Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawezaje Kudhibiti Hisia Zangu?

Ninawezaje Kudhibiti Hisia Zangu?

Vijana Huuliza . . .

Ninawezaje Kudhibiti Hisia Zangu?

“Mimi huwakasirikia wazazi wangu na kusema mambo mabaya bila kukusudia. Kisha mimi hujitenga nao hadi ninapohisi vizuri.” —Kate, mwenye umri wa miaka 13.

“Tatizo langu kubwa ni kutojiamini. Nyakati nyingine mimi hujihisi hoi kabisa.”—Ivan, mwenye umri wa miaka 19.

HISIA zina nguvu sana. Hisia huongoza mawazo yako na matendo yako. Zinaweza kukuchochea kufanya mema au mabaya. Nyakati nyingine, zinaweza kukulemea sana. Jacob, mwenye umri wa miaka 20, anasema: “Mimi huhisi kwamba sifai. Mara nyingi, mimi hushindwa kutimiza miradi yangu. Nyakati nyingine mimi hulia, au kukasirika sana na kuwakasirikia wengine. Ni vigumu kudhibiti hisia zangu.”

Hata hivyo, mtu anahitaji kujua jinsi ya kudhibiti hisia zake kadiri anavyoendelea kukomaa na kuwa mtu mzima mwenye kutegemeka. Sasa wataalamu fulani wanasema kwamba uwezo wa kudhibiti hisia na kushughulika na watu ni muhimu kuliko kuwa na akili nyingi. Hata Biblia inaonyesha kwamba ni muhimu sana kudhibiti hisia. Kwa mfano, andiko la Methali 25:28 linasema: “Mtu asiyeweza kuzuia hasira yake, ni kama mji usio na ulinzi unaposhambuliwa.” (Biblia Habari Njema) Kwa nini ni vigumu sana kudhibiti hisia?

Jambo Linalofanya Iwe Vigumu kwa Vijana

Watu wa umri na malezi mbalimbali huona ni vigumu kudhibiti hisia zao. Hata hivyo, inaweza kuwa vigumu zaidi kudhibiti hisia wakati kijana aliyebalehe anapoelekea kuwa mtu mzima. Kitabu Changing Bodies, Changing Lives cha Ruth Bell kinasema: “Vijana wengi waliobalehe huwa na hisia mbalimbali, kama vile hisia za kiajabu, zenye kufurahisha, zenye kuogopesha, na zinazowafanya wachanganyikiwe. Watu wengi huwa na hisia mbalimbali kuhusu kitu fulani wakati uleule. . . . Hisia za mtu zinaweza kubadilika haraka sana.”

Kwa kuwa wewe ni kijana, huna uzoefu mwingi maishani. (Methali 1:4) Kwa hiyo unapokabili hali fulani au magumu fulani kwa mara ya kwanza, huenda ukawa na wasiwasi au ukalemewa sana. Lakini Muumba wako anaelewa jinsi unavyohisi. Hata anajua ‘fikira zinazokufadhaisha.’ (Zaburi 139:23) Katika Neno lake ameonyesha kanuni zinazoweza kukusaidia.

Njia Muhimu za Kudhibiti Hisia

Njia moja ya kudhibiti hisia zako ni kujua kudhibiti mawazo yako. Mawazo mabaya yanaweza kukudhoofisha na kukuzuia usichukue hatua inayofaa. (Methali 24:10) Lakini ni nini kitakachokuwezesha kuwa na mawazo yanayofaa na hivyo kudhibiti hisia zako?

Kwanza, usifikirie mambo yasiyofaa ambayo yanaweza kukuvunja moyo au kukuogopesha. Ukifuata shauri la Biblia la kufikiria mambo ‘mazito’ na ya “uadilifu,” utafaulu kuondoa mawazo yasiyofaa na kuwa na mawazo yanayofaa. (Wafilipi 4:8) Huenda isiwe rahisi kufanya hivyo, lakini ukijitahidi unaweza kufanikiwa.

Fikiria kisa cha msichana anayeitwa Jasmine. Wakati mmoja alisema hivi: “Ninahisi kwamba nimelemewa sana na kila kitu. Nina kazi mpya na madaraka mapya. Najihisi hoi kabisa. Siwezi kupumzika.” Kijana anaweza kuhisi hivyo nyakati nyingine, na hilo linaweza kumfanya aogope na kukosa uhakika. Biblia inatueleza kuhusu kijana aliyeitwa Timotheo, ambaye alistahili kabisa kupata madaraka aliyopewa. Hata hivyo, inaonekana alihisi kwamba hafai kupata madaraka hayo.—1 Timotheo 4:11-16; 2 Timotheo 1:6, 7.

Huenda ukawa na wasiwasi unapopata daraka jipya. Huenda ukasema, ‘Sitaweza kamwe kulitimiza.’ Lakini unaweza kudhibiti hisia hizo za kutojiamini kwa kutofikiria mambo yasiyofaa. Jifunze jinsi unavyoweza kutimiza daraka hilo vizuri. Uliza maswali, na ufuate maagizo.—Methali 1:5, 7.

Kadiri unavyojua jinsi ya kufanya jambo fulani kwa ustadi, ndivyo wasiwasi wako utakavyopungua. Usikazie fikira udhaifu wako kwani kufanya hivyo kutakuzuia usifanye maendeleo. Wakati mmoja mtume Paulo alisema hivi alipochambuliwa: “Hata kama sina ustadi wa kusema, hakika sivyo nilivyo katika ujuzi.” (2 Wakorintho 10:10; 11:6) Vivyo hivyo, unaweza kuwa mwenye uhakika kwa kutambua vipawa vyako na kumwomba Mungu akusaidie kukabiliana na udhaifu wako. Mungu anaweza kukusaidia kama alivyowasaidia watu zamani.—Kutoka 4:10.

Jambo jingine linaloweza kukusaidia kudhibiti hisia zako ni kuweka miradi unayoweza kufikia na kutambua mipaka yako. Pia, epuka kujilinganisha isivyofaa na wengine. Biblia inatupa hili shauri zuri kwenye Wagalatia 6:4: “Lakini kila mmoja na athibitishe kazi yake mwenyewe ni nini, kisha atakuwa na sababu ya kufurahi kwa habari yake mwenyewe peke yake, na si kwa kujilinganisha na mtu yule mwingine.”

Kuzuia Hasira

Ni vigumu pia kudhibiti hasira. Kama Kate, aliyetajwa mwanzoni alivyosema, hasira huwafanya vijana wengi kusema na kufanya mambo yanayoumiza au yanayoweza kudhuru.

Ni kweli kwamba ni jambo la kawaida kukasirika nyakati nyingine. Lakini mkumbuke muuaji wa kwanza, Kaini. ‘Alipowaka hasira,’ Mungu alimwonya kwamba hasira inaweza kumchochea atende dhambi nzito. Mungu alimuuliza Kaini hivi: “Je, wewe utaishinda [dhambi]?” (Mwanzo 4:5-7) Ijapokuwa Kaini hakutii shauri hilo la Mungu, wewe unaweza kudhibiti hasira kwa msaada wa Mungu na kuepuka kutenda dhambi!

Ili uweze kufanya hivyo, unahitaji tena kudhibiti mawazo yako. Biblia inasema hivi kwenye Methali 19:11: “Ufahamu wa mtu hakika hupunguza hasira yake, na ni jambo lenye kupendeza anapopita kosa.” Mtu anapokukasirisha, jaribu kuelewa kwa nini amefanya hivyo. Je, alitaka kukuumiza kimakusudi? Je, alifanya hivyo bila kukusudia au bila kujua? Tunapovumilia makosa ya wengine tunaonyesha kwamba tunaiga rehema ya Mungu, na kufanya hivyo kunaweza kukusaidia kuzuia hasira.

Vipi ikiwa una sababu nzuri ya kukasirika? Maandiko yanasema hivi: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi.” (Waefeso 4:26) Huenda ikafaa kuzungumza na mtu huyo. (Mathayo 5:23, 24) Au huenda ikafaa zaidi kusahau jambo hilo kabisa, kuacha kukasirika, na kuendelea na maisha.

Marafiki wako wanaweza kuathiri jinsi unavyoshughulikia hasira. Ndiyo sababu Biblia inasema: “Usishirikiane na mtu yeyote mwenye mazoea ya kukasirika; wala usiende pamoja na mtu wa mifoko ya ghadhabu, ili usizoee njia yake na hakika uiwekee nafsi yako mtego.”—Methali 22:24, 25.

Ukishirikiana na watu wanaojitahidi kuzuia hasira unaweza kusitawisha sifa ya kujizuia. Makutaniko ya Kikristo ya Mashahidi wa Yehova yana watu wengi kama hao ambao wamekomaa, na wengi wana umri mkubwa na uzoefu kuliko wewe. Jitahidi kufahamiana na baadhi yao. Angalia jinsi wanavyoshughulikia matatizo. Wanaweza kukupa “mwongozo stadi” unapopatwa na matatizo. (Methali 24:6) Jacob, aliyenukuliwa awali, anasema: “Ninathamini sana rafiki yeyote mkomavu anayeweza kunipa mashauri ya Neno la Mungu. Ninapokumbuka kwamba Yehova ananipenda licha ya wasiwasi wangu, mimi hufaulu kujidhibiti na kutulia.”

Hatua Nyingine Zinazofaa

Kitabu kimoja maarufu cha mazoezi kinasema: “Uchunguzi mwingi sana umeonyesha kwamba mtazamo wa mtu hutegemea jinsi anavyosogeza mwili wake. Viwango vya homoni na oksijeni hubadilika mtu anaposongasonga.” Basi, hapana shaka kwamba kuna faida kufanya mazoezi. Biblia inatuambia hivi: “Mazoezi ya mwili yana faida yake.” (1 Timotheo 4:8, BHN) Unaweza kupanga kufanya mazoezi kwa kiasi na kwa ukawaida. Ukifanya hivyo, huenda ukahisi vizuri zaidi. Pia, unaweza kufaidika ukila vyakula bora kwa ukawaida.

Pia chunguza muziki na burudani unayopenda. Uchunguzi uliochapishwa katika gazeti The Harvard Mental Health Letter ulisema: “Kutazama jeuri . . . kunaweza kuamsha hasira za mtu na kumfanya awe mjeuri. . . . Watu waliotazama sinema zenye jeuri walifikiria kuhusu jeuri na shinikizo lao la damu lilipanda.” Basi, chagua kwa hekima kile unachosikiliza na unachotazama.—Zaburi 1:1-3; 1 Wakorintho 15:33.

Hatimaye, njia bora zaidi ya kujua jinsi ya kudhibiti hisia zako ni kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Muumba wako. Anatualika sote tuzungumze naye kupitia sala, kumweleza waziwazi hisia zetu. Mtume Paulo alihimiza hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote.” Kisha akasema: “Maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili.” Naam, unaweza kusitawisha uwezo wa kukabiliana na hali yoyote maishani. Mtume Paulo alisema hivi pia: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:6, 7, 13.

Msichana mmoja anayeitwa Malika anasema: “Nimejifunza kusali tena na tena. Kujua kwamba Yehova anajali hunisaidia kutulia na kudhibiti hisia zangu.” Kwa msaada wa Mungu, wewe pia unaweza kujifunza kudhibiti hisia zako.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Njia moja ya kudhibiti hisia zako ni kujua kudhibiti mawazo yako

[Picha katika ukurasa wa 20]

Ukishirikiana na wale wenye umri mkubwa unaweza kujifunza kudhibiti hisia zako