Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kubalehe Asanteni kwa mfululizo wa makala zenye kichwa “Kukabili Magumu ya Kubalehe.” (Julai 8, 2004) Hivi karibuni nilifikia kipindi cha kubalehe na nimepata matatizo fulani yanayosumbua dhamiri yangu. Nimepata katika makala hizo mashauri niliyohitaji ambayo yatanisaidia kumkumbuka Muumba wangu Mtukufu. Natumaini kwamba nitapita kwa mafanikio kipindi cha kubalehe na kuepuka maumivu yanayotokana na kutumbukia katika mitego ya ulimwengu huu.

R. R., Albania

Nilipokuwa mtoto, nilikuwa na marafiki wengi wa rika langu. Lakini tulipozidi kukua, tukaacha kuzungumziana. Baada ya mikutano ya Kikristo, niliketi garini na kujitenga na wengine. Nilitulia niliposoma kwamba ni kawaida kwa wabalehe kupata hisia mbalimbali na kwamba mojawapo ya njia bora za kushinda upweke ni kupendezwa na wengine, kutia ndani watu wenye umri tofauti. Siku hiyo nilizungumza na wengine mkutanoni bila kujali umri wao, na nilifurahi sana kufanya hivyo.

M. K., Japani

Nina umri wa miaka 15, na nilihitaji sana habari hiyo. Vijana walionukuliwa walinisaidia kuelewa kwamba kuna wengi wanaokabiliana na hisia zenye kuumiza na kwamba hisia hizo zinaweza kushindwa. Makala hiyo iliniimarisha na kunitia moyo!

L. R., Ukrainia

Asanteni kwa mfululizo huo. Inatia moyo kujua kwamba inawezekana kukabiliana na kipindi hicho kigumu. Natumaini kwamba makala hizo zitawasaidia vijana wengine wakabiliane na kipindi hicho kwa njia inayofaa.

R. V., Italia

Nimekuwa nikitamani sana mfululizo wa makala hizo. Hisia zangu hubadilika-badilika, na nyakati nyingine mimi huhisi wasiwasi na upweke. Sikuzote nilihisi hatia kwa sababu ya kuwa na hisia hizo. Lakini makala ya mwisho katika mfululizo huo ilisema hivi: “Yehova Mungu anataka ufurahi—ufurahi sana. Hiyo si furaha bandia inayofunika taabu ya moyoni.” Niliposoma maneno hayo, machozi yalinitoka. Makala hiyo pia ilisema kwamba hisia hizo zenye kusumbua si za kudumu. Jambo hilo lilinifariji sana. Nilipata nguvu mpya. Asanteni sana!

H. T., Japani

Nilipoona gazeti hilo kwenye Jumba la Ufalme, nililipitia mara moja. Nilipokuwa nikilisoma nyumbani, sikutaka kuliweka chini. Hata hivyo, nilihuzunika kufika mwisho wa makala hiyo, kwa sababu sikutaka iishe! Endeleeni kuandika makala kama hizo!

K. C., Marekani

Kibodi Nina umri wa miaka 12. Asanteni kwa makala yenye kichwa “Muziki—Unaochezwa kwa Vidole.” (Julai 8, 2004) Nilinunua kitabu kinachozungumzia ala za muziki, na kina maelezo kuhusu ala za muziki zenye kibodi. Hakifafanui kibodi kwa njia nzuri kama Amkeni! Nimekuwa nikitafuta makala kama hiyo kwa muda mrefu! Kwa kweli, uwezo wa kupiga ala za muziki ni zawadi bora kutoka kwa Muumba!

D. G., Ujerumani

Kudhulumiwa Hivi karibuni, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alinipa gazeti lenye mfululizo wenye kichwa “Ufanyeje Ukidhulumiwa Kazini?” (Mei 8, 2004) Rafiki yangu mmoja aliacha kazi kwa sababu ya kudhulumiwa kazini. Mtu anayeacha kazi kwa njia hiyo nchini Ujerumani hupoteza ridhaa ya miezi mitatu. Nilijitahidi nilivyoweza kumsaidia kijana huyo. Lakini kijana huyo alipokea malipo yake siku tatu baada ya kuambatanisha gazeti lenu na barua niliyotuma kwa idara ya kuwaajiri wafanyakazi.

R. S., Ujerumani