Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Je, Nitafute Mchumba Kwenye Mtandao wa Intaneti?”

“Je, Nitafute Mchumba Kwenye Mtandao wa Intaneti?”

Vijana Huuliza . . .

“Je, Nitafute Mchumba Kwenye Mtandao wa Intaneti?”

“Tulitumiana barua-pepe kila siku. Tulifanya mipango kuhusu mahali pa kuishi na kufanya kazi. Nilipaswa kutafuta pete za uchumba. Tulikuwa tumejuana kwa muda usiozidi mwezi mmoja na hatukuwa tumekutana kamwe uso kwa uso.”—Monika, Austria. *

TUSEME kwamba ungependa sana kukutana na mtu—mtu ambaye ungependa kumjua vizuri zaidi, mtu ambaye huenda hata ungependa kufunga ndoa naye. Lakini, kufikia sasa, hujafanikiwa bado. Kila mara, marafiki na washiriki wengine wa familia wanaokutakia mema wanapojaribu kukukutanisha na mtu fulani, mambo huenda mrama nawe huvunjika moyo hata zaidi. Huenda sasa unafikiria kutumia teknolojia kupata msaada.

Katika enzi hii ya kompyuta, huenda ikaonekana kuwa rahisi sana kumpata mwenzi mnayepatana. Wengine husema kwamba unachohitaji tu ni kutumia kituo fulani cha mazungumzo au matangazo kwenye mtandao wa Intaneti ambacho kimetayarishwa hasa kwa ajili ya waseja. Gazeti moja (The New York Times) laripoti kwamba katika mwezi mmoja tu huko Marekani peke yake, watu milioni 45 walitumia vituo vya uchumba kwenye mtandao wa Intaneti. Kituo kimoja cha uchumba kinadai kwamba watu zaidi ya milioni tisa katika nchi 240 hutumia huduma zake.

Kwa Nini Uchumba Kwenye Mtandao wa Intaneti Unavutia?

Je, wewe ni mtu mwenye haya na huona vigumu kuzungumza na watu? Je, unaogopa kukataliwa? Au, unahisi tu kwamba kwenu kuna upungufu wa wachumba? Basi huenda ukavutiwa na uchumba kwenye mtandao wa Intaneti. Kwanza, vituo vya uchumba kwenye mtandao wa Intaneti husema kwamba wewe ndiwe utakayefanya maamuzi. Unaweza kujichagulia umri, nchi, utu, picha, na majina bandia. Kwa kuwa wewe mwenyewe ndiwe unayefanya uchaguzi, huenda ukaona kwamba ni rahisi zaidi kuchumbia kwenye mtandao wa Intaneti kuliko kupata mfadhaiko wa kukutana na watu uso kwa uso.

Ukweli wa mambo ni nini? Je, uchumba kwenye mtandao wa Intaneti waweza kuleta furaha ya kudumu? Fikiria hili: Katika kipindi cha miaka sita, watu milioni 11 walijiandikisha katika kituo kimoja kinachowaunganisha wachumba. Hata hivyo, ni ndoa 1,475 tu zilizofungwa. Katika kituo kingine kilichokuwa na watu zaidi ya milioni moja, ni ndoa 75 tu zilizofungwa! Tatizo ni nini?

Je, Hiyo Ndiyo Njia Bora ya Kufahamiana?

Makala katika gazeti moja ilisema: “Kwenye mtandao wa Intaneti, kila mtu huonekana mwenye kupendeza, mnyoofu, na mwenye mafanikio maishani.” Lakini je, habari ambazo watu hutoa ni za kutegemeka kadiri gani? Makala nyingine ya habari ilisema hivi: “Inajulikana kwamba kila mtu hudanganya kwa kiasi fulani.” Mhariri wa gazeti linalopendwa sana na vijana alichunguza dai hilo. Alijiunga na vituo vitatu vya uchumba vinavyopendwa na watu wengi, na muda si muda watu kadhaa wakaanza kuwasiliana naye. Akaanza uchumba na wanaume kadhaa. Ikawaje? Ilikuwa kazi bure! Wanaume hao walisema uwongo wa wazi kujihusu. Anaonya hivi: “Kutokana na mambo niliyojionea, watu hudanganya.”

Huenda wakaona si kitu kudanganya kuhusu kimo au uzito wao. Huenda wengine wakadai kwamba ‘sura si muhimu sana.’ Ni kweli Biblia yenyewe inasema kwamba “uvutio unaweza kudanganya, nayo sura yenye kupendeza inaweza kuwa ubatili.” (Methali 31:30) Lakini je, kusema uwongo kuhusu mambo yanayoonekana kuwa madogo ni njia nzuri ya kuanzisha uhusiano? (Luka 16:10) Unawezaje kuamini mambo mengine mazito ambayo mtu huyo anaweza kusema kama vile miradi yake? Biblia inasema: “Semeni ukweli kila mtu na mwenzake.” (Zekaria 8:16) Ndiyo, unyoofu ndio msingi wa uhusiano unaoweza kusitawi.

Hata hivyo, mara nyingi kuchumbia kwenye mtandao wa Intaneti huhusisha matumaini yasiyo halisi. Ripoti katika gazeti moja (Newsweek) inasema hivi: “Wanaofanya uchumba kwenye mtandao wa Intaneti wanaweza kuandika barua-pepe zao kwa uangalifu sana na kujifanya wenye kuvutia zaidi. . . . Matokeo ni kwamba majibu watakayopata pia yatakuwa yenye kupendeza: wao nao watajifanya kuwa wazuri na wanapendezwa nawe, nawe utajifanya mzuri machoni pao na mwenye kupendezwa nao.” Profesa mmoja wa Chuo cha Ufundi cha Rensselaer huko New York anayechunguza mahusiano kwenye mtandao wa Intaneti anasema kwamba mahusiano hayo yanaweza kuwa yenye nguvu sana. Hata hivyo, mara nyingi imeonekana kwamba watu hao hawawezi kuwa na ndoa yenye furaha. Mtu mmoja aliandika kuhusu uchumba wake kwenye mtandao wa Intaneti: “Ni mtego. Unajijazia katika akili yako mambo ambayo unataka.”

Kukutana Uso kwa Uso

Hata hivyo, huenda wengine wakahisi kwamba kuna faida za kuwasiliana na mtu bila kuonana naye. Huenda wakafikiri kwamba kuchumbiana kwenye mtandao wa Intaneti huwasaidia kukazia utu wa mtu bila kukengeushwa na sura yake. Ni kweli kwamba Biblia inatutia moyo tuzingatie utu wa mtu. (1 Petro 3:4) Hata hivyo, tatizo ni kwamba unapokuwa na uhusiano na mtu kwenye mtandao wa Intaneti huwezi kuona ishara za mwili, tabasamu, au sura yake. Huwezi kuona jinsi anavyowatendea wengine au anavyojiendesha chini ya mkazo. Na mambo hayo ni muhimu ili kujua kama unaweza kumtumaini na kumpenda mtu huyo. Soma ufafanuzi wa Biblia kuhusu upendo kwenye 1 Wakorintho 13:4, 5. Ona kwamba upendo unaonyeshwa kwa mwenendo, wala si maneno. Kwa hiyo, chukua wakati kumchunguza mtu na kuona ikiwa matendo yake yanapatana na anayosema.

Mara nyingi, watu hao huanza kuambiana hisia na maoni yao mapema kabla ya kupata habari muhimu. Wenzi fulani hutoa ahadi haraka-haraka bila kufikiri, hata ingawa hawajuani vizuri. Makala yenye kichwa “Kwa Kweli Upendo Ni Kipofu Kwenye Mtandao wa Intaneti” inasimulia kuhusu watu wawili wanaoishi umbali wa kilometa 12,875 ambao walikutana kwenye mtandao wa Intaneti. Walikutana uso kwa uso baada ya majuma matatu. Mwanamume huyo anasema, “Mwanamke huyo alikuwa amejipaka wanja kupita kiasi. Sipendi wanawake wanaojipaka wanja.” Uhusiano huo uliisha mara moja. Mwanamume mwingine aliyekutana na mchumba wake uso kwa uso alisikitika sana hivi kwamba alifutilia mbali tiketi ya ndege ya kurudi nyumbani aliyokuwa amemkatia mwanamke huyo!

Mwanamke mmoja kijana anayeitwa Edda anakumbuka uchumba wake kwenye mtandao wa Intaneti. Anasema: “Uhusiano huo ulikuwa mzuri isivyoaminika. Tulikuwa tukipanga kufunga ndoa.” Lakini walipokutana uso kwa uso, uhusiano wao uligonga mwamba. “Hakuwa na sifa nilizotazamia, alikuwa mchambuzi na mwenye kulalamika. Uhusiano wetu haungefaulu.” Baada ya juma moja, uhusiano huo ulivunjika na Edda akavunjika moyo kabisa.

Katika uchumba wa mtandao wa Intaneti ambamo mambo mengi huwaziwa tu, hisia zinaweza kusitawi haraka kabla ya wakati unaofaa. Kwa hiyo unaweza kuumizwa kihisia uhusiano huo ukivunjika kama ilivyo kawaida. Methali 28:26 inaonya hivi: “Anayetegemea moyo wake mwenyewe ni mjinga.” Ndiyo, si jambo la hekima kufanya maamuzi mazito kwa kutegemea hisia na mambo ya kuwazia tu. Methali hiyo yaendelea hivi: “Lakini yeye anayetembea katika hekima ndiye atakayeponyoka.”

Hatari za Kufanya Maamuzi Haraka

Bila shaka si jambo la hekima kuingia haraka-haraka katika uhusiano bila kufahamiana vizuri. Mwandishi Mwingereza Shakespeare alisema hivi: “Mara nyingi ndoa inayofungwa haraka-haraka haifaulu.” Biblia inatoa shauri la moja kwa moja: “Kila mtu anayetenda haraka-haraka bila shaka huuelekea uhitaji.”—Methali 21:5.

Inasikitisha kwamba imekuwa hivyo kwa wengi ambao wamejihusisha na uchumba kwenye mtandao wa Intaneti. Baada ya kuwasiliana na mtu fulani kwa mwezi mmoja, Monika, aliyenukuliwa mwanzoni mwa makala hii, alifikiri kwamba alikuwa amempata mchumba aliyekuwa akimtafuta kwa muda mrefu. Licha ya kufanya mipango ya ndoa—hata kutafuta pete za uchumba—uchumba wake wa haraka ulimletea “huzuni kubwa.”

Unaweza kuepuka maumivu ya moyoni kwa kutii shauri hili la Biblia: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.” (Methali 22:3) Hata hivyo, uchumba kwenye mtandao wa Intaneti una hatari nyingine mbali na kumfanya mtu avunjike moyo na kuumia kihisia. Makala ya wakati ujao itazungumzia hatari hizo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina fulani yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Kwenye mtandao wa Intaneti, mara nyingi watu hutilia chumvi au husema uwongo kujihusu

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mara nyingi watu wanaowasiliana kwa barua-pepe za mapenzi hutamauka wanapokutana uso kwa uso