Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Nifanye Kazi za Mikono?

Kwa Nini Nifanye Kazi za Mikono?

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Nifanye Kazi za Mikono?

“Sikuwahi kuwazia kwamba ningefanya kazi za mikono. Nilifurahia sana kucheza na kompyuta yangu.”—Nathan.

“Vijana fulani walitudharau sisi tuliofanya kazi za mikono, kwani walifikiri tulikuwa wajinga na hivyo hatungeweza kufanya kazi nyingine yoyote.”—Sarah.

KAZI ZA MIKONO—watu wengi huziona kazi za mikono kuwa za kuchosha, chafu, na zisizopendeza. Profesa fulani wa uchumi anasema hivi kuzihusu: “Kazi hizo haziwafanyi watu watambuliwe katika ulimwengu huu unaozingatia sana cheo.” Hivyo, haishangazi kwamba vijana wengi hudhihaki hata wazo lenyewe la kufanya kazi za mikono.

Hata hivyo, Biblia hutuhimiza kuwa na maoni yanayofaa kuhusu kazi ngumu. Mfalme Sulemani alisema hivi: “Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kwamba ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.” (Mhubiri 2:24) Katika nyakati za Biblia, Waisraeli walikuwa wakulima. Kazi ya kulima, kuvuna, na kupura nafaka ilikuwa ngumu sana. Hata hivyo, Sulemani alisema kwamba kazi ngumu inaweza kumfurahisha mtu.

Karne kadhaa baadaye, mtume Paulo alisema hivi: “Mwizi asiibe tena, bali afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema.” (Waefeso 4:28) Paulo alizoea kufanya kazi ngumu. Ijapokuwa alikuwa na elimu nyingi, mara kwa mara alitengeneza mahema ili kujiruzuku.—Matendo 18:1-3.

Wewe huonaje kazi za mikono? Amini usiamini, kazi za mikono zinaweza kukunufaisha sana.

Mazoezi Muhimu Maishani

Ukifanya kazi ngumu kwa bidii, kama vile useremala au kukata nyasi, utakuwa na afya nzuri. Hata hivyo, kuna faida nyingine nyingi. Je, unaweza kurekebisha gurudumu la baiskeli lililotoboka? Je, unaweza kurekebisha dirisha lililovunjika au kuzibua mtaro ulioziba? Je, unajua kupika? Je, unaweza kusafisha nyumba? Vijana wanapaswa kujifunza kufanya kazi kama hizo. Wakifanya hivyo, watafanikiwa baadaye maishani watakapokuwa wakiishi peke yao.

Inapendeza kujua kwamba Yesu Kristo alijifunza kazi fulani za mikono alipokuwa duniani. Yosefu, ambaye alikuwa baba yake wa kambo, alimfunza useremala, na ndiyo sababu watu walimwita Yesu seremala. (Mathayo 13:55; Marko 6:3) Wewe pia unaweza kujifunza mambo mengi kwa kufanya kazi mbalimbali za mikono.

Kusitawisha Sifa Nzuri

Kufanya kazi ngumu kunaweza kuathiri maoni yako kujihusu. Dakt. Fred Provenzano akiandika kwa niaba ya Kituo cha Afya ya Akili na Elimu cha Marekani alisema kwamba kujifunza kazi fulani ya mikono kunaweza kukufanya “uhisi unaweza kujitegemea na hukufanya ujiamini zaidi,” na vilevile “kuwa na mipaka na utaratibu, mambo ambayo ni muhimu ili kupata kazi.” Kijana fulani anayeitwa John anasema hivi: “Kazi za mikono hukuzoeza kuwa na subira na kukufunza kutatua matatizo kwa kuyashughulikia.”

Sarah, aliyetajwa mwanzoni, anasema: “Kufanya kazi za mikono kulinizoeza kuwa na bidii. Nilijifunza kujidhibiti kiakili na kimwili.” Je, ni lazima tuchoshwe na kazi ngumu? Nathan anasema: “Nilijizoeza kufurahia kufanya kazi kwa mikono yangu. Kazi yangu ilikuwa nzuri zaidi kadiri nilivyoboresha ustadi wangu. Hilo lilinifanya nijiheshimu.”

Isitoshe, ukifanya kazi za mikono utajifunza kuridhika. Kijana anayeitwa James anasema hivi: “Mimi hufurahia useremala. Ingawa kazi hiyo huchosha, ninaweza kutazama vitu ambavyo nimetengeneza na kuona yale ambayo nimetimiza. Hilo hunipa uradhi.” Brian, ana maoni hayohayo. Anasema hivi: “Mimi hufurahia kutengeneza magari. Mimi huridhika na kujiamini zaidi ninapojua kwamba ninaweza kutengeneza kitu kilichoharibika na kukifanya kionekane kipya.”

Utumishi Mtakatifu

Kufanya kazi ngumu kunaweza kuwasaidia vijana Wakristo wanapomtumikia Mungu. Mfalme Sulemani alipoagizwa amjengee Yehova hekalu kubwa, alitambua kwamba kazi hiyo ingehitaji jitihada nyingi na ustadi mwingi sana. Biblia inasema: “Mfalme Sulemani akatuma watu na kumleta Hiramu kutoka Tiro. Yeye alikuwa mwana wa mwanamke mjane kutoka katika kabila la Naftali, na baba yake alikuwa mwanamume Mtiro, fundi wa shaba; naye alikuwa amejaa hekima na uelewaji na ujuzi kwa ajili ya kufanya kila kazi ya kutumia shaba. Basi akaja kwa Mfalme Sulemani, akaanza kufanya kazi yake yote.”—1 Wafalme 7:13, 14.

Hiramu alipata pendeleo kubwa sana la kutumia ustadi wake kutegemeza ibada ya Yehova. Kisa cha Hiramu huonyesha ukweli wa maneno ya Biblia yanayopatikana katika Methali 22:29: “Je, umemwona mtu stadi katika kazi yake? Yeye atasimama mbele ya wafalme; hatasimama mbele ya watu wa kawaida.”

Leo, hata vijana wasiokuwa na ujuzi wa ujenzi wameshiriki kujenga Majumba ya Ufalme. Kwa kujihusisha katika kazi mbalimbali, vijana hao wamejifunza kazi muhimu kama vile ufundi wa umeme, ufundi wa mabomba, uashi, na useremala. Unaweza kuwauliza wazee wa kutaniko lenu ikiwa unaweza kushiriki katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme.

James, ambaye ameshiriki kujenga Majumba kadhaa ya Ufalme, anasema hivi: “Wengi kutanikoni huenda wasiwe na wakati wala ustadi unaohitajiwa. Hivyo, unaposhiriki katika ujenzi, unasaidia kutaniko zima.” Nathan, alijifunza kutumia saruji katika ujenzi, na hilo lilimpa nafasi nyingine ya kumtumikia Mungu. Anaeleza hivi: “Nilisafiri kwenda Zimbabwe na kutumia ujuzi wangu katika ujenzi wa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Nilifanya kazi huko kwa miezi mitatu na hilo lilikuwa mojawapo ya mambo muhimu sana maishani mwangu.” Kwa sababu wanatamani sana kufanya kazi ngumu, vijana wengine wameomba kutumikia wakiwa watumishi wa kujitolea kwenye ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova nchini mwao.

Isitoshe, ukiwa na ustadi wa kufanya kazi za mikono, unaweza ‘kujitosheleza.’ (1 Timotheo 6:6) Vijana wengi ambao ni Mashahidi wa Yehova hutumikia wakiwa mapainia, yaani wahudumu wa wakati wote. Kujifunza kazi fulani kumewawezesha baadhi yao kujiruzuku, bila kutumia muda mrefu na pesa nyingi ili kupata elimu.

Jinsi ya Kujifunza

Bila shaka, unaweza kunufaika kwa kujua kazi za mikono iwe unajifunza kazi hizo ili kujiruzuku au kutumia ustadi huo nyumbani. Unaweza kufunzwa kazi hizo shuleni. Au labda, unaweza kujifunza kazi hizo nyumbani. Jinsi gani? Kwa kufanya kazi za nyumbani. Dakt. Provenzano, aliyetajwa mapema, anaandika hivi: “Kazi za nyumbani huwafaidi hasa vijana kwa kuwapa ustadi muhimu sana ambao utawanufaisha watakapokuwa wakiishi mbali na wazazi.” Hivyo, uwe macho ili uone kazi zinazohitaji kufanywa. Je, kuna nyasi zinazohitaji kukatwa au kiti kinachohitaji kurekebishwa?

Badala ya kukushushia heshima, kufanya kazi za mikono kutakunufaisha sana. Usiepuke kazi za mikono! Badala yake, jitahidi “kuona mema” kwa ajili ya kazi yako ngumu, kwani Mhubiri 3:13 husema kwamba “hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.”

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Kujifunza kazi fulani kumewawezesha vijana wengi wamtumikie Mungu zaidi

[Picha katika ukurasa wa 22]

Mara nyingi wazazi wako wanaweza kukufunza kazi fulani muhimu