Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuchanganya Ukatoliki na Dini za Kiafrika

Kuchanganya Ukatoliki na Dini za Kiafrika

Kuchanganya Ukatoliki na Dini za Kiafrika

Na mwandishi wa Amkeni! nchini Brazili

HUKO Salvador, jiji kuu la Jimbo la Bahia, nchini Brazili, mwaka mpya hukaribishwa kwa sherehe kubwa. Mamia ya wanawake huongoza maandamano hadi kwenye kanisa la Katoliki la Bonfim, ambako wao huosha ngazi za kanisa kwa maji yenye manukato. Desturi hiyo hufanywa kwa heshima ya Oxalá, mungu wa uumbaji wa Waafrika.

Watazamaji wapatao milioni moja hushuhudia desturi hiyo. Kisha wao hujiunga katika sherehe zenye nderemo nyingi zinazofanywa barabarani, huku muziki ukichezwa kwa vyombo vya muziki vya Kiafrika.

Desturi hiyo ambayo imefuatwa kwa miaka 250 ni mfano mmoja unaoonyesha jinsi imani mbalimbali zimechanganywa katika dini. Dini ya Ukatoliki ya Brazili imechanganya imani kwa njia hiyo. Inasemekana kwamba zaidi ya Wabrazili milioni 70 wanafuata moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja dini za Candomblé, Umbanda, Xangô, na dini nyingine za Wabrazili wenye asili ya Kiafrika. Lakini bado wengi wao wanadai kuwa Wakatoliki.

Mchanganyiko huo wa imani ulianzaje? Kanisa Katoliki linaonaje jambo hilo? Na je, inafaa kuchanganya imani?

Kichocheo cha “Kupata Dini ya Kweli”

Inakadiriwa kwamba zaidi ya Waafrika milioni sita wa kabila la Yoruba, Bantu, na makabila mengine walisafirishwa hadi Brazili wakiwa watumwa kuanzia katikati ya karne ya 16 hadi mwaka wa 1888, wakati ambapo biashara ya watumwa ilikomeshwa. Basi, watumwa hao ndio waliosababisha kuchanganywa kwa imani ya Waafrika na ya Wakatoliki wa Brazili.

Ijapokuwa Kanisa Katoliki liliwalazimisha watumwa wote kuwa Wakatoliki, lilikubali imani ya Ukatoliki ichanganywe na imani ya dini za Kiafrika. Kulingana na mwanahistoria Roger Bastide, wamishonari Wajesuti waliamini kwamba Waafrika wa asili wanapaswa kuvutwa kwenye Ukatoliki kama watoto, kwa kutumia muziki, dansi, na vyeo. Bastide aliandika hivi: “Hawapaswi kulazimishwa kuacha kabisa mila zao, lakini mila hizo zinapaswa kuchunguzwa na zile zinazokubalika zitumiwe kuwachochea kupata dini ya kweli.”

Katika vikundi vingi vya kidini vya Waafrika, kama vile vinavyohusishwa na “Mtakatifu” Benedict wa Ukatoliki na Bikira wa Rozari, desturi nyingi za Kiafrika zilifanywa ziwe za “Kikristo.” Mara moja kila mwaka, wakati wa sikukuu ya “Mtakatifu” Benedict, vikundi kama hivyo vilichagua mfalme na malkia miongoni mwa washiriki wake, na desturi hiyo ilitokana na zoea la makabila ya Waafrika la kuwa na wafalme.

“Watakatifu” au Orixá?

Kanisa Katoliki na dini nyingi za Kiafrika huamini kwamba kuna waombezi wengi kati ya Mungu na wanadamu. Kwa mfano, Wayoruba waliamini waombezi wanaoitwa orixá. Iliaminiwa kwamba waombezi hao walikuwa mashujaa na wafalme walioabudiwa ambao walidhibiti nguvu za asili na kuwapatanisha watu na mungu wao mkuu, Olorun. Vivyo hivyo, Wakatoliki huamini kwamba “watakatifu” humwomba Mungu kwa niaba ya wanadamu. Nao huwaomba “watakatifu” fulani wawalinde katika shughuli hususa.

Watumwa wengi hawakuacha kuamini waombezi wao walioitwa orixá, bali walificha imani yao kwa kuwaabudu “watakatifu” wenye sifa zinazofanana na za waombezi wao. Hivyo, waliwaona “watakatifu” Anthony na George, ambao walikuwa askari-jeshi na mashujaa wa Jumuiya ya Wakristo, kuwa sawa na Ogun, mungu wa vita wa Wayoruba.

Vivyo hivyo, walimfananisha Yemanjá, ambaye ni mama ya waombezi wote na mungu wa kike wa bahari zote, na “mizuka” ya Bikira Maria. Bwana wa Bonfim, ambaye ni “mtakatifu” maarufu zaidi wa Salvador, alifananishwa na Oxalá, mwombezi mkuu wa hekalu la Wayoruba. Bado uhusiano huo huonyeshwa katika desturi ya kila mwaka ya kuosha ngazi za kanisa. *

Kiongozi mmoja wa Wakatoliki kutoka jiji la Salvador anasema: “Watu huku humwamini Yesu, watakatifu wa dini ya Katoliki, na waombezi wanaoitwa orixá kwa usadikisho uleule.” Mtaalamu mwingine wa Brazili anaongeza hivi: “Watu wengi huhamahama dini moja na kuingia nyingine. Baada ya kuhudhuria Misa katika kanisa la Kikatoliki wao huenda moja kwa moja katika kanisa la candomblé [la Kiafrika].”

Zoea hilo la kuchanganya Ukatoliki na dini za Kiafrika ni suala tata. Lucas Moreira, aliyekuwa msimamizi wa Kongamano la Baraza la Maaskofu wa Brazili wa Kanisa Katoliki, alisema hivi: “Kila mtu anapaswa kufuata imani yake bila kuchanganya.” Zaidi ya hayo, askofu mwingine Mkatoliki anasema hivi: “Zoea la kuchanganya imani huzuia jitihada za kanisa.”

Kuna maoni mbalimbali kuhusu suala hilo. Viongozi fulani wa kanisa hupinga mambo wanayoona kuwa ya kipagani na ya kishetani, huku wengine wakitetea kuingizwa kwa sanamu na dansi za Waafrika katika desturi za Kanisa Katoliki.

Yesu Angesema Nini?

Yesu Kristo, Mwanzilishi wa Ukristo, aliwahubiria watu wa dini na makabila tofauti-tofauti. Lakini alisema hivi waziwazi: “Waabudu wa kweli watamwabudu Baba kwa roho na kweli, kwa maana, kwa kweli, Baba anawatafuta watu wa namna hiyo wamwabudu.” (Yohana 4:23) Isitoshe, Yesu alisema kwamba Baba, Yehova Mungu, hufunua ukweli kupitia Neno Lake, Biblia.—Yohana 17:17.

Yesu aliwaagiza wafuasi wake kuwafundisha ‘watu wa mataifa yote kushika mambo yote ambayo aliwaamuru.’ (Mathayo 28:19, 20) Hakusema kamwe wabadilishe mafundisho yake ili wawavutie watu waliofuata desturi na imani tofauti. Katika siku za mitume, watu fulani walijaribu kuingiza dhana na desturi za dini nyingine. Hata hivyo, jitihada hizo zilishutumiwa. Mtume Paulo alisema hivi: ‘Tokeni katikati yao, na mjitenge, na [Mungu] atawakaribisha ndani.’—2 Wakorintho 6:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Kulingana na Dicionário de Cultos Afro-Brasileiros (Kamusi ya Dini za Wabrazili Wenye Asili ya Kiafrika), desturi ya kuosha ngazi za kanisa la Bonfim huhusianishwa sana na desturi ya Kiyoruba inayoitwa maji ya Oxalá, inayohusisha kuosha otás (mawe matakatifu) ya Oxalá.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Makuhani wa kike Wabrazili wenye asili ya Kiafrika wakiosha ngazi za kanisa

Umati wa watu kwenye ngazi za kanisa huko Bonfim, Brazili

[Hisani]

Top: De: A Tarde—Wilson da Rocha Besnosik; bottom: De: A Tarde—Antônio Queirós