Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilimtumikia Mungu Licha ya Magumu

Nilimtumikia Mungu Licha ya Magumu

Nilimtumikia Mungu Licha ya Magumu

SIMULIZI LA IVAN MIKITKOV

Afisa wa Halmashauri ya Usalama wa Kitaifa ya Sovieti (KGB) alinionya hivi: “Ukikaa katika mji wetu, utarudishwa gerezani.” Nilikuwa tu nimetoka gerezani baada ya kumaliza kifungo cha miaka 12. Baba na mama yangu walikuwa wagonjwa sana na walihitaji msaada wangu. Ningefanya nini?

NILIZALIWA mwaka wa 1928 katika kijiji cha T̩aul, huko Moldova. * Nilipokuwa na umri wa mwaka mmoja, baba yangu Alexander, alienda Ias̩i, Rumania, ambako alikutana na Wanafunzi wa Biblia, kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Aliporudi T̩aul, aliwaeleza majirani na familia yake mambo aliyojifunza. Baada ya muda, kikundi kidogo cha Wanafunzi wa Biblia kilianzishwa huko T̩aul.

Familia yetu ilikuwa na wavulana wanne, nami nilikuwa kitinda-mimba. Tangu utotoni nilishirikiana na watu wa kiroho ambao waliniwekea mfano mzuri. Kadiri miaka ilivyopita, nilitambua kwamba ningekabili upinzani kwa sababu ya kumtumikia Yehova na mambo yangekuwa magumu. Hata leo bado ninakumbuka jinsi polisi walivyopekua-pekua nyumba yetu, wakitafuta vitabu vyetu vya Biblia vilivyofichwa. Pindi hizo hazikuniogopesha. Nilijifunza katika funzo letu la Biblia kwamba Mwana wa Mungu, Yesu Kristo, na hata wanafunzi wake waliteswa. Mara nyingi katika mikutano yetu tulikumbushwa kwamba wafuasi wa Yesu wanapaswa kutazamia mateso.—Yohana 15:20.

Twaimarishwa Kukabiliana na Mateso

Mnamo mwaka wa 1934, nilipokuwa na umri wa miaka sita tu, barua ilisomwa katika kutaniko letu la T̩aul ikitujulisha kuhusu mateso ya Wakristo wenzetu nchini Ujerumani. Tulihimizwa kusali kwa ajili yao. Sijasahau kamwe barua hiyo ingawa nilikuwa mtoto mdogo.

Miaka minne baadaye uaminifu wangu ulijaribiwa kwa mara ya kwanza. Wakati wa somo la kidini shuleni, kasisi Mwothodoksi aliniamuru kila mara nivae msalaba shingoni. Nilipokataa, aliwaomba wanafunzi wengine darasani wavae misalaba yao ili kuonyesha kwamba walikuwa wafuasi wa kanisa. Kasisi alininyooshea kidole na kuwauliza hivi wanafunzi: “Je, mngependa kuwa na mtu kama huyu darasani? Kila mtu asiyemtaka ainue mkono.”

Wanafunzi wote waliinua mikono kwa kuwa walimwogopa kasisi. Akaniambia hivi: “Waona, hakuna mtu anayekutaka. Ondoka mara moja.” Baada ya siku kadhaa, msimamizi wa shule alikuja nyumbani kwetu. Baada ya kuzungumza na wazazi wangu, aliniuliza ikiwa nilitaka kuendelea na shule. Nilimwambia nitaendelea. Akajibu: “Maadamu mimi ni msimamizi, utaendelea na shule na kasisi hataweza kukuzuia.” Alitimiza ahadi yake, kwani kasisi hakunisumbua tena.

Mateso Yaongezeka

Katika mwaka wa 1940, eneo tuliloishi la Bessarabia, likawa sehemu ya Muungano wa Sovieti. Mnamo Juni 13 na 14, 1941, watu wote waliokuwa mashuhuri kisiasa au katika jamii walipelekwa uhamishoni Siberia. Mashahidi wa Yehova hawakupelekwa uhamishoni wakati huo. Hata hivyo, tangu wakati huo tulihubiri na kufanya mikutano kwa busara zaidi.

Mwishoni wa Juni 1941, Ujerumani ilishambulia ghafula Muungano wa Sovieti ambao kufikia wakati huo ulikuwa na ushirikiano mzuri na Ujerumani. Baada ya muda mfupi, majeshi ya Rumania yaliuteka tena Bessarabia. Kwa mara nyingine tena tukatawaliwa na Rumania.

Katika vijiji vya karibu, Mashahidi waliokataa kujiunga na jeshi la Rumania walikamatwa, na wengi wao walihukumiwa miaka 20 na kazi ngumu. Baba aliitwa kwenye kituo cha polisi na kupigwa vibaya sana kwa sababu ya kuwa Shahidi. Mimi pia nililazimishwa kutoka shuleni ili niende kanisani.

Mambo yalibadilika wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Mnamo Machi 1944, Wasovieti waliteka mara moja sehemu ya kaskazini ya Bessarabia. Kufikia Agosti, walikuwa wameteka nchi nzima. Wakati huo nilikuwa na umri wa miaka 16 hivi.

Punde si punde, wanaume wote wakakamavu katika kijiji chetu walikuwa wameandikishwa katika jeshi la Sovieti. Lakini Mashahidi hawakujiunga na upande wowote. Kwa hiyo, walifungwa miaka kumi gerezani. Mnamo Mei 1945, Ujerumani ilisalimu amri na Vita vya Pili vya Ulimwengu vikaisha huko Ulaya. Hata hivyo, Mashahidi wengi huko Moldova walikaa gerezani hadi mwaka wa 1949.

Matatizo Baada ya Vita

Baada ya vita kwisha mwaka wa 1945, kulikuwa na ukame sana nchini Moldova. Licha ya ukame huo, serikali ya Sovieti iliendelea kuwatoza wakulima kodi kubwa ya mazao yao. Hilo likasababisha njaa kubwa sana. Kufikia mwaka wa 1947, nilikuwa nimeona maiti nyingi katika barabara za T̩aul. Ndugu yangu Yefim alikufa, na kwa majuma kadhaa nilidhoofika sana kwa sababu ya njaa hata sikuweza kutembea. Lakini njaa iliisha, na Mashahidi waliokuwako wakaendelea na huduma ya hadharani. Nilihubiri katika kijiji chetu, naye ndugu yangu Vasile, ambaye alinizidi umri kwa miaka saba, alihubiri katika vijiji vya karibu.

Mashahidi walipoendelea kuhubiri kwa bidii, wenye mamlaka walianza kuwachunguza kwa makini zaidi. Serikali ya Sovieti ilianza kupekua nyumba zetu ili kutafuta vichapo vya Biblia na kutukamata kwa sababu tulihubiri na hatukushiriki siasa wala kutumikia jeshini. Mashahidi kadhaa kutoka makutaniko ya karibu walipelekwa uhamishoni huko Siberia mwaka wa 1949. Basi kwa mara nyingine tena wale waliobaki walijitahidi kuhubiri kwa uangalifu zaidi.

Wakati huo, nilikuwa na ugonjwa mbaya sana ambao ulinidhoofisha polepole. Mwishowe madaktari walisema kwamba nilikuwa na TB ya mifupa, na mwaka wa 1950 mguu wangu wa kulia ulifungwa plasta.

Kupelekwa Uhamishoni Siberia

Mnamo Aprili 1, 1951, mguu wangu ukiwa na plasta, mimi, familia yangu pamoja na Mashahidi wengine tulikamatwa na kupelekwa uhamishoni Siberia. * Hatukuwa na wakati wa kutosha kujitayarisha, hivyo tulibeba chakula kidogo tu. Baada ya muda mfupi, kikaisha.

Hatimaye, baada ya kukaa majuma mawili ndani ya gari-moshi, tulifika Asino, katika wilaya ya Tomsk. Tulishushwa kama ng’ombe. Ingawa kulikuwa na baridi kali sana, tulifurahia hewa safi. Mnamo mwezi wa Mei, theluji ilipoyeyuka, tulisafirishwa umbali wa kilometa 100 kwa meli hadi Torba, ambako kulikuwa na kambi ya kupasua mbao katika misitu ya Siberia. Tukaanza kifungo na kazi ngumu—ambacho tuliambiwa kingeendelea milele.

Ingawa kufanya kazi ngumu katika kambi ya kupasua mbao ni tofauti na kufungwa gerezani, tulikuwa tukichunguzwa daima. Wakati wa usiku tulilala pamoja katika behewa. Wakati wa kiangazi, tulijenga makao sahili ambayo kwa sehemu yalichimbiwa ardhini, ambamo tungeishi wakati wa baridi kali.

Kwa sababu ya plasta niliyokuwa nayo mguuni, nilipewa kazi ya kutengeneza misumari badala ya kufanya kazi misituni. Kazi hiyo iliniwezesha kunakili kisiri magazeti ya Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vya Biblia. Kwa kawaida, vichapo hivyo viliingizwa kisiri katika eneo letu kutoka Ulaya magharibi, umbali wa maelfu ya kilometa.

Nakamatwa na Kufungwa

Plasta niliyokuwa nayo iliondolewa mwaka wa 1953. Licha ya kujitahidi kuwa mwangalifu, polisi wa KGB waligundua utendaji wangu wa kiroho pamoja na kazi yangu ya kunakili vichapo vya Biblia. Mwishowe, nilihukumiwa miaka 12 katika kambi ya gereza pamoja na Mashahidi wengine. Hata hivyo, wakati wa kesi, sote tulitoa ushahidi mzuri kumhusu Mungu wetu, Yehova, na makusudi yake ya upendo kwa wanadamu.

Mwishowe tulipelekwa kwenye kambi mbalimbali karibu na Irkutsk, mamia ya kilometa upande wa mashariki. Watu ambao walionwa kuwa maadui wa Serikali ya Sovieti waliteswa katika kambi hizo. Kuanzia Aprili 8, 1954, hadi mapema mwaka wa 1960, nilifungwa katika kambi 12 za kazi ngumu. Baadaye, nilisafirishwa zaidi ya kilometa 3,000 kuelekea magharibi kwenye kambi kubwa za Mordovia za wafungwa kilometa 400 hivi kusini-mashariki mwa Moscow. Nilipata fursa ya kukutana na Mashahidi waaminifu kutoka sehemu nyingi za Muungano wa Sovieti.

Wasovieti waligundua kwamba Mashahidi waliporuhusiwa kuchangamana na wafungwa wengine wasio Mashahidi, baadhi ya wafungwa hao pia walikuja kuwa Mashahidi. Kwa hiyo, katika magereza makubwa ya Mordovia yaliyofikia umbali wa kilometa 30 au zaidi, ambayo yalikuwa na kambi nyingi za kazi ngumu, walijaribu kututenga na wafungwa wengine. Zaidi ya Mashahidi 400 waliwekwa pamoja katika kambi yetu. Dada Wakristo wapatao 100 au zaidi walikuwa katika kambi nyingine kubwa umbali wa kilometa kadhaa.

Nilijitahidi sana kusaidia kupanga mikutano ya Kikristo katika kambi yetu, vilevile kunakili vichapo vya Biblia ambavyo vililetwa kambini kisiri. Bila shaka wasimamizi wa kambi waligundua jambo hilo. Muda mfupi baadaye, mnamo Agosti 1961, nilihukumiwa mwaka mmoja katika gereza maarufu la Vladimir la enzi ya utawala wa Zari, kilometa 200 hivi kaskazini-mashariki mwa Moscow. Rubani Mmarekani Francis Gary Powers, ambaye alikuwa akiendesha ndege iliyopigwa risasi Mei 1, 1960, ilipokuwa ikipeleleza Urusi, alifungwa pia katika gereza hilo hadi Februari 1962.

Nilipokuwa katika Gereza la Vladimir, nilipewa chakula kidogo tu cha kuniwezesha kuishi. Nilistahimili njaa kwa sababu nikiwa kijana nilizoea hali hiyo, lakini nilishindwa kuvumilia baridi kali sana ya mwaka wa 1961 na 1962. Mabomba ya kupasha joto gereza yaliharibika, na hivyo chumba changu kilikuwa na baridi kali kupindukia. Daktari mmoja aliona hali yangu yenye kusikitisha na kufanya mipango ili nipelekwe kwenye chumba kingine kilichokuwa afadhali katika majuma ya kwanza ya baridi kali.

Naimarishwa Kuvumilia Magumu

Mawazo yasiyofaa yanaweza kumvunja mtu moyo baada ya kukaa peke yake kwa miezi kadhaa, na wasimamizi wa gereza hutaka hivyo. Hata hivyo, nilisali daima nikaimarishwa na roho ya Yehova pamoja na maandiko niliyokumbuka.

Nilipokuwa katika Gereza la Vladimir nilikumbuka maneno ya mtume Paulo kwamba “tunakazwa katika kila njia, lakini hatubanwi kupita kiasi cha kuweza kusonga,” na “tunafadhaishwa, lakini si bila njia ya kutokea kabisa.” (2 Wakorintho 4:8-10) Baada ya mwaka mmoja, nilirudishwa katika kambi kubwa ya Moldova. Nikakamilisha kifungo changu cha miaka 12 katika kambi hizo mnamo Aprili 8, 1966. Baada ya kuachiliwa huru, walisema kwamba mimi ni mtu “asiyeweza kubadilika.” Kwangu, huo ulikuwa uthibitisho wa wazi kwamba nilidumisha uaminifu wangu kwa Yehova.

Mara nyingi nimeulizwa jinsi tulivyopata na kunakili vichapo vya Biblia katika kambi za Sovieti licha ya jitihada za kutuzuia kufanya hivyo. Si watu wengi waliojua siri hiyo, kama anavyosema mfungwa mmoja wa kisiasa kutoka Latvia ambaye alifungwa miaka minne katika kambi ya wanawake ya Potma. Aliandika hivi baada ya kufunguliwa mwaka wa 1966: “Kwa njia fulani Mashahidi waliendelea kupata vichapo vingi.” Amalizia hivi: “Ni kana kwamba malaika waliruka kambini na kudondosha vichapo hivyo.” Kwa kweli, tulitimiza kazi hiyo kwa msaada wa Mungu tu!

Kipindi cha Uhuru wa Kadiri

Nilipoachiliwa huru, wale walioongoza kazi ya kuhubiri waliniomba nihamie magharibi mwa Ukrainia, karibu Moldova, kuwasaidia ndugu zetu wa Moldova. Hata hivyo, singeweza kufanya mengi kwa sababu niliwahi kuwa mfungwa, na polisi wa KGB walinichunguza daima. Baada ya miaka miwili, baada ya kutishwa kwamba ningefungwa tena, nilihamia kwenye jamhuri ya Sovieti ya Kazakhstan, ambako wenye mamlaka hawakuchunguza sana vitambulisho. Kisha katika mwaka wa 1969, wazazi wangu walipokuwa wagonjwa sana, nilihamia Ukrainia ili kuwatunza. Nikiwa kaskazini mwa jiji kuu la Donetsk, katika mji wa Artyomosk, afisa mmoja wa KGB alinitisha kwamba angenirudisha gerezani, kama ninavyosimulia mwanzoni mwa makala hii.

Baadaye niligundua kwamba afisa huyo alitaka tu kunitisha. Hakuwa na sababu nzuri ya kunishtaki. Niliazimia kuendelea na huduma yangu ya Kikristo, lakini polisi wa KGB walinichunguza kila mahali nilipoenda, hivyo niliendelea kuwatunza wazazi wangu. Baba na Mama walikufa wakiwa waaminifu kwa Yehova. Baba alikufa Novemba 1969, lakini Mama aliendelea kuishi hadi Februari 1976.

Niliporudi Ukrainia, nilikuwa na umri wa miaka 40. Nilipokuwa nikiwatunza wazazi wangu, nilishirikiana na kutaniko ambamo mlikuwa na dada mmoja kijana aliyeitwa Maria. Alikuwa na umri wa miaka minane tu wakati ambapo, kama familia yetu, yeye na wazazi wake walipohamishwa kutoka Moldova hadi Siberia mwanzoni mwa Aprili 1951. Maria alisema kwamba alivutiwa na uimbaji wangu. Huo ulikuwa mwanzo, na ingawa sote tulitumia wakati mwingi katika huduma, hatukukosa wakati wa kusitawisha urafiki. Kufikia mwaka wa 1970, nilikuwa nimemsadikisha tufunge ndoa.

Muda si muda, binti yetu Lidia akazaliwa. Kisha, mwaka wa 1983 Lidia alipokuwa na umri wa miaka kumi, mtu mmoja aliyekuwa Shahidi zamani alinisaliti kwa polisi wa KGB. Kufikia wakati huo, nilikuwa nimetumikia nikiwa mwangalizi anayesafiri kwa miaka kumi hivi kotekote mashariki mwa Ukrainia. Wale waliopinga utendaji wetu wa Kikristo waliwakusanya watu fulani ili watoe ushahidi wa uwongo wakati wa kusikizwa kwa kesi, nikahukumiwa kifungo cha miaka mitano.

Nilipokuwa gerezani sikuruhusiwa kushirikiana na Mashahidi wengine. Hata hivyo, hakuna kitu au mtu yeyote angeweza kunizuia kumfikia Yehova, na sikuzote alinitia nguvu. Zaidi ya hayo, nilipata nafasi za kuwahubiria wafungwa wengine. Hatimaye, baada ya kukaa gerezani kwa miaka minne, niliachiliwa na kuungana tena na mke na binti yangu, ambao walidumisha uaminifu wao kwa Yehova.

Kurudi Moldova

Tulikaa Ukrainia kwa mwaka mwingine mmoja, kisha tukarudi kuishi Moldova ambako ndugu wakomavu wenye uzoefu walihitajika. Wakati huo, kulikuwa na uhuru zaidi wa kwenda sehemu mbalimbali katika nchi ya Sovieti. Tulifika Bălţi mwaka wa 1988, ambako Maria aliishi kabla ya kupelekwa uhamishoni miaka 37 mapema. Kufikia mwaka wa 1988 kulikuwa na Mashahidi 375 hivi katika jiji la pili kwa ukubwa nchini Moldova; leo kuna zaidi ya Mashahidi 1,500! Hata ingawa tuliishi Moldova, bado nilitumikia nikiwa mwangalizi anayesafiri huko Ukrainia.

Kufikia wakati tengenezo letu lilipoandikishwa kisheria katika Muungano wa Sovieti mnamo Machi 1991, maelfu ya watu walikuwa wamekatishwa tamaa na kushindwa kwa Ukomunisti. Wengi walitatanika na hawakuwa na tumaini lolote la wakati ujao. Kwa hiyo Moldova ilipokuwa jamhuri huru, majirani wetu na hata baadhi ya wale waliotutesa zamani walipendezwa sana na kweli za Biblia! Baada ya kupelekwa uhamishoni mwaka wa 1951, ni Mashahidi wachache sana waliobaki Moldova, lakini sasa kuna zaidi ya Mashahidi 18,000 katika nchi hiyo ndogo yenye watu 4,200,000. Kwa kweli mateso tuliyopata hayawezi kulinganishwa na mambo mazuri sana ambayo tumefurahia!

Katikati ya miaka ya 1990, niliacha kutumikia nikiwa mwangalizi anayesafiri kwa sababu ya afya mbaya. Nyakati nyingine mimi huvunjika moyo kwa sababu ya hali yangu. Hata hivyo, nimetambua kwamba Yehova anajua kinachoweza kututia moyo. Yeye hutupa kitia-moyo tunachohitaji wakati unaofaa. Kama ningeweza kuanza maisha yangu upya, je, ningechagua njia tofauti? Hapana. Badala yake, laiti ningekuwa na ujasiri zaidi katika huduma yangu na kuwa mtendaji zaidi na mwenye nguvu zaidi.

Nahisi kwamba Yehova amenibariki na watumishi wake wote wamebarikiwa licha ya hali zao mbalimbali. Tuna tumaini jangavu, imani iliyo hai, na uhakika wa kwamba karibuni kila mtu atakuwa na afya kamilifu katika ulimwengu mpya wa Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika makala hii tutatumia jina la kisasa la nchi hiyo, Moldova badala ya majina yake ya zamani.

^ fu. 21 Miisho-juma miwili ya kwanza ya Aprili 1951, Wasovieti walitekeleza mpango wa kuwakamata Mashahidi wa Yehova zaidi ya 7,000 pamoja na familia zao walioishi katika sehemu ya magharibi ya Muungano wa Sovieti na kuwasafirisha maelfu ya kilometa kwa gari-moshi upande wa mashariki hadi Siberia.

[Picha katika ukurasa wa 20, 21]

Makao yetu tukiwa uhamishoni huko Torba, Siberia, 1953. Baba na Mama (kushoto), na ndugu yangu Vasile na mwana wake (kulia)

[Picha katika ukurasa wa 21]

Gerezani, 1955

[Picha katika ukurasa wa 23]

Dada Wakristo huko Siberia, Maria (chini kushoto) alikuwa na umri wa miaka 20 hivi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Tukiwa na binti yetu, Lidia

[Picha katika ukurasa wa 23]

Harusi yetu, mwaka wa 1970

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa na Maria leo