Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Atakayeiokoa Milima?

Ni Nani Atakayeiokoa Milima?

Ni Nani Atakayeiokoa Milima?

KATIKA mwaka wa 2002, Kongamano la Ulimwengu la Milima lilifanywa kwa siku nne huko Bishkek nchini Kyrgyzstan (Asia ya kati). Huo ulikuwa mkutano wa kwanza wa kimataifa kuhusu milima. Wadhamini wa mkutano huo walitumaini kwamba mwaka wa 2002 ungekuwa “mwanzo wa enzi mpya, wakati ambapo watu wangetambua umuhimu wa milima.”

Katika kongamano hilo, “Sera za Milima za Bishkek” ziliidhinishwa. Sera hizo zinatia ndani maagizo kwa ajili ya kila mtu anayehusika katika kuhifadhi milima. Kusudi la sera hizo ni “kuboresha maisha ya watu wanaoishi milimani, kuhifadhi mazingira ya milima, na kutumia mali za asili zinazopatikana milimani kwa njia bora zaidi.”

Maendeleo fulani yamefanywa. Ulimwenguni pote, kuna mbuga za kitaifa zinazolinda maeneo yenye kuvutia sana na yenye jamii nyingi za viumbe. Katika sehemu nyingi za ulimwengu, vikundi vya wanamazingira vimefaulu kwa kadiri fulani kuzuia uharibifu wa mazingira. Mradi mmoja uliopendekezwa katika Kongamano la Milima huko Bishkek ulihusu jitihada kabambe za kuondoa takataka za nyuklia katika milima ya Kyrgyzstan. Takataka hizo zenye sumu hatari zingechafua vyanzo vya maji yanayotumiwa na asilimia 20 ya watu huko Asia ya kati.

Hata hivyo, bado miradi ya kuhifadhi milima inakabili matatizo makubwa. Kwa mfano, mwaka wa 1995, viongozi huko Kanada walianzisha “Sheria ya Misitu” ili kulinda msitu wa mvua uliobaki huko British Columbia. Hata hivyo, uchunguzi uliofanywa baadaye ulionyesha kwamba kampuni za kukata miti zilipuuza sheria hiyo na kuendelea kukata miti hata katika maeneo yenye miinuko mikali. Sheria hiyo ililegezwa mwaka wa 1997 kwa sababu wafanyabiashara wa mbao walisema kwamba inawalemea sana.

Matatizo yanayoikabili milima hayasababishwi tu na shughuli za kibiashara. Azimio la mwisho katika Kongamano la Bishkek lilionyesha kwamba vita, umaskini, na njaa huchangia uharibifu wa milima unaoendelea. Milima na sehemu nyingine za dunia zitaendelea kuharibiwa mpaka visababishi vyote vya uharibifu wa mazingira vitakapokomeshwa.

Mungu Anajali Uumbaji Wake

Licha ya hali hizo zenye kusikitisha, tuna sababu ya kuwa na tumaini. Mungu Mweza-Yote anajua mambo yanayokabili uumbaji wake. Biblia humfafanua kuwa Yule “ambaye vilele vya milima ni vyake.” (Zaburi 95:4) Yeye pia huwajali wanyama wa milimani. Kwenye Zaburi 50:10, 11, Yehova anasema hivi: “Kila mnyama wa mwituni ni wangu, wanyama walio juu ya milima elfu moja. Najua vizuri kila kiumbe chenye mabawa cha milimani, na makundi ya wanyama wa porini yako pamoja nami.”

Je, Mungu ana njia ya kuokoa mazingira ya ulimwengu yaliyomo hatarini? Bila shaka! Biblia inasema kwamba ‘ameusimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe.’ (Danieli 2:44) Yesu Kristo, Mtawala aliyewekwa rasmi wa serikali hiyo ya mbinguni, anaijali sana dunia na wakaaji wake. (Methali 8:31) Utawala wake utaleta amani duniani, utakomesha matumizi yote mabaya ya mali za asili, na kurekebisha maeneo ya dunia yaliyoharibiwa.—Ufunuo 11:18.

Ikiwa unatamani sana suluhisho hilo, bila shaka utaendelea kusali kwamba ‘Ufalme wa Mungu uje.’ (Mathayo 6:9, 10) Hapana shaka sala hizo zitajibiwa. Karibuni, Ufalme wa Mungu utakomesha ukosefu wa haki na kurekebisha maeneo ya dunia yaliyoharibiwa. Wakati huo, kwa njia ya mfano, milima ‘itapiga vigelegele kwa shangwe.’—Zaburi 98:8.