Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Upweke Nilichochewa kuwaandikia baada ya kusoma mfululizo wenye kichwa “Kuwa Peke Yako Bila Kuhisi Upweke.” (Juni 8, 2004) Mwanzoni, mfululizo huo haukunipendeza. Lakini nilipoanza kusoma nilitambua kwamba mimi sionyeshi hisia zangu. Madokezo yaliyotolewa ndiyo niliyohitaji.

A. V., Marekani

Nina ugonjwa wa kifafa na kushuka moyo, kwa hiyo mara nyingi mimi hulala kwa sababu ya dawa ninazotumia. Mara nyingi mimi huhisi upweke na kukosa furaha. Makala hizo zilinisaidia kujua kwamba hata tunapohisi upweke, hatuko peke yetu.

J. C., Marekani

Nina umri wa miaka 14 na wakati fulani nilitaka kukubaliwa na wanadarasa wenzangu. Nilifikiri wao ni marafiki wangu. Hata hivyo, walipoona kwamba niko tofauti kwa kuwa mimi ni Mkristo, nilitambua kwamba wangeniacha ikiwa singebadilika niwe kama wao. Sasa ninatambua kwamba marafiki wa kweli, wazee kwa vijana, wanaweza kupatikana tu katika kutaniko la Kikristo.

N. C., Hispania

Mfululizo huo ulinisaidia kuelewa kwa nini nilihisi vibaya mume wangu aliposafiri kwa ajili ya shughuli za kazi na kuniacha peke yangu. Ushauri wenu kuhusu uhitaji wa kuona upweke kuwa jambo la kawaida na kuzungumza na rafiki mkomavu limenisaidia sana.

J. H., Jamhuri ya Cheki

Hivi karibuni nitahamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri. Mama yangu anafurahia jambo hilo lakini nyakati nyingine yeye huhisi upweke. Nilipata makala hizo nilipokuwa nikifikiria jinsi ya kushughulikia hali hiyo. Sasa ninapanga kuwasiliana na mama yangu kwa ukawaida, na kumweleza jinsi ninavyofurahia utumishi.

N. K., Japani

Mnara wa London Makala yenye kichwa “Mnara wa London—Jengo la Ukumbusho la Nyakati za Maasi” ilikuja wakati unaofaa. (Juni 8, 2004) Mwalimu wangu na wanafunzi kadhaa wa shule yetu walikuwa wamerudi tu kutoka London. Makala hiyo ilinisaidia kuwazia jinsi London ilivyo, bila gharama!

P. L., Ujerumani

Mahangaiko Hivi majuzi nilichoka sana kwa sababu ya mahangaiko. Nilihisi vibaya zaidi nilipowazia kwamba hali hiyo ilisababishwa na kukosa imani. Nilishukuru sana nilipoona makala yenye kichwa “Maoni ya Biblia: Je, Kuhangaika Kunaonyesha Kwamba Mtu Hana Imani?” (Juni 8, 2004) Kila wakati ninapokuwa na wasiwasi Yehova hunitia moyo.

Y. I., Japani

Idadi ya Watu Katika makala yenye kichwa “Idadi ya Watu, Biblia, na Wakati Ujao,” mnasema kwamba Waisraeli walitoka Misri baada ya miaka 215. (Mei 8, 2004) Lakini Kutoka 12:40, 41 inasema ilikuwa miaka 430.

R. C., Marekani

“Amkeni!” linajibu: Kutoka 12:40 inasema: “Na kukaa kwa wana wa Israeli, waliokuwa wamekaa katika Misri, kulikuwa miaka 430.” Ona kwamba “kukaa kwa wana wa Israeli” hakumaanishi tu wakati ambapo Wayahudi walikaa Misri; bali, ni wazi kwamba inamaanisha kipindi chote kilichoanza wakati Abrahamu aliingia katika nchi ya Kanaani. Mtume Paulo alionyesha kwamba kipindi hicho cha miaka 430 kilianza wakati agano pamoja na Abrahamu lilipohalalishwa. (Wagalatia 3:16, 17) Hilo lilitukia wakati ambapo Abrahamu aliingia Kanaani mwaka wa 1943 K.W.K. Kronolojia ya Biblia inaonyesha kwamba hilo lilitukia miaka 215 kabla ya Wayahudi kuhamia Misri. Basi inamaanisha kwamba Wayahudi ‘walikaa Misri’ kwa miaka 215 inayobaki.”—Ona makala yenye kichwa “Chronology,” katika Buku la Kwanza la “Insight on the Scriptures,” kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.