ni mama asiye na mwenzi anayelea watoto wawili akiwa peke yake. Anasema: “Imekuwa vigumu kuwafundisha maadili na mambo ya kiroho.” Anaongeza hivi: “Wakati fulani, kijana wangu alikuja nyumbani akiwa amelewa. Nilimwonya kwamba akifanya hivyo tena, sitamruhusu aingie ndani ya nyumba. Aliporudia, nilimfungia nje ingawa nilihuzunika sana kufanya hivyo. Nafurahi kwamba hakurudia tena kufanya hivyo.”

Muda mfupi baadaye, Margarita alianza kujifunza Biblia, na hilo lilimsaidia kuwafundisha watoto wake kanuni za maadili. Sasa hivi watoto hao wawili ni Mashahidi wa Yehova ambao wanafanya utumishi wa wakati wote.

Waume Wanapohamia Kwingineko

Waume wengi katika nchi zinazoendelea huhamia nchi tajiri ili kutafuta kazi, na kuwaacha wake zao wawalee watoto wakiwa peke yao. Mama mmoja huko Nepal anayeitwa Laxmi anasema hivi: “Mume wangu amekuwa katika nchi nyingine kwa miaka saba. Watoto wangu hawanitii kama wanavyomtii baba yao. Ikiwa angekuwapo kwa ukawaida, ingekuwa rahisi kuwazoeza.”

Laxmi anajitahidi kukabiliana na magumu hayo. Kwa kuwa hajasoma sana, amepanga watu fulani wawasaidie watoto wake wakubwa kufanya kazi za shule. Hata hivyo, yeye huhangaikia elimu yao ya kiroho, na hivyo hujifunza nao Biblia kila juma. Kila siku, yeye huzungumzia andiko la Biblia pamoja nao, naye huandamana nao kwa ukawaida kwenye mikutano ya Kikristo.

Akina Mama Wasiokuwa na Elimu Nyingi

Tatizo lingine ambalo wanawake wengi hukabili katika nchi fulani ni kutojua kusoma na kuandika. Aurelia ambaye ni mama ya watoto sita huko Mexico, anaeleza matatizo ambayo mama hukabili kwa sababu ya kutokuwa na elimu. Anasema: “Mama yangu alizoea kusema kwamba wanawake hawapaswi kuelimishwa. Hivyo, sikujifunza kusoma na singeweza kuwasaidia watoto wangu kufanya kazi za shule. Hilo lilinihuzunisha. Lakini kwa kuwa sikutaka wateseke kama nilivyokuwa nimeteseka, nilijitahidi sana kuwasaidia wapate elimu.”

Mama anaweza kutimiza mengi hata ikiwa hajasoma sana. Msemo huu ni kweli kabisa: “Ukiwaelimisha wanawake, umewaelimisha walimu wa wanaume.” Bishnu anayetoka Nepal, ambaye ni mama ya wana watatu, hakujua kusoma na kuandika. Hata hivyo, tamaa yake ya kujifunza kweli za Biblia na kuwafundisha watoto wake kweli hizo ilimchochea ajitahidi sana kujua kusoma na kuandika. Alihakikisha kwamba watoto wake wanafanya kazi za shule, na mara nyingi alienda katika shule walizosomea ili kuzungumza na walimu kuhusu hali ya watoto wake.

Silash, mwana wa Bishnu, anasema hivi kuhusu mafundisho ya kiroho na ya kiadili ambayo mama yao aliwapa: “Jambo lililonipendeza zaidi kuhusu jitihada zake za kutufundisha ni kwamba tulipokosea alitutolea mifano ya Biblia ili kutusahihisha. Njia hiyo ya kutufundisha ilikuwa na matokeo na ilinisaidia kukubali shauri.” Bishnu amefaulu kuwafundisha wana wake, kwani wote watatu wamekuwa vijana wanaomcha Mungu.

Antonia anayeishi huko Mexico, ambaye ni mama ya watoto wawili, anasema hivi: “Nilienda shule ya msingi tu. Tuliishi katika kijiji kilicho mbali, na shule ya sekondari ilikuwa mbali sana. Lakini nilitaka watoto wangu wasome zaidi kuliko mimi, kwa hiyo nilitenga wakati mwingi kuwasaidia. Niliwafundisha alfabeti na nambari. Binti yangu alijua kutaja herufi za jina lake na kuandika herufi zote za alfabeti kabla hajaanza kwenda shule. Mwana wangu alijua kusoma vizuri kabla hajaanza kwenda shule ya watoto wadogo.”

Antonia alipoulizwa kile alichofanya ili kuwafundisha watoto wake mambo ya kiroho na ya kiadili, alisema: “Niliwafundisha hadithi za Biblia. Kabla binti yangu hajajua kuzungumza, angeweza kusimulia hadithi za Biblia kwa ishara. Mwana wangu alitoa hotuba yake ya kwanza ya usomaji wa Biblia kwenye mikutano yetu ya Kikristo akiwa na umri wa miaka minne.” Mama wengi wasio na elimu nyingi wamefaulu kuwafundisha watoto wao.

Kushinda Mila Zinazodhuru

Mila moja ya kabila la Tzotzil nchini Mexico ni kuwaoza mabinti wao wakiwa na umri wa miaka 12 au 13. Mara nyingi wasichana huuzwa kwa wanaume wazee wanaotaka mke wa pili au wa tatu. Mwanamume asiporidhishwa na msichana huyo, anaweza kumrudisha na kudai pesa zake. Petrona alikabili mila hiyo alipokuwa mdogo. Mama yake alikuwa ameuzwa, akaolewa, akazaa mtoto na kutalikiwa kufikia wakati ambapo alikuwa na miaka 13! Mtoto huyo wa kwanza alikufa, na baada ya hapo mama ya Petrona aliuzwa na kuolewa mara mbili zaidi. Kwa jumla, alizaa watoto wanane.

Petrona alitaka kuepuka mila hiyo, na anaeleza jinsi alivyofaulu kufanya hivyo: “Nilipomaliza shule ya msingi, nilimwambia Mama kwamba sikutaka kuolewa bali nilitaka kuendelea na masomo. Mama alisema kwamba hangeweza kufanya lolote na kuniambia kuwa napaswa kuongea na baba yangu.”

Baba aliniambia hivi: “Nitakuoza. Unajua Kihispania na unajua kusoma. Unataka nini kingine? Ukitaka kuendelea na masomo, utajilipia karo.”

Petrona anasema hivi: “Basi nikaamua kujilipia karo. Nilipamba nguo kwa nyuzi ili kupata pesa.” Hivyo ndivyo alivyoepuka kuozwa. Baada ya Petrona kuwa mkubwa, mama yake alianza kujifunza Biblia, na hilo lilimpa ujasiri wa kuwafundisha dada wadogo wa Petrona kanuni za Biblia. Kwa kutegemea mambo yaliyompata, mama huyo aliwafundisha madhara ya mila ya kuwaoza wasichana wadogo.

Katika sehemu nyingi, baba tu ndiye huwatia nidhamu wavulana. Petrona anasema: “Wanawake wa kabila la Tzotzil hufundishwa kwamba wako chini ya wanaume. Wanaume hupiga ubwana sana. Wavulana wadogo huwaiga baba zao, nao huwaambia mama zao hivi: ‘Hupaswi kuniambia la kufanya. Baba yangu asiponiambia, sitafanya.’ Kwa hiyo akina mama hawawezi kuwaelimisha wavulana wao. Lakini, baada ya mama yangu kujifunza Biblia, amefaulu kuwafundisha ndugu zangu. Wanaweza kukariri andiko hili la Waefeso 6:1, 2: ‘Enyi watoto, watiini wazazi wenu. . . . Mheshimu baba yako na mama yako.’”

Mama mmoja huko Nigeria anayeitwa Mary anasema hivi: “Utamaduni wa mahali nilipolelewa haumruhusu mama kuwafundisha au kuwatia nidhamu wavulana. Hata hivyo, kwa kufuata mfano wa Loisi na Eunike—nyanya na mama ya Timotheo—niliazimia kutoruhusu mila zinizuie kuwafundisha watoto wangu.”—2 Timotheo 1:5.

Mila nyingine inayofuatwa sana katika nchi fulani ni kuwatahiri wasichana. Mila hiyo inahusisha kuondoa sehemu ya kiungo cha uzazi cha msichana. Waris Dirie, mwanamitindo maarufu na mwakilishi wa pekee wa Hazina ya Idadi ya Watu ya Umoja wa Mataifa, ndiye aliyejulisha umma mambo mengi kuhusu mila hiyo. Kupatana na mila za kwao za Kisomali, mama yake alimlazimisha kutahiriwa alipokuwa mdogo. Kulingana na ripoti moja, kati ya wanawake na wasichana milioni nane hadi milioni kumi huko Mashariki ya Kati na Afrika wanakabili hatari ya kupashwa tohara. Hata huko Marekani, inakadiriwa kwamba wasichana 10,000 wamo hatarini.

Kwa nini wasichana hutahiriwa? Watu fulani hufikiri kwamba viungo vya uzazi vya wasichana ni viovu na vinawafanya kuwa najisi na kuwafanya wasistahili kuolewa. Isitoshe, kuwatahiri wasichana huonwa kuwa njia ya kuhakikisha kwamba watadumu wakiwa mabikira na waaminifu. Mama asipotekeleza mila hiyo atamkasirisha mume wake na jamii yao.

Hata hivyo, mama wengi wametambua kwamba hakuna sababu yoyote inayofaa ya kidini, kitiba, au ya usafi inayounga mkono mila hiyo. Kitabu cha Nigeria kinachoitwa Repudiating Repugnant Customs kinaonyesha kwamba mama wengi wamekataa katakata kuwatahiri binti zao.

Kwa kweli, akina mama ulimwenguni pote wanafaulu kuwalinda na kuwafundisha watoto wao licha ya magumu wanayokabili. Je, kweli jitihada zao zinathaminiwa?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

“Uchunguzi mwingi umeonyesha kwamba wanawake hutimiza daraka muhimu katika miradi yote ya maendeleo yenye mafanikio. Wanawake wanapohusishwa, faida huonekana mara moja: afya ya washiriki wa familia huwa bora, nao hulishwa vizuri; mapato na akiba ya familia huongezeka. Na jambo hilo halihusu familia tu bali pia jamii na nchi nzimanzima.”—Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Kofi Annan, Machi 8, 2003.

[Hisani]

UN/DPI photo by Milton Grant

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 8]

Aliacha Kazi kwa Ajili Yetu

Kijana mmoja Mbrazili anayeitwa Juliano anasema hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka mitano, mama yangu alikuwa na kazi nzuri sana. Hata hivyo, dada yangu alipozaliwa, mama yangu aliamua kuacha kazi ili atutunze. Washauri fulani kazini walijaribu kumshawishi abadili uamuzi wake. Walimwambia kwamba watoto wake wakiisha kufunga ndoa na kuondoka nyumbani jitihada zake zote zitakuwa bure na kwamba hatapata faida yoyote. Lakini watu hao walikosea; siwezi kamwe kusahau upendo ambao mama alituonyesha.”

[Picha]

Mama ya Juliano na watoto wake; kushoto: Juliano akiwa na umri wa miaka mitano

[Picha katika ukurasa wa 6]

Bishnu alijifunza kusoma na kuandika kisha akawasaidia wana wake kupata elimu bora

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mwana mdogo wa Antonia hutoa hotuba za usomaji wa Biblia katika mikutano ya Kikristo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Petrona ni mfanyakazi wa kujitolea katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Mexico. Mama yake, ambaye baadaye alikuja kuwa Shahidi, huwafundisha dada wadogo wa Petrona

[Picha katika ukurasa wa 8]

Waris Dirie ni mpinzani maarufu wa mila ya kuwatahiri wasichana

[Hisani]

Photo by Sean Gallup/ Getty Images