Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Sayansi na Mungu Nilisisimka kusoma mfululizo wenye kichwa “Je, Sayansi Inaweza Kukusaidia Umwamini Mungu?” (Juni 22, 2004) Nimemtumia ndugu yangu mdogo wa kambo nakala moja ya gazeti hilo kwani yeye ni mtaalamu wa mambo ya atomu. Makala hizo zilieleza kwa usahihi kabisa kwamba msongo uliopo kati ya wanasayansi huwafanya wengi wasiamini kwamba Mungu yuko. Ninasadiki kwamba kutoamini kwamba Mungu yuko kumekuwa dini ya wanasayansi kwa sababu ya washupavu wa kidini kuielezea Biblia isivyofaa. Ninawashukuru sana kwa kuzungumzia mambo hayo.

A. B., Marekani

Mfululizo huo ulikuwa wenye kupendeza sana. Picha zenye kuvutia zilitusaidia kuelewa zile nguvu nne za asili ambazo hufanya kuwe na uhai duniani. Maswali ambayo yalielekezwa kwa wanadini yalifunua jinsi utimilifu na unyenyekevu wao ulivyo dhaifu. Pokeeni shukrani zangu nyingi kwa mfululizo wa makala hizo zote.

F. W., Marekani

Concorde Nina umri wa miaka 16, nami ningependa kuwashukuru kwa makala yenye kichwa “Safari ya Mwisho ya Ndege ya Concorde.” (Juni 22, 2004) Tangu wakati nilipokuwa mchanga, nimevutiwa sana na ndege hiyo inayosonga kasi sana. Inastaajabisha kuona vitu ambavyo mwanadamu anaweza kutengeneza kwa sababu ya akili na hekima ambayo Mungu amempa.

T.D.C., Ufaransa

Niliwahi kusafiri kwa ndege ya Concorde. Nilifurahia hasa kuona jua “likichomoza” upande wa magharibi tulipotoka London na kutua saa tatu tu baadaye mjini New York jua likiwa linaangaza wakati wa alasiri!

R. M., Marekani

Mpenzi Anayedhulumu Asanteni sana kwa makala yenye kichwa “Vijana Huuliza . . . Nifanyeje Mpenzi Wangu Aache Kunitesa?” (Juni 22, 2004) Nilikuwa katika uhusiano ambao ulinihatarisha kimwili na kihisia. Nilimwogopa mpenzi wangu, na jambo hilo lilifanya uhusiano huo wenye kudhulumu uendelee kwa muda mrefu zaidi. Nilifaulu kuvunja uhusiano huo kwa msaada wa wazazi wangu, wazee Wakristo, na Yehova Mungu. Makala hiyo itawanufaisha wale wanaohitaji msaada.

J. A., Marekani

Ninatumaini kwamba makala hiyo itamsaidia mtu asiolewe na mwanamume atakayemtesa. Uhusiano unapoanza mtu anapaswa kukataa kudhulumiwa kihisia, kimwili, na kwa maneno. Mimi nilijifunza somo hilo baada ya kuumia.

T. G., Kanada

Msimamizi Aliyebadilika Nilimfanyia kazi msimamizi aliyekuwa mpole na mwenye huruma kwa miaka mitano. Kisha kampuni hiyo ikauzwa nasi tukapata msimamizi mpya. Kila mara alinitukana. Kila siku niliaibishwa, nikatukanwa, naye alisema uwongo kunihusu. Nilishuka moyo na kufadhaika sana. Kisha nikapokea gazeti la Mei 8, 2004, lenye mfululizo wenye kichwa “Ufanyeje Ukidhulumiwa Kazini?” Niliwekelea nakala moja juu ya meza yangu mahali ambapo angeweza kuiona na kuisoma ikiwa alitaka. Naye alifanya hivyo. Tangu wakati huo tabia yake imebadilika sana. Yeye hanidhulumu tena. Hata anasema kwamba ninafanya kazi yangu vizuri zaidi. Hicho ni kitulizo kwelikweli!

K.D.A., Côte d’Ivoire

Upweke Makala zenye kichwa “Kuwa Peke Yako Bila Kuhisi Upweke” zilikuwa zenye kupendeza sana. (Juni 8, 2004) Nilifurahia hasa mapendekezo yaliyoonyeshwa katika sanduku lililo kwenye ukurasa wa 7, “Jinsi Unavyoweza Kukabiliana na Upweke.” Nimetumia mapendekezo mengi kati ya hayo na nina uhakika kwamba yatawatia moyo watu wengi.

E. M., Marekani