Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Je, Wafungwa Wanaweza Kurekebishwa?”

“Je, Wafungwa Wanaweza Kurekebishwa?”

“Je, Wafungwa Wanaweza Kurekebishwa?”

Hilo ndilo swali lililokuwa kwenye jalada la toleo la “Amkeni!” la Mei 8, 2001. Wasomaji wengi walionyesha uthamini wao kwa ajili ya mfululizo wa makala hizo, ambazo zilitia ndani ripoti moja kuhusu programu ya ufundishaji inayotegemea Biblia ambayo inaendeshwa na Mashahidi wa Yehova katika gereza kuu la Atlanta, Georgia, Marekani. Haya ni baadhi ya maelezo kutoka katika barua hizo nyingi zilizopokewa.

▪ “Kwa kuwa nimekuwa mfungwa kwa miaka minane iliyopita, nimeona kwamba kazi ya kufundisha Biblia ambayo inafanywa na Mashahidi wa Yehova katika magereza imefanikiwa kwelikweli. Nilipokuwa gerezani huko Atlanta, nilipata pendeleo la kufanya kazi pamoja na ndugu watano kati ya wale walioonyeshwa kwenye makala yenu. Nilishukuru sana kwa ajili ya upendo na utegemezo wao. Ninawashukuru ndugu kama hao ambao hutuonyesha upendo sisi ambao tumekosea lakini tunajaribu kujirekebisha na kuwa watu bora.”—R. J.

▪ “Kwa sasa niko gerezani, na ndugu kutoka kwenye Jumba la Ufalme lililo karibu walipanga programu nzuri sana ya ufundishaji. Kwa sababu hiyo, mfungwa mwenzangu amebatizwa, nami ingawa nilikuwa nimetengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo wakati fulani, sasa nimerudishwa. Wengine wengi wanajifunza Biblia. Inatia moyo sana kujua kwamba tunashiriki katika kazi ya kufundisha watu duniani pote. Inapendeza sana kumtumikia Yehova, bila kujali mahali tulipo.”—J. M.

▪ “Mnamo mwaka wa 1970, nilifungwa kwa uhalifu ambao sikuwa nimefanya. Nilitumikia kifungo cha miaka 14. Nilipokuwa gerezani, nilianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Nilivutiwa sana na unyoofu na hangaiko lao. Nilipoachiliwa, niliendelea kujifunza na nikabatizwa muda mfupi baadaye. Nyakati nyingine, bado mimi huhisi nimefadhaika na kukasirika kwa sababu ya kutendewa kwa njia isiyo ya haki. Lakini ninajikumbusha kwamba karibuni, Yehova atakomesha ukosefu wote wa haki na kuteseka. Wafungwa wanaweza kurekebishwa wakifuata maagizo yanayopatikana katika Biblia. Pia wanaweza kuthamini jitihada ya kazi ngumu inayofanywa na ndugu zetu ambao hutoa wakati wao ili kuwasaidia. Bila shaka ninashukuru!”—R. S.

▪ “Nilipokuja gerezani nilikuwa nikivuta sigara, nikitumia dawa za kulevya, nikitumia lugha mbaya, na sikuwa nikiheshimu mamlaka. Pia nilikuwa mshiriki wa genge fulani. Isitoshe, nilikuwa nimetengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo. Sasa nimerudishwa, na ninafanya maendeleo mazuri. Kwa sababu ya kweli, ninahisi kwamba tayari niko huru!”—I. G.