Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Mtoto Aliyeharibika Uso Niliguswa sana na simulizi la Mailyn. (“Mailyn Atapata Uso Mpya,” Mei 22, 2004) Nilitiwa moyo sana niliposoma jinsi msichana huyo wa miaka 11 anavyowaeleza wengine kuhusu tumaini lake linalotegemea Biblia licha ya kwamba anakabiliana na ugonjwa mbaya.

M. B., Italia

Mtazamo unaofaa wa Mailyn na familia yao ulinitia moyo sana. Leo vyombo vya habari hukazia kupita kiasi umuhimu wa kuwa na sura nzuri. Jambo hilo linaweza kuvunja moyo sana. Ningependa kumjulisha Mailyn kwamba ninaona wazi urembo wake wa kweli. Ninatumaini kwamba nitashangilia pamoja naye wakati Yehova atakapompa uso mpya katika ulimwengu mpya. Imani yake imeniimarisha.

M. S., Marekani

Hivi karibuni nitafanyiwa upasuaji ili kuondolewa titi moja. Wakati ugonjwa unapoathiri sura yako, unahitaji nguvu na ujasiri ili usikate tamaa. Ujasiri na mtazamo wa Mailyn uliniimarisha. Ninamwambia Mailyn hivi: Ninakutakia mema. Ninakuona kuwa mrembo!

G. R., Ufaransa

Nilizaliwa nikiwa na kasoro ya mwili ambayo hufanya mdomo wa juu ujigawe. Shuleni watoto wengi waliniangalia vibaya. Wengine hata walinitemea mate. Ninafikiri kwamba mambo ambayo mama alinifundisha katika Biblia yalinipa ujasiri na uhakika. Hata sasa, nikiwa na umri wa miaka 31 mimi huhuzunishwa na uso wangu. Kwa hiyo nilipendezwa sana na simulizi la Mailyn. Ninajua kwamba kwa msaada wa Yehova tunaweza kukabiliana na mambo yoyote yatakayotupata.

T. S., Japani

Mailyn alinihakikishia kwamba furaha na uradhi hazitokani na umbo la mtu. Zinapatikana tu tunapomtumikia na kumpenda Mungu wetu. Mfano wa Mailyn unanichochea.

A. T., Ufilipino

Kudhulumiwa Wakati wa Uchumba Ninashukuru sana kwa ajili ya makala yenye kichwa “Vijana Huuliza . . . Jamani! Mbona Ananitesa?” (Mei 22, 2004) Mchumba wangu alikuwa akinidhulumu. Mambo yalipoenda mrama mchumba wangu alinilaumu. Katika familia yetu watu walikuwa wenye jeuri na walitukanana, kwa hiyo tabia yake ilionekana kuwa ya kawaida. Ninafurahi kwamba nimevunja uhusiano huo; ameonyesha kwamba hastahili kuwa mwenzi wangu wa ndoa.

Jina limebanwa, Belize

Makala hiyo ilieleza jinsi ninavyohisi. Kabla na baada ya ndoa yangu, nilipatwa na hali mbalimbali zilizoelezwa katika makala hiyo. Nilidhulumiwa sana kiasi cha kwamba niliacha kujiheshimu. Ninatumaini makala hiyo itawasaidia wengi wachunguze uhusiano wao wanapochumbiana. Ni jambo la hekima sana kufahamiana kabla ya kuoana ili kuepuka matatizo kama hayo.

M. M., Ujerumani

Mbegu Zinazosafiri Asanteni sana kwa kuchapisha makala yenye kichwa “Mbegu Inayosafiri Baharini.” (Mei 22, 2004) Miaka kadhaa iliyopita niliokota mbegu moja kama hizo kwenye ufuo karibu na nyumba yangu, lakini sikujua kwamba ilikuwa mbegu. Niliposoma makala hiyo nilishangaa kujua kwamba nilikuwa nimeokota mbegu ambayo labda ilikuwa imesafiri kutoka Afrika ya Kati au Afrika Magharibi! Asanteni sana kwa kuchapisha makala kama hizo zenye kupendeza.

M. K., Japani