Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Hukubali Ndoa Kati ya Watu wa Jinsia Moja?

Je, Mungu Hukubali Ndoa Kati ya Watu wa Jinsia Moja?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Hukubali Ndoa Kati ya Watu wa Jinsia Moja?

WAKATI ibada ya kanisa inapoendelea, wanaume wawili wanasimama wakiwa wameshikana mikono mbele ya kasisi maarufu wa Kanisa la Episkopali. Wanafanya “agano . . . mbele za Mungu na kanisa.” Akiwa amevaa vazi lililopambwa sana la rangi ya dhahabu-nyeupe, kasisi huyo anabariki ndoa yao waziwazi. Baada ya hapo, wenzi hao wanakumbatiana na kubusiana na wanapigiwa makofi. Kulingana na kasisi huyo, ndoa kama hizo za watu wa jinsia moja “ni takatifu na zinastahili kubarikiwa, . . . zinastahili kuitwa: takatifu.”

Hata hivyo, viongozi wengine wa kidini wanapinga kabisa ndoa kati ya watu wa jinsia moja. “Tumesikitishwa sana na uamuzi wa [kasisi] huyo,” akasema Cynthia Brust, mnenaji wa Baraza la Kianglikana la Marekani, ambalo ni kikundi cha Waepiskopali wasiopenda mabadiliko. Aliongeza hivi: “Kubariki ndoa kati ya watu wa jinsia moja kunapingana na mafundisho ya Biblia yaliyo wazi kuhusu ndoa na ngono [ambazo] zinaruhusiwa tu kati ya mwanamume na mwanamke waliounganishwa katika ndoa takatifu.”

Mjadala mkali kuhusu suala hilo hauzushwi tu katika dini. Mijadala mikali ya kisiasa inafanywa katika nchi nyingi kwa sababu kuna athari kubwa za kijamii, kisiasa, na kiuchumi ambazo zinahusu malipo ya uzeeni, mwenzi mmoja kunufaika na mpango wa bima ya afya wa mwenzake, na kodi.

Mara nyingi masuala yanayohusu haki za msingi za raia na kutambuliwa kisheria ni tata mno nazo hutokeza tofauti za maoni miongoni mwa umma. Wakristo wa kweli wanapaswa kuwa waangalifu ili kudumisha msimamo wa kutokuwamo kwa kuepuka mijadala ya kisiasa. (Yohana 17:16) * Hata hivyo, watu fulani ambao wanaiheshimu Biblia hutatanishwa na suala la ndoa kati ya watu wa jinsia moja na ngono kati ya watu wa jinsia moja. Unaonaje ndoa kati ya watu wa jinsia moja? Mungu ameweka kiwango gani cha ndoa? Maoni yako huathirije uhusiano wako pamoja na Mungu?

Muumba Wetu Huweka Kiwango

Muumba wetu aliweka sheria za kuongoza ndoa muda mrefu kabla serikali hazijaanza kufanya hivyo. Kitabu cha kwanza katika Biblia kinatuambia hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Kulingana na kichapo Vine’s Expository Dictionary of Biblical Words, neno la Kiebrania “mke, linamaanisha mtu wa kike.” Yesu alithibitisha kwamba wale wanaounganishwa katika ndoa wanapaswa kuwa “mwanamume na mwanamke.”—Mathayo 19:4.

Kwa hiyo, Mungu alikusudia ndoa idumu na iwe kifungo cha karibu sana kati ya mwanamume na mwanamke. Wanaume na wanawake wameumbwa wakamilishane ili waweze kutimiziana mahitaji yao ya kihisia-moyo, kiroho, na mahitaji na tamaa zao za ngono.

Simulizi linalojulikana sana la Biblia kuhusu Sodoma na Gomora linaonyesha maoni ya Mungu kuhusu ngono kati ya watu wa jinsia moja. Mungu alisema: “Kilio cha malalamiko juu ya Sodoma na Gomora ni kikubwa, na dhambi yao ni nzito sana.” (Mwanzo 18:20) Upotovu wa kiadili wa wakati huo ulidhihirika wakati wageni wawili walipomtembelea Loti mwadilifu. “Wanaume wa Sodoma . . . wakaizingira nyumba kuanzia mvulana mpaka mzee, watu wote wakiwa kikundi kimoja. Nao wakaendelea kumwita Loti na kumwambia: ‘Wako wapi wale wanaume ambao waliingia kwako usiku wa leo? Walete nje kwetu ili tulale nao.’” (Mwanzo 19:4, 5) Biblia inasema: “Watu wa Sodoma walikuwa wabaya nao walikuwa wakimtendea Yehova dhambi nzito.”—Mwanzo 13:13.

Wanaume hao ‘waliwakiana tamaa kali katika uchu wao kuelekeana wao wenyewe, wanaume kwa wanaume.’ (Waroma 1:27) Walikuwa ‘wamezidi mno na kwenda kufuatilia mwili kwa ajili ya matumizi yasiyo ya asili.’ (Yuda 7) Katika nchi ambako kampeni za kupigania haki za watu wanaofanya ngono na wenzao wa jinsia moja zimeenea, huenda wengine wasikubali kutumia maneno ‘-siyo ya asili’ kufafanua tabia ya kufanya ngono na mtu wa jinsia moja. Hata hivyo, Mungu ndiye mwamuzi wa mwisho kuhusiana na mambo yanayopatana na asili. Aliwaagiza hivi watu wake wa kale: “Nawe usilale na mwanamume kama vile unavyolala na mwanamke. Ni jambo lenye kuchukiza.”—Mambo ya Walawi 18:22.

Daraka Lako Mbele za Mungu

Biblia inaonyesha waziwazi jambo hili: Mungu haungi mkono wala haruhusu tabia ya kufanya ngono na mtu wa jinsia moja. Pia yeye hapendezwi na watu ‘wanaokubaliana na wale wanaozoea kuzifanya.’ (Waroma 1:32) Nayo “ndoa” haiwezi kufanya zoea hilo liheshimike. Mwongozo wa Mungu kwamba ‘ndoa iheshimiwe na wote’ hautii ndani ndoa kati ya watu wa jinsia moja ambazo humchukiza.—Waebrania 13:4.

Hata hivyo, kwa msaada wa Mungu, mtu yeyote anaweza kujifunza ‘kujiepusha na uasherati,’ ambao unatia ndani ngono kati ya watu wa jinsia moja, na “ajue jinsi ya kukiweza chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima.” (1 Wathesalonike 4:3, 4) Ni kweli kwamba si rahisi kufanya hivyo. Nathan *, ambaye zamani alikuwa na zoea la kufanya ngono na watu wa jinsia yake, alisema: “Nilifikiri kwamba singeweza kuacha zoea hilo kamwe.” Lakini alibadilika kwa msaada wa “roho ya Mungu wetu.” (1 Wakorintho 6:11) Nathan alitambua kwamba Yehova anaweza kutatua tatizo lolote na kumpa mtu nguvu na msaada anaohitaji ili kutimiza viwango Vyake na kupata baraka Zake.—Zaburi 46:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Hata kama sheria za nchi zinapingana na dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia, Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na maandamano au kampeni zozote za kisiasa za kubadili sheria hizo.

^ fu. 14 Si jina lake halisi.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]

Photo by Chris Hondros/Getty Images