Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wale Wanaoitwa ‘Miungu’”

“Wale Wanaoitwa ‘Miungu’”

“Wale Wanaoitwa ‘Miungu’”

MTUME Paulo alipomponya mwanamume aliyekuwa amelemaa huko Listra, watu walipaaza sauti na kusema: “Miungu imekuwa kama binadamu nayo imeshuka kwetu!” Wakamwita Paulo Herme, na mwandamani wake Barnaba, Zeu. (Matendo 14:8-14) Huko Efeso, Demetrio, fundi wa fedha, alionya kwamba ikiwa Paulo angeruhusiwa aendelee kuhubiri, ‘hekalu la Artemi, mungu mkuu wa kike, lingeonwa kuwa si kitu.’—Matendo 19:24-28.

Watu wa karne ya kwanza—kama watu wengi leo—waliabudu “wale wanaoitwa ‘miungu,’ iwe wako mbinguni au duniani.” Paulo alisema: “[Kuna] ‘miungu’ mingi na ‘mabwana’ wengi.” Hata hivyo, alieleza pia: “Kwa kweli kwetu sisi kuna Mungu mmoja aliye Baba,” na “kuna Bwana mmoja, Yesu Kristo.”—1 Wakorintho 8:5, 6.

Je, Yesu Pia Aliitwa Mungu?

Yesu hakudai kamwe kuwa Mungu. Hata hivyo, akiwa mtawala aliyewekwa rasmi na Yehova, anaitwa katika unabii wa Isaya, “Mungu Mwenye Nguvu,” na “Mkuu wa Amani.” Unabii wa Isaya unaongeza: “Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani.” (Isaya 9:6, 7) Kwa hiyo, akiwa “Mkuu”—mwana wa Mfalme Mkuu, Yehova—Yesu atakuwa Mtawala katika serikali ya kimbingu ya “Mungu Mweza-Yote.”—Kutoka 6:3.

Hata hivyo, huenda mtu akauliza, ‘Yesu ni “Mungu Mwenye Nguvu,” katika maana gani, na je, mtume Yohana hakusema kwamba Yesu mwenyewe ni Mungu?’ Katika tafsiri ya Biblia ya Union Version, andiko la Yohana 1:1 linasema: “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu.” Watu fulani hudai kwamba “Neno,” aliyezaliwa duniani akiwa Yesu, ndiye Mungu Mweza-Yote mwenyewe. Je, ni kweli?

Mstari huo ukifasiriwa kumaanisha kwamba Yesu ndiye Mungu Mweza-Yote mwenyewe, basi utapinga taarifa inayotangulia ya kwamba “Neno alikuwako kwa Mungu.” Mtu aliye “kwa” mwingine hawezi kuwa mtu yuleyule. Tafsiri nyingi za Biblia huonyesha tofauti iliyopo, zikitaja waziwazi kwamba Neno hakuwa Mungu Mweza-Yote. Kwa mfano, tafsiri mbalimbali za Biblia zinasema hivi: “Neno alikuwa mungu,” na “Neno alikuwa na sifa za Mungu.” *

Mistari ya Biblia ambayo katika lugha ya Kigiriki inafanana na Yohana 1:1 hutumia neno “mungu.” Kwa mfano, umati ulisema hivi kumhusu Herode Agripa wa Kwanza: ‘Ni sauti ya mungu.’ Na wakati ambapo Paulo hakufa baada ya kuumwa na nyoka mwenye sumu, watu walisema: “Yeye ni mungu.” (Matendo 12:22; 28:3-6) Kusema kwamba Neno ni “mungu” wala si Mungu, kunapatana na sarufi ya Kigiriki na mafundisho ya Biblia.—Yohana 1:1.

Hebu fikiria jinsi Yohana alivyomtambulisha “Neno” katika sura ya kwanza ya Injili yake. Aliandika: “Neno akawa mwili, akakaa katikati yetu, nasi tukautazama utukufu wake, utukufu kama ule ulio [si wa Mungu bali] wa mwana mzaliwa-pekee kutoka kwa baba.” Kwa hiyo, “Neno,” aliyekuwa mwili, aliishi duniani akiwa Yesu na watu walimwona. Kwa hiyo, hangeweza kuwa Mungu Mweza-Yote, ambaye Yohana anasema hivi juu yake: “Hakuna mwanadamu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.”—Yohana 1:14, 18.

Huenda mtu akauliza, ‘Basi, kwa nini Tomasi alipomwona Yesu aliyekuwa amefufuliwa, alisema “Bwana wangu na Mungu wangu!”?’ Kama tulivyoona, Yesu ni mungu kwa kuwa ana sifa kama za Mungu, lakini siye Baba. Yesu alikuwa amemwambia Maria Magdalene: “Ninapanda kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu na kwa Mungu wangu na Mungu wenu.” Pia, kumbuka sababu iliyomfanya Yohana aandike Injili yake. Mistari mitatu baada ya kusimulia kisa cha Tomasi, Yohana anaeleza kwamba aliandika ili watu wapate “kuamini kwamba Yesu ndiye Kristo Mwana wa Mungu”—si kwamba ndiye Mungu.—Yohana 20:17, 28, 31.

Ni Nani Aliye “Mungu wa Ulimwengu Huu”?

Ni wazi kwamba kuna miungu mingi. Kama vile tumeona, majina ya baadhi yao yanatajwa katika Biblia. Hata hivyo, watu walioona nguvu za Yehova zamani za kale walisema hivi: “Yehova ndiye Mungu wa kweli! Yehova ndiye Mungu wa kweli!” (1 Wafalme 18:39) Hata hivyo, kuna mungu mwingine mwenye nguvu. Biblia inasema: “Hao hawaamini kwa sababu yule mungu wa ulimwengu huu amezitia giza akili zao.”—2 Wakorintho 4:4, Biblia Habari Njema.

Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu aliwaonya wanafunzi wake mara tatu kuhusu mungu huyo, akimwita “mtawala wa ulimwengu huu.” Yesu alisema kwamba mtawala au mungu huyo mwenye nguvu “atatupwa nje.” (Yohana 12:31; 14:30; 16:11) Mungu huyo ni nani, na ulimwengu anaotawala ni nini?

Si mwingine ila yule malaika mwasi, Shetani Ibilisi. Tunajuaje? Biblia inaeleza kwamba alipomjaribu Yesu, Shetani alimwonyesha “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo, naye akamwambia: ‘Nitakupa mambo yote haya ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.’” (Mathayo 4:8, 9) Hilo halingekuwa jaribu kamwe ikiwa Shetani angekuwa akimwahidi Yesu vitu visivyo vyake. Mtume Yohana alisema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.”—1 Yohana 5:19.

Kumbuka kwamba Yesu aliahidi: “Mtawala wa ulimwengu huu atatupwa nje.” (Yohana 12:31) Kwa kweli, ulimwengu, au mfumo huu wa mambo, utaondolewa pamoja na mtawala wake, kama ilivyotabiriwa na mtume Yohana aliposema: “Ulimwengu unapitilia mbali.” Hata hivyo, Yohana anaongeza: “Yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17) Sasa, na tuchunguze makusudi matukufu ya Mungu wa pekee wa kweli na jinsi tunavyoweza kufaidika kutokana nayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona The New Testament, ya James L. Tomanek; The Emphatic Diaglott, interlinear reading, ya Benjamin Wilson; The Bible—An American Translation, ya J.M.P. Smith na E. J. Goodspeed.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Watu wa Listra waliwaita Paulo na Barnaba miungu

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Yesu alimwambia Maria Magdalene: ‘Ninapanda kwenda kwa Mungu wangu na Mungu wenu’