Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Msaada kwa Ajili ya Vijana wa Leo

Msaada kwa Ajili ya Vijana wa Leo

Msaada kwa Ajili ya Vijana wa Leo

VIJANA leo wanakua katika ulimwengu unaoweza kuwaogopesha. Baadhi yao huwaona wazazi wakitengana au kutalikiana bila kujua la kufanya. Wengine huwaona wanashule wenzao wakianza kutumia dawa za kulevya na kujihusisha na uhalifu. Wengi hukazwa na vijana wenzao wa jinsia zote wajihusishe na ngono. Na pindi kwa pindi karibu vijana wote wanaobalehe huhisi kwamba watu hawawaelewi, hujihisi wapweke, na hushuka moyo.

Vijana wanahitaji nini ili wakabiliane na magumu yanayowakumba? Dakt. Robert Shaw anaandika hivi: “Watoto wanahitaji kiwango thabiti cha adili, kiwango ambacho kitawasaidia wachague marafiki wanaofaa, wafanye maamuzi mazuri, na wawahurumie wengine.” Biblia ndicho kiwango kinachofaa zaidi cha adili kwa kuwa kina mawazo ya Muumba. Ni nani anayeweza kujua mengi zaidi kuhusu mambo tunayohitaji ili kukabiliana na nyakati zenye taabu za leo kuliko Yehova Mungu?

Mwongozo Halisi na Unaofaa

Kanuni za Biblia ni halisi na zinafaa. Hizo ni muhimu sana kwa wazazi na watu wengine wazima wanaotaka kuwasaidia vijana wafanikiwe wakiwa watu wazima.

Kwa mfano, Biblia inasema kihalisi kwamba “ujinga umefungwa pamoja na moyo wa mvulana,” au kama tafsiri ya Biblia Habari Njema isemavyo, “mtoto hupenda mambo ya kijinga moyoni.” (Methali 22:15) Vijana fulani waliobalehe huonekana kama wamekomaa kuliko umri wao, lakini bado wao ni vijana wasio na uzoefu. Kwa hiyo, wanaweza kupatwa na wasiwasi, tamaa, na hisia zenye kusumbua ambazo huwa za kawaida mtu anapokua. (2 Timotheo 2:22) Vijana hao wanaweza kusaidiwaje?

Biblia inatia moyo kwamba kuwe na mawasiliano ya kawaida kati ya wazazi na watoto. Hiyo huwahimiza wazazi hivi: ‘Sema viwango vya Mungu unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.’ (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Mawasiliano hayo hunufaisha katika njia mbili. Kwanza, yanamfundisha kijana njia za Mungu. (Isaya 48:17, 18) Pili, yanawafanya wazazi na watoto waweze kuwasiliana. Hilo ni muhimu hasa wakati vijana wanapitia kipindi cha kubalehe ambapo wanaweza kuwa wenye haya na wapweke.

Bila shaka, vijana wengi wanaobalehe hupitia vipindi vya kuhisi upweke. Hata hivyo, wengine huhisi upweke kwa muda mrefu sana. Kitabu kimoja cha marejeo kuhusu kubalehe kinasema hivi: “Vijana hao husema ni vigumu kwao kuwa na marafiki shuleni, kwamba hawana mtu wa kuzungumza naye, kwamba wanahisi upweke, kwamba ni vigumu kupendwa na watoto wengine, na kwamba wanahisi kuwa hawana mtu wa kumwomba msaada.” *

Wazazi na watu wazima wanaweza kupendezwa na vijana na kuwasaidia kukabiliana na matatizo yao. Jinsi gani? Mhariri mkuu wa gazeti fulani la vijana anaandika hivi: “Njia pekee ya kujua mambo ambayo vijana wanafikiria ni kuwauliza.” Ni wazi kwamba wakati na subira vinahitajiwa ili kuwasaidia vijana wafunue yanayowahangaisha. Lakini jitihada hizo hunufaisha.—Methali 20:5.

Vijana Wanahitaji Mipaka Inayofaa

Zaidi ya kuwasiliana, vijana wanahitaji, na wanataka, kuwekewa mipaka inayofaa. Biblia inasema kwamba “mvulana aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.” (Methali 29:15) Wataalamu wanaamini kwamba vijana huvunja sheria kwa sababu ya kutowekewa mipaka iliyo wazi. Shaw aliyenukuliwa mapema anasema: “Ikiwa mtoto anaachiliwa daima, naye hakatazwi jambo lolote au kuwekewa vizuizi, hatajifunza kwamba hapaswi kamwe kuingilia faragha, hisia, mahitaji, na mapendezi ya watu wengine. Bila kuwa na hisia ya huruma iliyositawishwa vizuri, mtoto hataweza kuonyesha upendo.”

Dakt. Stanton Samenow ambaye amefanya kazi kwa muda mrefu na vijana wanaotaabika anasema jambo kama hilo. Anaandika hivi: “Wazazi fulani wanaamini kwamba watoto hawapaswi kuwekewa mipaka. Bila kufikiri, wao huamini kwamba kuwapa madaraka au kuwawekea matakwa kutawalemea watoto wao na kuwazuia wasifurahie utoto wao. Lakini kukosa kuwawekea mipaka kunaweza kuwadhuru. Wazazi hao hawatambui kwamba ni vigumu kwa mvulana au msichana ambaye hupata nidhamu kidogo sana kujitia nidhamu.”

Je, hilo lamaanisha kwamba wazazi wanapaswa kuwa wakali? Sivyo. Kuweka mipaka ni sehemu moja tu ya kuwalea watoto kwa njia inayofaa. Ikiwa wataweka sheria nyingi kupita kiasi na zilizo ngumu, hilo linaweza kutokeza hali mbaya katika familia. Biblia inasema: “Enyi akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.”—Wakolosai 3:21; Waefeso 6:4.

Kwa hiyo, pindi kwa pindi wazazi wanahitaji kuchunguza tena mbinu zao za kufundisha na kutia nidhamu, hasa watoto wao wanapokua wakubwa na kuanza kuonyesha dalili za ukomavu. Labda sheria au vizuizi fulani vinaweza kupunguzwa au kurekebishwa ikitegemea uwezo wa kijana wa kutenda kwa njia inayofaa.—Wafilipi 4:5.

Kusitawisha Uhusiano

Kama ilivyoonyeshwa katika makala iliyotangulia, Biblia ilitabiri kwamba kabla Mungu hajaingilia kati na kuondoa mambo mabaya duniani, ulimwengu ungepatwa na “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Kuna uthibitisho kwamba tunaishi katika kipindi hicho, yaani, “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo usiomwogopa Mungu. Kama tu watu wazima, vijana hufanya jitihada kubwa ya kuishi katika ulimwengu ulio na watu “wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio na upendo wa asili, . . . wasiojizuia.”—2 Timotheo 3:1-5. *

Wazazi wanaohisi kwamba hawana uhusiano mzuri pamoja na mwana au binti yao anayebalehe wanaweza kuchukua hatua ya kusitawisha uhusiano, kwa kuzungumza nao mara kwa mara. Ni jambo la kusifika kwamba wazazi wengi wanajitahidi sana kuwasaidia watoto wao na kuwa na uhusiano wa karibu nao.

Biblia ni kifaa muhimu sana katika kufanya hivyo. Imewasaidia wazazi wengi watimize daraka lao na kuwasaidia vijana waepuke mitego inayoweza kuwadhuru. (Kumbukumbu la Torati 6:6-9; Zaburi 119:9) Kwa kuwa Biblia ni kitabu kutoka kwa Muumba, Yehova Mungu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba hiyo huandaa msaada bora zaidi kwa vijana wa leo. *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Kitabu hicho kinasema kwamba tofauti na kijana ambaye hujihisi mpweke mara kwa mara, yule anayejihisi mpweke kwa muda mrefu sana huhisi ametengwa mara nyingi kwa kipindi kirefu. Yeye “huamini kwamba kutokuwa na marafiki ni jambo lisiloweza kubadilika, lisiloweza kuzuiwa, na hutokea kwa sababu ya kasoro zake” na kwamba hali hiyo “haiwezi au haitabadilika.”

^ fu. 16 Ona sura ya 11 katika kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 18 Mashahidi wa Yehova wameona kwamba kitabu kinachotegemea Biblia, Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi kinasaidia sana. Kila mojawapo ya sura zake 39 hujibu swali lenye kuchochea fikira. Baadhi ya vichwa vyake ni: “Naweza Kufanyaje Marafiki wa Kweli?” “Naweza Kukabilianaje na Msongo wa Marika?” “Naweza Kufanyaje Upweke Wangu Uniondoke?” “Je! Niko Tayari Kufanya Urafiki na Mtu wa Jinsia Tofauti?” “Kwa Nini Ukatae Madawa ya Kulevya?” “Vipi Juu ya Ngono Kabla ya Ndoa?”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mweleze mtu mzima anayejali mambo yanayokuhangaisha