Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ahadi za “Mungu wa Pekee wa Kweli”

Ahadi za “Mungu wa Pekee wa Kweli”

Ahadi za “Mungu wa Pekee wa Kweli”

YEHOVA MUNGU aliwaweka wanadamu wa kwanza katika paradiso duniani—bustani ya Edeni. Aliwaagiza wazae watoto na ‘kuitiisha dunia,’ mgawo ambao ungetia ndani kupanua makao yao yaliyokuwa Paradiso huku familia yao ikizidi kuwa kubwa. (Mwanzo 1:26-28; 2:15) Je, kusudi la Mungu la wanadamu wote kufurahia maisha katika paradiso duniani litatimia?

Bila shaka, litatimia! Kulingana na unabii wa Biblia, “[Yehova] kwa kweli atameza kifo milele” na “hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” Hilo litakapotukia, “hakika mtu atasema: ‘Tazama! Huyu ndiye Mungu wetu. Tumemtumaini yeye, naye atatuokoa. Huyu ndiye Yehova. Tumemtumaini yeye. Na tuwe na shangwe na kushangilia katika wokovu wake.’”—Isaya 25:8, 9.

Kitabu cha mwisho cha Biblia kinaeleza jinsi hali zitakavyokuwa duniani baada ya ulimwengu, au mfumo wa mambo uliopo unaotawaliwa na Shetani, kuondolewa. Kuhusu “dunia mpya” ambayo ni jamii ya wanadamu wanaompenda Mungu, Biblia inasema: “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu, naye atakaa pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Na Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:1-4.

Hizo ni ahadi nzuri kama nini! Je, tunaweza kuziamini? Hebu fikiria jinsi kifo cha kidhabihu cha Yesu na miujiza aliyofanya inavyotuhakikishia kwamba Mungu atazitimiza ahadi zake zote.—2 Wakorintho 1:20.

Yesu Atoa Uhai Wake Kuwa Fidia

Shetani alipomshawishi Adamu amwasi Mungu na kufanya dhambi, wazao wote wa Adamu walirithi dhambi yake. Biblia inasema: “Kama vile kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” Biblia yaendelea kusema hivi: “Kupitia kutii kwa mtu mmoja [mwanadamu mkamilifu Yesu] wengi watafanywa kuwa waadilifu.” (Waroma 5:12, 19) Kama makala ya kwanza katika mfululizo huu ilivyosema, Yesu ndiye “Adamu wa mwisho,” yule ‘anayetoka mbinguni,’ ambaye alitoa uhai wake “kuwa fidia badala ya wengi.”—1 Wakorintho 15:45, 47; Mathayo 20:28.

Kwa hiyo, wote wanaomwamini Yesu wanaweza “kuachiliwa huru [kutoka katika dhambi] kwa njia ya fidia” na wanaweza kupata uzima wa milele. (Waefeso 1:7; Yohana 3:36) Kwa kweli tunaweza kufurahi kwamba Yehova Mungu aliupenda ulimwengu wa wanadamu sana hivi kwamba alimtoa Mwana wake awe Mwokozi wetu! (Luka 2:10-12; Yohana 3:16) Kuchunguza jinsi Yesu alivyowasaidia wanadamu walioteseka katika karne ya kwanza hutusaidia kuelewa jinsi wakati ujao utakavyokuwa. Na mambo ambayo Yesu alifanya kwa kweli yalikuwa mambo ya ajabu!

Mwonjo wa Ulimwengu Mpya

Yesu alikuwa na uwezo wa kuwaponya wagonjwa wote walioletwa kwake. Aliwaponya wagonjwa wote, haidhuru magonjwa waliyokuwa nayo. Zaidi ya hayo, alilisha maelfu ya watu kimuujiza kwa samaki wachache na mikate, na alifanya hivyo zaidi ya mara moja.—Mathayo 14:14-22; 15:30-38.

Yesu alipomponya mtu aliyezaliwa akiwa kipofu, jirani na rafiki zake walikiri muujiza huo, lakini viongozi wa kidini Wayahudi waliutilia shaka. Basi, mtu aliyeponywa akawaambia hivi: “Kutoka zamani za kale haijasikiwa kamwe kwamba mtu yeyote alifungua macho ya mtu aliyezaliwa akiwa kipofu. Kama mtu huyu hangekuwa ametoka kwa Mungu, hangeweza kufanya lolote.”—Yohana 9:32, 33.

Wakati wa huduma ya Yesu, binamu yake, Yohana Mbatizaji, aliyekuwa amefungwa gerezani, aliwatuma wajumbe ili wakaulizie habari za Yesu. Biblia inasema: “Saa hiyo akaponya wengi magonjwa na maradhi yenye kuhuzunisha na roho waovu, na kuwapa vipofu wengi uwezo wa kuona.” Kisha Yesu akawaambia wajumbe hao: “Nendeni, mkamwambie Yohana yale mliyoona na kusikia: vipofu wanaona, vilema wanatembea, wenye ukoma wanatakaswa na viziwi wanasikia, na wafu wanafufuliwa.”—Luka 7:18-22.

Hebu fikiri: Ikiwa jambo zuri lilitukia wakati uliopita, je, hilo halikuhakikishii kwamba litatukia tena? Kupitia miujiza yake, Yesu alionyesha kwa kiwango kidogo mambo atakayofanya kwa kiwango kikubwa zaidi atakapotawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Miujiza yake inathibitisha kwamba alitumwa na Mungu na kwamba kwa kweli alikuwa Mwana wa Mungu.

Ufalme wa Mungu utakapotawala, kutakuwa na utimizo halisi wa unabii mbalimbali wa mambo mazuri. Kama ilivyotabiriwa, macho ya vipofu yatafunguliwa, masikio ya viziwi yatazibuliwa, magonjwa yataondolewa, vilema wataruka-ruka kama paa, wala hakuna atakayekuwa mgonjwa. Pia kutakuwa na amani na usalama duniani pote. Hata wanyama walio hatari leo wataishi kwa amani pamoja na wanadamu. —Isaya 9:6, 7; 11:6-9; 33:24; 35:5, 6; 65:17-25.

Je, ungependa kuishi milele chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu ulimwengu utakapokuwa hivyo? Yesu alionyesha jambo unalohitaji kufanya aliposali hivi kwa baba yake: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Usiruhusu chochote kikuzuie kuendelea kupata ujuzi huo unaoongoza kwenye uzima.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mungu anaahidi dunia itakuwa hivi