Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mikazo Inayowakumba Vijana wa Leo

Mikazo Inayowakumba Vijana wa Leo

Mikazo Inayowakumba Vijana wa Leo

KUBALEHE kunaweza kuwa kipindi kigumu hata ikiwa kijana yuko chini ya hali nzuri. Katika kipindi hicho, vijana hupatwa na hisia ambazo hawajawahi kuwa nazo. Kila siku wao hukabili mikazo kutoka kwa walimu na vijana wengine. Wao hukabili uvutano kutoka kwenye televisheni, filamu, muziki, na Intaneti. Hivyo, ripoti ya Umoja wa Mataifa inaeleza kwamba kubalehe ni “kipindi cha badiliko ambacho huwa na mfadhaiko na mikazo.”

Kwa kusikitisha, mara nyingi vijana hawana uzoefu wa kushughulika na mfadhaiko na mikazo katika njia inayofaa. (Methali 1:4) Bila mwongozo unaofaa, ni rahisi wajihusishe katika tabia zinazodhuru. Kwa mfano, ripoti hiyo ya Umoja wa Mataifa inasema: “Utafiti unaonyesha kwamba mara nyingi vijana huanza kutumia dawa za kulevya wanapobalehe au wanapokaribia kuwa watu wazima.” Ndivyo ilivyo kuhusu tabia nyingine mbaya kama vile jeuri na ngono za ovyoovyo.

Wazazi wanaofikiri kwamba mambo hayo hutukia tu miongoni mwa “maskini” au watu wa kabila fulani hukosea sana. Matatizo ambayo vijana wanakabili leo huwapata wote bila kujali hali za kiuchumi, za kijamii, na za kikabila. Mwandishi Scott Walter anaandika hivi: “Ikiwa unafikiri kwamba vijana wanaovunja sheria ni wavulana wachache tu wa kabila fulani dogo wenye umri wa miaka 17 wanaoishi mitaani na ambao mama zao maskini hupokea msaada kutoka kwa serikali, basi hujui ni nini kinachoendelea. Siku hizi, mtoto mwenye matatizo hayo anaweza kuwa mzungu, anaweza kuishi katika eneo la matajiri, anaweza kuwa na umri unaopungua (sana) miaka 16, na anaweza kuwa msichana.”

Lakini kwa nini vijana wengi sana wamo hatarini? Je, vijana wa zamani hawakukabili magumu na vishawishi? Ndiyo, lakini tunaishi katika kipindi kinachotajwa na Biblia kuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1-5) Kuna hali na magumu fulani ya pekee yanayowapata vijana hasa wakati huu. Acheni tuchunguze baadhi ya hali hizo.

Mabadiliko Katika Familia

Kwa mfano, fikiria hali zinazobadilika katika familia. “Zaidi ya mtoto mmoja kati ya watatu nchini Marekani hushuhudia wazazi wake wakitalikiana kabla ya kufikia umri wa miaka 18,” linaripoti jarida linaloitwa Journal of Instructional Psychology. Takwimu kama hizo zinapatikana pia katika nchi nyingine za Magharibi. Ndoa inapovunjika, vijana hulazimika kukabiliana na hisia zenye uchungu. Jarida hilo linasema kwamba “kwa ujumla, ni vigumu kwa watoto ambao wazazi wametalikiana hivi karibuni kufanya vizuri sana shuleni au kuchangamana na watoto wengine kuliko inavyokuwa kwa watoto wa familia ambazo wazazi wako pamoja, familia za mzazi mmoja zilizo imara, au wa familia zenye mzazi wa kambo . . . Isitoshe, mara nyingi talaka ya wazazi huathiri hali nzuri ya kihisia na ya kujiheshimu ya mtoto.”

Pia idadi inayoongezeka ya wanawake wanaoajiriwa imeanza kuathiri familia. Uchunguzi mmoja kuhusu vijana wanaofanya uhalifu nchini Japani ulionyesha kwamba ni vigumu zaidi kuwatunza watoto katika familia ambazo wazazi wote wameajiriwa kuliko ilivyo katika familia ambazo mzazi mmoja hushinda nyumbani.

Ni kweli kwamba familia nyingi zinahitaji mishahara ya watu wawili ili kuandaa mahitaji ya msingi. Pia mishahara ya watu wawili inaweza kuwaandalia watoto maisha ya starehe zaidi. Lakini kuna tatizo: Mamilioni ya watoto wanapotoka shuleni hawampati mtu nyumbani. Mara nyingi wazazi wanaporudi wanakuwa wamechoka na wana matatizo mengi ya kazini. Matokeo huwaje? Vijana wengi hawapati uangalifu wa kutosha kutoka kwa wazazi. Kijana mmoja alisema hivi: “Hatutumii wakati tukiwa pamoja kama familia.”

Wachunguzi wengi wanahisi hiyo si dalili nzuri ya wakati ujao kwa vijana. Dakt. Robert Shaw anasema hivi: “Naamini kwamba njia ambazo wazazi wametumia kuwalea watoto wao katika miaka thelathini iliyopita, zinawafanya watoto waepuke kuwa na uhusiano na familia zao, wasipende kuzungumza, wawe na matatizo ya kujifunza, na wasiweze kudhibitiwa. Wazazi hujikuta wakiwa wamenaswa katika jamii inayokazia kupata mali na mafanikio yanayopita kiasi na hilo huwafanya watumie wakati mwingi sana kazini na watumie pesa nyingi sana hivi kwamba hawawezi kupata wakati wa kufanya mambo ya lazima ili wawe na uhusiano wa karibu pamoja na watoto wao.”

Jambo jingine linalotisha hali ya vijana ni hili: Mara nyingi watoto ambao wazazi wao hufanya kazi wana wakati mwingi wa kufanya mambo bila uangalizi wa wazazi na hilo linaweza kutokeza matatizo.

Maoni Yanayobadilika Kuhusu Nidhamu

Maoni yanayobadilika kuhusu nidhamu kutoka kwa wazazi yanawaathiri vijana wa leo. Kama Dakt. Ron Taffel alivyosema waziwazi, wazazi wengi “huachilia madaraka yao.” Wanapofanya hivyo, vijana hukua bila sheria au miongozo yoyote ya kudhibiti tabia zao.

Katika visa fulani, inaonekana maoni ya wazazi kuhusu nidhamu huathiriwa na mambo yaliyowapata walipokuwa watoto. Wanataka kuwa marafiki wa watoto wao wala si watoa nidhamu. Mama mmoja anasema hivi: “Niliachilia mambo sana. Wazazi wangu walikuwa wakali sana nami nilitaka kumtendea mtoto wangu kwa njia tofauti. Lakini nilikosea.”

Ni mambo gani ambayo wazazi hufanya ili kuepuka kutoa nidhamu? Gazeti USA Today linaripoti hivi: “Uchunguzi wa hivi karibuni wa vijana 600 hivi wanaotibiwa athari za dawa za kulevya huko New York, Texas, Florida na California ulionyesha kwamba asilimia 20 kati yao wametumia dawa za kulevya mbali na vinywaji vinavyolewesha wakiwa na wazazi wao, na kwamba asilimia 5 hivi walionyeshwa jinsi ya kutumia dawa hizo—hasa bangi—na baba au mama zao.” Ni nini ambacho kingemchochea mzazi kufanya jambo hilo la kipumbavu? Mzazi mmoja alikiri hivi: “Nilimwambia binti yangu kwamba ni afadhali atumie dawa hizo nyumbani, mahali ambapo ningeweza kumwona.” Yaonekana wengine wanafikiri kwamba kutumia dawa za kulevya pamoja na watoto wao ni njia ya “kuimarisha” uhusiano wao.

Wanaathiriwa na Vyombo vya Habari

Pia kuna uvutano wenye nguvu wa vyombo vya habari. Kulingana na mtafiti Marita Moll, uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba kwa wastani, vijana nchini Marekani walitumia saa nne na dakika 48 kila siku wakitazama televisheni au wakitumia kompyuta.

Je, jambo hilo linaweza kuwa na madhara? Makala moja iliyochapishwa katika gazeti Science iliripoti kwamba “mashirika sita makubwa ya kitaaluma nchini Marekani,” kutia ndani Shirika la Kitiba la Marekani, yanakubaliana kwamba jeuri inayoonyeshwa katika vyombo vya habari inahusiana na “tabia ya jeuri ambayo watoto fulani wanayo.” Gazeti hilo lilisema kwamba, “licha ya wataalamu kukubaliana, inaonekana kwamba watu wa kawaida hawaelewi habari zinazotolewa katika vyombo vya habari kwamba jeuri inayoonyeshwa katika vyombo hivyo hufanya jamii iwe yenye jeuri zaidi.”

Kwa mfano, fikiria video za muziki. Mara nyingi, wazazi hushtuka kuona jinsi baadhi ya video hizo zinavyoonyesha ngono waziwazi. Je, kweli zinaweza kuathiri tabia ya vijana fulani? Kulingana na uchunguzi mmoja uliofanyiwa wanafunzi 500 wa chuo, “maneno ya muziki wenye jeuri yaliwafanya wawe na mawazo na hisia zenye jeuri zaidi.” Kulingana na uchunguzi mwingine wa hivi karibuni, “inaelekea kwamba vijana wanaotumia wakati mwingi zaidi wakitazama ngono na jeuri inayoonyeshwa katika video hizo za muziki wa rapu watafanya mambo hayo.” Uchunguzi huo uliofanyiwa zaidi ya wasichana 500 ulionyesha kwamba wale wanaotumia muda mwingi wakitazama video hizo yaelekea watampiga mwalimu, watakamatwa, au watafanya ngono na watu tofauti-tofauti.

Vijana na Kompyuta

Katika miaka ya karibuni kompyuta pia imekuwa na uvutano mkubwa katika fikira za vijana. Jarida Pediatrics linasema kwamba, “idadi ya kompyuta zinazotumiwa nyumbani imeongezeka sana katika miaka ya hivi karibuni. Nchini kote [Marekani], nyumba mbili kati ya tatu zilizo na watoto wenye umri wa kwenda shule (miaka 6 hadi 17) zilikuwa na kompyuta . . . Asilimia ya watoto waliokuwa na umri wa kati ya miaka 3 hadi 17 nchini Marekani na walioishi katika nyumba iliyokuwa na kompyuta iliongezeka kutoka asilimia 55 katika mwaka wa 1998 hadi asilimia 65 katika mwaka wa 2000.” Katika nchi nyingine pia idadi ya watu wanaotumia kompyuta imeongezeka.

Hata hivyo, kijana hahitaji kuwa na kompyuta yake ili aitumie. Hivyo, mtafiti mmoja anadai kwamba “karibu asilimia 90 ya vijana walio na umri kati ya miaka 5 hadi 17 hutumia kompyuta, na asilimia 59 kati yao hutumia Intaneti.” Hilo hufanya vijana waweze kupata habari nyingi kuliko wakati mwingine wowote na hilo ni jambo zuri ikiwa kompyuta itatumiwa vizuri, mtu mzima akiwepo. Lakini kwa kusikitisha, wazazi wengi sana wamewaruhusu vijana watumie kompyuta bila usimamizi wowote.

Ili kuonyesha hilo, mtafiti Moll anaandika katika jarida Phi Delta Kappan kwamba kulingana na uchunguzi uliofanywa katika mwaka wa 2001 kuhusu kutumia Intaneti, “asilimia 71 ya wazazi walifikiri kwamba walijua ‘kiasi kikubwa au kiasi kinachofaa’ kuhusu jinsi watoto wao wanavyotumia Intaneti. Hata hivyo, wakati watoto walipoulizwa swali hilohilo, asilimia 70 kati yao walisema kwamba wazazi wao ‘walijua kidogo sana au hata hawakujua chochote’ kuhusu jinsi walivyotumia Intaneti.” Kulingana na uchunguzi huo, “asilimia 30 ya watoto walio na umri wa miaka 9 hadi 10 walisema kwamba walitumia vituo vya Intaneti vya kibinafsi na vile vinavyopaswa kutumiwa na watu wazima peke yao. Tatizo hilo linakuwa baya zaidi kwa kuwa asilimia 58 ya watoto walio na umri wa miaka 11 hadi 12, asilimia 70 ya walio na umri wa miaka 13 hadi 14, na asilimia 72 ya wale walio na umri wa miaka 15 hadi 17 wameripoti kwamba wamewahi kutumia vituo hivyo. . . . Katika uchunguzi uliofanywa nchini Uingereza kuhusu kutumia Intaneti nyumbani, mzazi mmoja kati ya saba alikiri kwamba hakujua lolote kuhusu mambo ambayo watoto wake walikuwa wakitazama kwenye vituo vya Intaneti.”

Vijana wanapotumia Intaneti bila kusimamiwa wanaweza kutazama ponografia. Hata hivyo, kuna hatari nyingi zaidi. Taffel aliyetajwa mapema, anasema: “Watoto wetu wanafanya marafiki shuleni na kwenye Intaneti, na kwa sababu hiyo wanatumia wakati mwingi na watoto ambao mara nyingi hatuwajui.”

Ni wazi kwamba vijana wa leo wanapatwa na mikazo na matatizo ambayo vijana wa zamani hawakupatwa nayo. Basi haishangazi kwamba vijana wengi wanajiendesha kwa njia inayotia wasiwasi! Je, kuna lolote linaloweza kufanywa ili kuwasaidia vijana wa leo?

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Naamini kwamba njia ambazo wazazi wametumia kuwalea watoto wao katika miaka thelathini iliyopita, zinawafanya watoto waepuke kuwa na uhusiano na familia zao, wasipende kuzungumza, wawe na matatizo ya kujifunza, na wasiweze kudhibitiwa.”—DAKT. ROBERT SHAW

[Picha katika ukurasa wa 6, 7]

Hali katika familia imebadilika kwa kuwa wanawake wengi zaidi wameajiriwa

[Picha katika ukurasa wa 7]

Ni rahisi kwa vijana kuingia katika taabu wasiposimamiwa

[Picha katika ukurasa wa 8]

Watafiti wamehusianisha video za muziki zenye jeuri na mwenendo wenye jeuri

[Picha katika ukurasa wa 9]

Je, unajua watoto wako wanatazama nini kwenye Intaneti?