Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mungu wa Pekee wa Kweli” Ni Nani?

“Mungu wa Pekee wa Kweli” Ni Nani?

“Mungu wa Pekee wa Kweli” Ni Nani?

YESU alisali mara nyingi kwa Mungu, aliyemwita Baba yake, na pia aliwafundisha wengine kufanya hivyo. (Mathayo 6:9-11; Luka 11:1, 2) Katika sala aliyotoa pamoja na mitume wake muda mfupi tu kabla ya kifo chake, Yesu aliomba hivi: “Baba, saa imefika; mtukuze mwana wako, ili mwana wako apate kukutukuza wewe. Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:1, 3.

Ona kwamba Yesu anasali kwa Yule anayemwita “Mungu wa pekee wa kweli.” Kisha anaonyesha cheo cha juu cha Mungu anapoendelea kusali hivi: “Kwa hiyo sasa wewe, Baba, nitukuze kando yako kwa utukufu niliokuwa nao kando yako kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:5) Kwa kuwa Yesu alisali kwa Mungu na kuomba kuwa kando ya Mungu, Yesu angewezaje wakati uleule kuwa “Mungu wa pekee wa kweli”? Na tuchunguze jambo hilo.

Cheo cha Yesu Huko Mbinguni

Yesu aliuawa muda mfupi baada ya kutoa sala hiyo. Hata hivyo, hakuwa mfu kwa muda mrefu. Alikaa kaburini kuanzia Ijumaa alasiri hadi Jumapili asubuhi. (Mathayo 27:57–28:6) Mtume Petro anasema: “Yesu huyo Mungu alimfufua, uhakika ambao sisi sote ni mashahidi.” (Matendo 2:31, 32) Je, Yesu angeweza kujifufua? Hapana, Biblia inasema kwamba wafu “hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) “Mungu wa pekee wa kweli,” Baba wa mbinguni wa Yesu, alimfufua Mwanawe.—Matendo 2:32; 10:40.

Muda mfupi baadaye, Stefano, mwanafunzi wa Yesu aliuawa na wanyanyasaji wa kidini. Kabla hajapigwa mawe, Stefano alipata maono. Alisema: “Tazameni! Ninaziona mbingu zimefunguka na Mwana wa binadamu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.” (Matendo 7:56) Stefano alimwona Yesu, yule “Mwana wa binadamu,” akimtumikia Mungu, akiwa “kwenye mkono wa kuume wa Mungu” au ‘kando ya Mungu’ kama alivyokuwa kabla ya kuja duniani.—Yohana 17:5.

Baadaye, baada ya Stefano kuuawa, Yesu alimtokea kimuujiza Sauli, aliyejulikana sana kwa jina lake la Kiroma, Paulo. (Matendo 9:3-6) Paulo alipokuwa huko Athene, Ugiriki, alizungumza kuhusu “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo.” Alisema kwamba Mungu huyo, yule “Mungu wa pekee wa kweli,” anakusudia “kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia kwa mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.” (Matendo 17:24, 31) Mtume Paulo anamtaja Yesu kuwa “mwanamume”—naam, mwenye cheo cha chini kuliko Mungu—ambaye Mungu alimfufua akaishi mbinguni.

Mtume Yohana pia alimfafanua Yesu kuwa wa cheo cha chini kuliko Mungu. Yohana alisema kwamba aliandika Injili yake ili wasomaji waamini kwamba “Yesu ndiye Kristo Mwana wa Mungu,” wala si kwamba ndiye Mungu. (Yohana 20:31) Yohana pia alipata maono ya mbinguni ambamo alimwona “Mwana-Kondoo,” ambaye anamwita Yesu katika Injili yake. (Yohana 1:29) Mwana-Kondoo huyo anasimama pamoja na wengine 144,000 ambao Yohana anasema “wamenunuliwa [au kufufuliwa] kutoka duniani.” Yohana anaeleza kwamba wale 144,000 wana “jina [la Mwana-Kondoo] na jina la Baba yake . . . juu ya mapaji ya nyuso zao.”—Ufunuo 14:1, 3.

Je, “Mwana-Kondoo” huyo angeweza kuwa ndiye “Baba”? Bila shaka la. Katika Biblia, hao ni watu wawili tofauti. Hata wana majina tofauti.

Jina la Mwana-Kondoo na la Baba

Kama vile tumeona, jina la Mwana wa Mungu, ambaye ndiye Mwana-Kondoo, ni Yesu. (Luka 1:30-32) Namna gani jina la Baba yake? Linapatikana katika Biblia mara elfu kadhaa. Kwa mfano, andiko la Zaburi 83:18 linasema: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” Inasikitisha kwamba jina la Mungu, Yehova, limeondolewa katika tafsiri nyingi za Biblia na badala yake majina kama vile “BWANA” na “MUNGU,” yakiwa yameandikwa kwa herufi kubwa hutumiwa. Herufi hizo kubwa zinakusudiwa kumtofautisha Yehova na wengine wanaoitwa miungu au mabwana. * Hata hivyo, katika tafsiri nyingi za Biblia, jina la Mungu limerudishwa mahali pake panapofaa.

Biblia ya Kiingereza American Standard Version (1901) ni mojawapo ya Biblia ambazo zimelirudisha jina la Mungu, Yehova, mahali pake panapofaa. Dibaji yake inasema: “Baada ya kufanya uchunguzi kwa uangalifu, wasahihishaji wa American Standard Version, walikata kauli kwa pamoja kwamba ushirikina wa Wayahudi wa kwamba jina la Mungu ni takatifu sana lisiweze kutamkwa, haupaswi kuathiri tafsiri za Agano la Kale katika Kiingereza au lugha nyingine, bali tafsiri hizo zinapaswa kuwa kama tafsiri kadhaa za wamishonari wa kisasa.” *

Fundisho la Utatu Lilianzia Wapi?

Vipi, basi, kuhusu fundisho la kwamba Yehova na Yesu, ni Mungu yuleyule, kama fundisho la Utatu linavyodai? Katika toleo lake la Aprili-Juni 1999, gazeti moja (The Living Pulpit) liliufafanua Utatu hivi: “Kuna Mungu na Baba mmoja, Bwana mmoja Yesu Kristo, na Roho Mtakatifu mmoja, ‘watu’ watatu . . . ambao wanalingana au ni mtu yuleyule . . . ; watu watatu ambao wote ni Mungu, wenye sifa zilezile za asili, na hata hivyo wakiwa tofauti, na wenye nyutu tofauti.” *

Fundisho hilo lisiloeleweka la Utatu lilianzia wapi? Toleo la Mei 20-27, 1998, la gazeti moja (Christian Century), linamnukuu kasisi anayekiri kwamba Utatu ni “fundisho la kanisa wala si la Yesu.” Ingawa Utatu si fundisho la Yesu, je, linapatana na mafundisho yake?

Baba Ni Mkuu Kuliko Mwana

Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako litakaswe.” Baba yetu wa mbinguni, ambaye jina lake ni Yehova, anatajwa katika Biblia kuwa mkuu kuliko Mwana wake. Kwa mfano, Yehova amekuwapo “kizazi baada ya kizazi.” Lakini Biblia inasema kwamba Yesu ndiye “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote.” Yesu mwenyewe alifundisha kwamba Yehova ni mkuu kuliko yeye aliposema: “Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Mathayo 6:9; Zaburi 90:1, 2; Wakolosai 1:15; Yohana 14:28) Hata hivyo, kulingana na fundisho la Utatu, Baba na Mwana ni “Mungu.”

Katika sala Yesu alikazia kwamba Baba ni mkuu kuliko Mwana, na kwamba Baba ni mtu tofauti. Alisali hivi kabla ya kuuawa: “Baba, ikiwa unataka, niondolee kikombe hiki [yaani, kifo cha aibu]. Hata hivyo, acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Ikiwa Mungu na Yesu ni “mtu mmoja” kama fundisho la Utatu linavyosema, ingewezekanaje tamaa au mapenzi ya Yesu yawe tofauti na ya Baba yake?—Waebrania 5:7, 8; 9:24.

Isitoshe, ikiwa Yehova na Yesu ni mtu yuleyule, mmoja wao angewezaje kujua mambo ambayo yule mwingine hajui? Kwa mfano, Yesu alisema hivi kuhusu wakati wa kuhukumiwa kwa ulimwengu: “Kuhusu siku ile au saa ile hakuna mtu anayejua, wala malaika mbinguni wala Mwana, ila Baba.”—Marko 13:32.

Fundisho la Utatu na Kanisa

Utatu si fundisho la Yesu wala la Wakristo wa awali. Kama tulivyoona, ni “fundisho la kanisa.” Katika toleo la 1999 kuhusu Utatu, gazeti moja (The Living Pulpit) lilisema hivi: “Wakati mwingine, ni kana kwamba kila mtu anafikiri utatu ni fundisho la msingi la Kikristo,” lakini makala hiyo iliongeza kusema kwamba hilo “si fundisho la Biblia.”

Kichapo kimoja cha 1967 (New Catholic Encyclopedia) kinazungumzia kwa urefu fundisho la Utatu na kinakiri hivi: “Baada ya kuchunguza mambo yote, inaonekana Fundisho la Utatu lilianza mwishoni mwa karne ya 4 . . . . Ile dhana ya ‘Mungu mmoja katika Watu watatu’ haikuwa imetia mizizi, wala haikuwa imekubaliwa katika maisha ya Wakristo na imani za kidini za watu, kabla ya mwisho wa karne ya 4.”

Martin Werner, profesa wa Chuo Kikuu cha Bern, Uswisi, alisema hivi: “Popote katika Agano Jipya panapozungumzia uhusiano wa Yesu na Mungu, Baba, iwe panazungumzia kuhusu kuja kwake duniani akiwa mwanadamu au kuhusu kuwa kwake Masihi, inaeleweka na kuonekana waziwazi kwamba yuko chini yake.” Ni wazi kwamba mambo ambayo Yesu na Wakristo wa kwanza waliamini ni tofauti kabisa na fundisho la Utatu la makanisa leo. Basi, fundisho hilo lilianzia wapi?

Chanzo cha Utatu

Biblia inataja kwamba kuna miungu mingi inayoabudiwa na watu, kutia ndani Ashtorethi, Milkomu, Kemoshi, na Moleki. (1 Wafalme 11:1, 2, 5, 7) Hata watu wengi katika taifa la kale la Israeli wakati mmoja waliamini kwamba Baali ndiye Mungu wa kweli. Kwa hiyo, Eliya, nabii wa Yehova akawaambia hivi: “Ikiwa Yehova ndiye Mungu wa kweli, mfuateni yeye; lakini ikiwa ni Baali, mfuateni yeye.”—1 Wafalme 18:21.

Kabla ya Yesu kuzaliwa, wapagani walizoea kuabudu miungu mitatu-mitatu. Mwanahistoria Will Durant anasema: “Dhana za utatu mtakatifu zilianzia Misri.” Katika kichapo kimoja (Encyclopædia of Religion and Ethics) James Hastings aliandika: “Kwa mfano, katika dini ya Kihindi kuna miungu watatu: Brahmā, Siva, na Viṣṇu; na katika dini ya Misri kuna miungu watatu Osiris, Isis, na Horus.”

Kwa hiyo kuna miungu mingi. Je, Wakristo wa kwanza walikiri hivyo? Na je, walimwona Yesu kuwa Mungu Mweza-Yote?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kwa mfano, ona andiko la Zaburi 110:1 katika Union Version. Yesu na Petro walinukuu mstari huu.—Mathayo 22:42-45; Matendo 2:34-36.

^ fu. 12 Soma makala yenye kichwa “Je, Tunapaswa Kulitumia Jina la Mungu?” kwenye ukurasa wa 31 wa gazeti hili.

^ fu. 14 Ile Imani ya Athanasia, iliyoundwa mamia kadhaa ya miaka baada ya kifo cha Yesu, ilifasiri Utatu hivi: “Baba ni Mungu: Mwana ni Mungu: na Roho Mtakatifu ni Mungu. Hata hivyo wao si Miungu mitatu bali Mungu mmoja.”

[Picha katika ukurasa wa 7]

MISRI

Utatu wa Horus, Osiris, na Isis, katika milenia ya pili K.W.K.

[Picha katika ukurasa wa 7]

PALMYRA, SYRIA

Utatu wa mungu mwezi, Bwana wa Mbingu, na mungu jua, karne ya kwanza hivi W.K.

[Picha katika ukurasa wa 7]

INDIA

Utatu wa mungu wa Kihindu, karne ya saba hivi W.K.

[Picha katika ukurasa wa 7]

NORWAY

Utatu (Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu), karne ya 13 hivi W.K.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 7]

Top two photos: Musée du Louvre, Paris