Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukabili Ugonjwa kwa Ucheshi

Kukabili Ugonjwa kwa Ucheshi

Kukabili Ugonjwa kwa Ucheshi

NA MWANDISHI WA AMKENI! NCHINI HISPANIA

CONCHI ni mwanamke mchangamfu wa makamo ambaye amekabiliana na ugonjwa wa kansa kwa miaka saba. Tangu alipogunduliwa kuwa na kansa ya matiti, amefanyiwa upasuaji mara saba ili kudhibiti uvimbe hatari. Anakabilianaje na ugonjwa huo?

Anasema hivi: “Madaktari wanaponijulisha habari mbaya, mimi hulia sana ili kuondoa huzuni moyoni. Kisha mimi hujitahidi kuendelea na maisha yangu kama kawaida na kufanya mambo ninayopenda—kama vile kujifunza Kichina, kuhudhuria makusanyiko ya Kikristo, na kwenda likizo pamoja na familia na rafiki zangu. Sikuzote mimi hukumbuka maneno haya ya Yesu: ‘Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?’”—Mathayo 6:27.

Kisha anaongezea: “Na daima mimi hujitahidi kuwa mcheshi. Ninataniana na madaktari, natazama sinema zinazonichekesha na zaidi ya yote, ninajitahidi kuwasiliana kwa ukawaida na marafiki na watu wa ukoo. Kuwa na marafiki ambao unaweza kucheka nao ni kitulizo kizuri. Siku moja, kabla ya kufanyiwa upasuaji marafiki fulani na watu wa ukoo walinisimulia kisa chenye kuchekesha kilichokuwa kimetukia usiku uliotangulia. Nilicheka sana hivi kwamba nilipoingizwa kwenye chumba cha upasuaji nilikuwa nimetulia kabisa.”

Mbali na Conchi, kuna wengine ambao wamegundua kwamba ucheshi na mtazamo unaofaa unaweza kuwasaidia kukabiliana na magonjwa. Madaktari wa leo wameanza kugundua umuhimu wa ucheshi katika kupambana na uchungu na magonjwa.

Ucheshi Unafaidi Mwili na Akili

Hilo si jambo jipya. Miaka 3,000 iliyopita, Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Moyo wenye shangwe ni dawa nzuri.” (Methali 17:22) Lope de Vega, mtungaji wa vitabu Mhispania aliyeishi karne ya 17, pia aliandika hivi: “Tukiwa wacheshi sana, nafikiri tutakuwa na afya nzuri zaidi.” Lakini katika ulimwengu wa leo wenye mambo mengi yenye kufadhaisha, inaonekana kwamba watu huepuka ucheshi. Inaonekana kwamba tunaishi katika enzi yenye ufanisi mwingi wa kiteknolojia, lakini ni enzi ambayo ucheshi unapungua. Kitabu kimoja kinachozungumzia sanaa ya ucheshi (El arte de la risa) kinasema kwamba katika jamii ya leo inaonekana kwamba “Kompyuta zimechukua mahali pa ubinadamu.” Nyakati nyingine, inaonekana kwamba kompyuta zinachukua mahali pa lugha ya ucheshi, ishara na tabasamu.

Ucheshi huwasaidia wagonjwa kuwa na mtazamo, hisia, na mazoea yanayofaa. Makala ya hivi karibuni iliyoandikwa na Dakt. Jaime Sanz-Ortiz, mtaalamu wa matibabu ya kansa na ya kutuliza maumivu, inasema kwamba ucheshi “hufanya iwe rahisi kuwasiliana, huboresha kinga ya mwili dhidi ya magonjwa, huondoa maumivu, hupunguza mahangaiko, hutuliza mikazo ya kihisia na ya misuli, na humpa mtu tumaini na kuboresha uwezo wake wa kufikiri.”

Thamani ya Ucheshi

Kwa nini ucheshi huwa na matokeo katika kuponya magonjwa? Kwa sababu ni sifa inayotusaidia kushughulikia hali mbalimbali tukiwa na mtazamo unaofaa, hata katika hali zisizofaa. Sanz-Ortiz asema hivi: “Tunapokuwa wacheshi katika maisha yetu ya kila siku, tunadumisha nguvu zetu, tunaondoa uchovu, na kuepuka kujisikitikia.”

Kwa kawaida, mambo yanayowafanya watu wacheke au kutabasamu hutegemea kila mtu au utamaduni. Sanz-Ortiz aeleza: “Kwa kuwa kila mtu hupendezwa na mambo tofauti, ucheshi pia hutegemea akili ya mtazamaji.” Lakini haidhuru malezi au elimu yetu, mara nyingi ucheshi ni njia nzuri sana ya kuwasiliana na ya kuondoa mahangaiko, mfadhaiko, au wasiwasi. Basi ikiwa ucheshi unaweza kutusaidia sana, tunawezaje kuusitawisha?

Hatua ya kwanza tunayoweza kuchukua ni kuacha kukazia tu matatizo yetu au ugonjwa wetu na kuanza kujitahidi kufurahia mambo mazuri maishani mwetu. Isitoshe, tunapaswa kujitahidi kuwa na usawaziko, na kuepuka maoni yanayofanya hali yetu ionekane kuwa mbaya zaidi. Tunaweza pia kusitawisha ucheshi kwa kuangalia mambo kwa njia tofauti. Si lazima tucheke au kutabasamu nyakati zote, hata hivyo, tukiona jambo lenye kuchekesha katika hali fulani, tutaweza kukabiliana na hali hiyo. Sanz-Ortiz anakazia hivi: “Ucheshi hutusaidia kusahau mahangaiko yetu na kuwa na maoni tofauti kuelekea tatizo . . . , na kuweza kulitatua kwa njia mbalimbali.”

Bila shaka, ucheshi hautatui kila tatizo tunalokabiliana nalo maishani, hata hivyo, mara nyingi hutusaidia kukabiliana na matatizo kwa njia inayofaa na yenye usawaziko. Conchi anasema kwamba “ugonjwa si jambo la kuchekesha, lakini unapaswa kujitahidi kudumisha ucheshi wako. Mimi huona maisha yangu kuwa kama shamba la mboga lenye mimea mbalimbali, na mmoja kati ya mimea hiyo ni ugonjwa wangu. Hata hivyo, mimi hujitahidi kuuzuia usienee na kufunika mimea mingine. Bila shaka, siwezi kusema kwamba nimeushinda ugonjwa wa kansa, lakini bado ninafurahia maisha, na hilo ni jambo muhimu sana.”

[Picha katika ukurasa wa 27]

Conchi atiwa moyo na mume wake, Felix, pamoja na dada yake mdogo, Pili