Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilifurahia Kufanya Mengi Zaidi

Nilifurahia Kufanya Mengi Zaidi

Nilifurahia Kufanya Mengi Zaidi

SIMULIZI LA CLAIRE VAVY

KISIWA cha Madagaska, kiko umbali wa kilometa 400 hivi kutoka Msumbiji, nchi iliyoko Afrika ya Mashariki. Kisiwa hicho kina milima mingi na misitu ya mvua. Nilizaliwa mashariki mwa kisiwa hicho katika kijiji cha Betoko II. Katika mwaka wa 1987, nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilihamia mji wa pwani wa Mahanoro ili kwenda shule.

Niliishi Mahanoro pamoja na ndugu yangu mkubwa Celestin, ambaye alikuwa ameanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Miaka miwili baadaye nikawa Shahidi. Niliazimia kumtumikia Yehova Mungu kwa kadiri niwezavyo.

Najitahidi Kufikia Miradi Yangu

Mojawapo ya miradi yangu ya kwanza ilikuwa kusaidia familia yetu huko Betoko II, na katika sala nilimweleza Yehova kwa ukawaida kuhusu tamaa yangu. Hata hivyo, nilirudi nyumbani wakati tu wa likizo ya shule. Safari ya kurudi nyumbani ilikuwa ngumu na ilinibidi kusafiri kwa kilometa 100. Mtu angeweza kusafiri kwa gari kwa kilometa 40 za kwanza, kisha atembee kwa kilometa 60 kupitia kijia chembamba milimani ambacho kingepitika tu kwa miguu.

Ilinibidi kupanda milima mingi mirefu, na sehemu fulani za kijia hicho zilikuwa nyembamba sana. Iwapo ningeanza safari yangu mapema na kutembea hadi jioni, ningesafiri kwa kilometa 40 hivi. Nilikuwa nikibeba mizigo yenye uzito wa zaidi ya kilo 15 kichwani, mgongoni, na mikononi. Nilibeba hasa vitabu vya Biblia ambavyo niliwagawia watu wa ukoo na watu wengine wanaopendezwa. Watu wengi waliniita “yule mtu mwenye mizigo mingi.”

Mwanzoni, washiriki wa familia yetu walikataa kunisikiliza nilipowahubiria licha ya jitihada zangu. Hata hivyo, muda mfupi baadaye walibadilika na kuanza kuuliza maswali mengi sana hivi kwamba nyakati nyingine tulilala saa nane za usiku.

Ziara Nisiyoweza Kusahau

Katika Desemba 24, 1990, nilirudi nyumbani huko Betoko II wakati wa likizo. Washiriki wa familia yetu walifurahi kuniona kwani walifikiri kwamba nimekuja tusherehekee Krismasi. Walivunjika moyo sana nilipowaeleza sababu yangu ya kutosherehekea Krismasi. Waliona haya kuwaeleza wanakijiji wenzetu kuhusu jambo hilo, kwani watu katika kijiji chetu walishirikiana sana. Hivyo, niliona ni afadhali mimi mwenyewe niwaeleze. Lakini ningefanyaje hivyo?

Kwa kuwa nilikuwa na umri mdogo sikujua la kufanya. Nilifikiria sana ikiwa inafaa kuwaeleza wanakijiji mambo niliyoamini walipokusanyika kanisani siku iliyofuata. Nilitoa sala ndefu ya kutoka moyoni na kumwomba Yehova mwongozo wake. Kisha nikamwuliza hivi ndugu yangu mkubwa anayeitwa Paul, ambaye alikuwa mwalimu wa kanisa: “Je unafikiri ingefaa niwaeleze watu watakaokuwa kanisani kesho kwa nini sisherehekei Krismasi?” Alishauriana na wengine, nao wakakubali.

Siku iliyofuata, niliitwa baada ya ibada kumalizika kanisani. Nilisali tena kwa Yehova kisha nikabeba vichapo vya Biblia na kwenda navyo kanisani. Baada ya utangulizi, niliwashukuru wote kwa kunisaidia kuiheshimu sana Biblia. Niliwaeleza kwamba baada ya kuhamia mjini niliendelea kujifunza Biblia. Pia nilisema kwamba nimejifunza kweli nyingi za Biblia ambazo hatukuwa tumefundishwa.

Nilitumia nafasi hiyo kueleza kuhusu tumaini la kuishi milele katika dunia iliyo paradiso linaloelezwa katika Biblia (Zaburi 37:29; Ufunuo 21:3, 4), sababu gani watu wachache waaminifu wataenda mbinguni (Yohana 14:2, 3; Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3), na fundisho la Biblia kwamba wafu hawajui lolote kwani ni kana kwamba wanalala na hivyo hawateseki (Mhubiri 9:5, 10; Yohana 11:11-14, 38-44). Pia niliwajulisha kwamba Wakristo wa mapema hawakusherehekea Krismasi na kwamba sherehe hiyo ni ya kipagani.

Nilipomaliza kuwahubiria, wengi wao walisema kwamba mambo niliyosema yalikuwa ya kweli. Baadhi yao waliuliza maswali zaidi. Baadaye niliwaonyesha vichapo nilivyokuwa navyo na kuwaambia kwamba hivyo ni vitabu vya kuwasaidia watu kujifunza Biblia ambavyo huchapishwa na Mashahidi wa Yehova. Niliwaambia kwamba niko tayari kumsaidia mtu yeyote anayetaka kujifunza Biblia. Wengi walichukua vichapo vya Biblia.

Nagundua Jambo la Kustaajabisha

Mwanamke mmoja ambaye sikuwa nimewahi kumwona alikuja na kuniambia, “Dada yangu anayeishi katika kijiji kingine ni wa dini yenu.” Niliuliza hivi kwa mshangao, “Anaishi wapi?”

Akajibu hivi, “Anaishi huko Andranomafana.” Kijiji hicho kiko umbali wa kilometa 30 kutoka Betoko II.

Nilimwambia mwanamke huyo kwamba labda dada yake ni wa dini nyingine kwani Mashahidi wote katika eneo hilo wanafahamiana. Hata hivyo, aliendelea kusisitiza akisema kwamba dada yake alikuwa amemfundisha mambo yaleyale niliyokuwa nimefundisha kanisani. Nilimwomba jina na anwani ya dada yake kwa kuwa nilitamani sana kwenda huko bila kukawia. Hata hivyo, mama yangu akanihimiza nisiende siku hiyohiyo kwani safari hiyo ilikuwa ngumu, na ingenibidi kusafiri kwa miguu. Siku mbili baadaye nilienda Andranomafana nikiwa na ndugu yangu Charles.

Mara tulipofika tuliwauliza wanakijiji hivi, “Je kuna Mashahidi wa Yehova huku?” Nilivunjika moyo walipojibu hivi, “Katika kijiji hiki hakuna makanisa mengine ila kanisa Katoliki, Pentekoste, na Independent.”

Kisha mwanamke mmoja akasema, “Ikiwa unawatafuta Mashahidi wa Yehova, huenda unamtafuta Marceline na familia yake.” Huyo ndiye mtu niliyekuwa nimeambiwa nimtafute!

Mtu fulani alikwenda kumwita Marceline. Marceline alikuja lakini alionekana ana wasiwasi. Wanakijiji wengi walituzunguka, kwani walifikiri sisi ni maofisa wanaotaka kumhoji. Baadaye nilipata habari kwamba yeye na familia yake walikuwa wamenyanyaswa katika kijiji hicho kwa sababu ya kufuata ‘dini isiyo ya kawaida.’

Marceline alitupeleka kando na umati ili tuzungumze. Nilipomwuliza ikiwa yeye ni Shahidi wa Yehova, alikubali. Kisha akaenda na kuleta kitabu Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, ambacho Mashahidi wa Yehova walitumia zamani kuwafundisha watu Biblia, na vilevile nakala za zamani za Mnara wa Mlinzi. Vichapo hivyo vyote vilikuwa vimechakaa na kuraruka-raruka. Nikamwuliza hivi, “Mlijifunza gazeti gani Jumapili?”

Marceline akajibu hivi, “Haya tu ndiyo magazeti tuliyo nayo, nasi huyasoma tena na tena.” Hapo ndipo nilipomweleza Marceline kwamba mimi pia ni Shahidi. Alifurahi sana! Nilipomweleza kwamba ningependa kumwona mwanamume anayeongoza mikutano yao, aliniambia kwamba anaishi katika eneo jingine lililo mbali zaidi.

Nagundua Jambo Jingine la Kupendeza

Siku iliyofuata mimi na Marceline tulienda kumtembelea mwanamume huyo. Tulipofika alishangaa na kufurahi sana kutuona. Tuligundua kwamba yeye ni Shahidi aliyekuwa ametoka mji wa pwani wa Toamasina, ulioko kilometa 200 kaskazini-mashariki. Miaka kadhaa mapema, alilazimika kurudi huku akiwa na familia yake baada ya kupoteza kazi yake ghafula. Aliporudi alianza kuhubiri, kuongoza mafunzo ya Biblia na mikutano.

Shahidi huyo pamoja na familia yake walifurahi sana kuona magazeti ya karibuni zaidi ya Mnara wa Mlinzi niliyokuwa nayo. Pia niliwaonyesha kitabu Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani, ambacho tulikuwa tukitumia kama kitabu cha msingi cha funzo. Ilikuwa mara ya kwanza kwao kukiona. Jumapili iliyofuata nilirudi Andranomafana ili kuhudhuria mikutano pamoja nao. Niliwatia moyo wawasiliane na ofisi ya tawi ya Mashahidi huko Antananarivo, ambalo ndilo jiji kuu, kwani ofisi haikujua kama kulikuwa na kikundi hiki.

Kuanzia Januari 1991, karibu kila mwezi nilienda Andranomafana kutoka Mahanoro ili niwapelekee magazeti ya karibuni zaidi ya Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine. Ilikuwa safari ya kilometa 130, nami nilitembea kwa zaidi ya kilometa 90, kupanda na kushuka milima mirefu, kupitia misitu mikubwa na, kuliponyesha niling’ang’ana na matope mazito yenye utelezi.

Mizigo iliongezeka kadiri wale waliohitaji vichapo na magazeti walivyoongezeka. Licha ya kuchoka sana na kuumwa na misuli baada ya kila safari, nilipata furaha na uradhi mwingi. Ilikuwa shangwe kubwa kama nini kwangu kuona jinsi kikundi hicho kilivyofurahi kupokea vichapo vyote vipya na kuona jinsi walivyoitikia kweli za Biblia!

Naanza Utumishi wa Wakati Wote

Mnamo Septemba 1, 1992, niliwekwa kuwa painia, yaani mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Nilifanya kazi ya upainia huko Mahanoro lakini nilikuwa nikiwaandikia barua watu wa ukoo waliokuwa Betoko II. Baada ya muda tulianza kujifunza kupitia barua, nao wakaniomba nirudi kijijini ili niwasaidie. Nilikuwa tayari kufanya hivyo lakini kwanza nilitaka kuhakikisha ikiwa kwa kweli walitaka kujifunza Biblia na kufanya maendeleo ya kiroho. Kwa hiyo kwa muda fulani niliendelea kuishi huko Mahanoro nikifanya upainia.

Mwishoni mwa mwaka wa 1993, nilipata pendeleo la kuhudhuria shule ya mapainia huko Antananarivo. Baadaye niliambiwa nitoe ombi la kuwa painia wa pekee. Kufanya hivyo kungemaanisha kwamba ninaweza kutumwa katika sehemu yoyote nchini. Hata hivyo, sikufanya hivyo kwani nilitaka kuwasaidia watu wa ukoo kule Betoko II, ambao waliishi mbali na makutaniko ya karibu. Kwa hiyo nilirudia mgawo wangu kule Mahanoro.

Wakati mwangalizi anayesafiri wa Mashahidi wa Yehova alipozuru, nilimwuliza kuhusu kurudi kuwasaidia watu wa ukoo. Kufikia wakati huo kutaniko lilikuwa limeanzishwa kule Andranomafana naye alipendekeza kwamba nihamie huko ili nishirikiane na kutaniko hilo na kuhubiri eneo la Betoko II. Nilianza mgawo huo katika Septemba 1, 1994. Mwezi huohuo, nilihudhuria kusanyiko la wilaya pamoja na ndugu yangu Paul, ambaye zamani alikuwa mwalimu wa dini. Baada ya muda watu 30 walikuwa wakihubiri huko Andranomafana, na Jumapili kulikuwa na wastani wa watu 65 waliohudhuria mikutano yetu.

Sikuacha Kutembea

Muda mfupi tu baada ya kurudi Betoko II, ndugu na dada zangu wanne walistahili kuhubiri wakiwa Mashahidi wa Yehova, na baada ya hapo wakabatizwa. Baada ya kurudi Betoko II, nilisafiri kwa ukawaida kwenda Anosibe An’ala, umbali wa kilometa 50, ili kuchukua magazeti. Ingawa ilikuwa safari yenye kuchosha, nilifurahia sana nilipoona ukuzi wa kiroho katika eneo hilo.

Leo kuna kutaniko linalokua katika Betoko II, kukiwa na wastani wa watu 45 wanaohudhuria mikutano Jumapili. Sasa, washiriki wote wa karibu wa familia yetu ni Mashahidi, na wengi wao ni mapainia wa kawaida. Mmoja wa ndugu zangu wadogo ni painia wa pekee. Mnamo Novemba 1, 2001, mimi pia niliwekwa kuwa painia wa pekee, na nilipewa mgawo katika kijiji cha Antanambao-Manampotsy. Lakini nilitoka Betoko II nikiwa na furaha nyingi.

Nilipoanza kujifunza kweli za Biblia mnamo 1987, kulikuwa na Mashahidi wasiozidi 3,000 nchini Madagaska. Sasa kuna Mashahidi zaidi ya 14,000. Sawa na wengi wao, ninashukuru sana kwa pendeleo la kutumia nguvu zangu kufanya mengi zaidi ili kuwasaidia wengine. Nami ninamshukuru Yehova kwa kubariki jitihada zangu.

[Picha katika ukurasa wa 24, 25]

Mara nyingi nilibeba vichapo vyenye uzito wa zaidi ya kilo 15 kwa kilometa 60 hadi kijijini mwetu

[Picha katika ukurasa wa 25]

Ndugu yangu mkubwa Paul

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ndugu yangu Charles

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na washiriki kadhaa wa familia yetu. Kwa sasa hawa wote ni Mashahidi wa Yehova