Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Yuko Kila Mahali?

Je, Mungu Yuko Kila Mahali?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Yuko Kila Mahali?

INAFAA kusema kwamba Mungu anaweza yote na anajua yote. Hata hivyo, ili kuonyesha ukuu wake, watu fulani husema kwamba Mungu yuko kila mahali. Wao huamini kwamba Mungu yuko kila mahali wakati uleule.

Wazo la kwamba Mungu anaweza yote na anajua yote huungwa mkono na Biblia. (Mwanzo 17:1; Waebrania 4:13; Ufunuo 11:17) Bila shaka, Mungu ni mweza yote na anajua yote kwani hakuna kitu kisichokuwa dhahiri machoni pake. Hata hivyo, je, yeye yuko kila mahali, au ana makao halisi?

Mungu Yuko Wapi?

Mistari mbalimbali katika Biblia husema kwamba ‘mbingu’ ni ‘makao ya Mungu yaliyofanywa imara.’ (1 Wafalme 8:39, 43, 49; 2 Mambo ya Nyakati 6:33, 39) Hata hivyo, simulizi moja la Biblia hufafanua ukuu wa Yehova Mungu kwa maneno haya: “Je, kweli Mungu atakaa pamoja na wanadamu duniani? Tazama! Mbingu, ndiyo, mbingu za mbingu, haziwezi kukutosha.”—2 Mambo ya Nyakati 6:18.

Biblia husema kwamba “Mungu ni Roho.” (Yohana 4:24) Hivyo, yeye huishi katika makao ya kiroho mbali na ulimwengu unaoonekana. Biblia inaposema kuwa ‘mbingu’ ni makao ya Mungu, hiyo hufafanua ukuu wa makao yake yaliyo tofauti sana na makao yetu. Biblia hufundisha jambo muhimu inapoonyesha kwamba makao ya Mungu ni tofauti kabisa na ya wanadamu na kwamba Mungu huishi mahali fulani hususa.—Ayubu 2:1-2.

Mungu Ni Mtu

Yesu alieleza kuhusu makao ya Yehova alipowaambia wanafunzi wake: “Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi. . . . ninaenda kuwatayarishia ninyi mahali.” (Yohana 14:2) Yesu alienda wapi? Hatimaye, Yesu “aliingia mbinguni kwenyewe, ili sasa aonekane mbele za uso wa Mungu kwa ajili yetu.” (Waebrania 9:24) Simulizi hilo hutufundisha mambo mawili muhimu. Kwanza, Mungu ana makao halisi. Pili, Mungu ni mtu wala si kani isiyo isiyoweza kufafanuliwa iliyo kila mahali.

Kwa sababu hiyo, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake kusema “Baba yetu uliye mbinguni,” wanaposali kwa Yehova, ambaye ni mtu aliye mahali fulani hususa, yaani, katika makao ya kiroho mbinguni. (Mathayo 6:9; 12:50) Fundisho hilo linapatana na jinsi watu wa Mungu walivyokuwa wamefundishwa kusali yapata miaka 1,500 mapema. Sala hii inapatikana katika maandishi ya kale zaidi yaliyoongozwa na Mungu: “Utazame chini kutoka katika makao yako matakatifu, mbinguni, na kuwabariki watu wako.”—Kumbukumbu la Torati 26:15.

Roho ya Mungu Huwafikia Wote Popote Walipo

Ijapokuwa Biblia husema kwamba Mungu ana makao hususa, hiyo huonyesha kwamba roho takatifu yaweza kuwa kila mahali. Mtunga-zaburi Daudi aliuliza hivi: “Ni wapi ninapoweza kwenda mbali na roho yako, na ni wapi ninapoweza kukimbilia mbali na uso wako?” (Zaburi 139:7) Taarifa kama hizo zimewatatanisha watu fulani na kuwafanya wafikiri kwamba Mungu yuko kila mahali. Hata hivyo, tunapochunguza muktadha wa andiko hilo na wa maandiko mengine, tunatambua kwamba roho takatifu ya Yehova, yaani, nguvu zake zikiwa katika hali ya kutumika, zinaweza kutoka mahali hususa alipo Mungu na kwenda mahali popote katika ulimwengu.

Kama mkono wa baba unavyonyooshwa ili kumbembeleza na kumtegemeza mtoto, ndivyo mkono wa Yehova, yaani roho takatifu, inavyoenea katika sehemu yoyote ya makao ya kiroho na ya kimwili ili kutimiza makusudi ya Yehova. Hivyo, Mtunga-zaburi angeweza kusema hivi: “Kama ningechukua mabawa ya mapambazuko, ili nipate kuishi katika bahari ya mbali sana, huko, pia, mkono wako ungeniongoza nao mkono wako wa kuume ungenishika.”—Zaburi 139:9, 10.

Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu

Kwa upendo Yehova Mungu amejishusha na kutueleza yeye ni mtu wa aina gani na jinsi makao yake yalivyo, na amefanya hivyo kwa njia iliyo wazi sana na inayoeleweka vizuri na mwanadamu. Kwa kufanya hivyo ni kana kwamba kwa njia ya mfano Yehova “anajishusha kutazama mbingu na dunia.” (Zaburi 113:6) Hata hivyo, wanadamu hawawezi kuelewa kwa ukamili jinsi Mungu alivyo.

Yehova ametukuka sana, ni mkuu sana, na ni wa ajabu sana hivi kwamba haiwezekani kufafanua kikamili jinsi alivyo kwa maoni ya wanadamu. Hivyo, ingawa Biblia hueleza kuhusu makao hususa ya Mungu yaliyoko mbinguni, sisi hatuwezi kufahamu kwa ukamili jinsi makao hayo ya kiroho yalivyo.—Zaburi 139:6.

Hata hivyo, tunafurahi sana kufahamu kwa kiasi fulani utu wa Yehova na kutambua kwamba yeye si nguvu fulani isiyo na utu na isiyoeleweka. Yeye ni mtu aliye na makao hususa na sifa mbalimbali kama vile upendo na huruma. Ujuzi huo hutuwezesha kuwa na uhusiano bora zaidi, yaani, urafiki wa kibinafsi na wa kudumu pamoja na Mweza-Yote aliye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote.—Yakobo 4:8.