Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Utatazama Sinema Zipi?

Utatazama Sinema Zipi?

Utatazama Sinema Zipi?

KATIKA miaka ya hivi karibuni, watu wamekuwa na maoni mbalimbali kuhusu kuongezeka kwa ngono, jeuri, na lugha chafu katika sinema au televisheni. Wengine husema kwamba picha fulani inayoonyesha ngono ni chafu, huku wengine wakisema kwamba ni jambo la kuwaziwa tu. Wengine husema kwamba sinema huonyesha watu wakiuawa ovyoovyo, hali wengine husema kwamba mauaji hayo ni ya haki. Wengine husema kwamba lugha chafu huchukiza huku wengine wakidai kwamba hayo ni mambo ya kawaida. Kile ambacho mtu mmoja huona kuwa kichafu, mwingine husema ni uhuru wa usemi. Mtu anaposikiliza maoni hayo mbalimbali anaweza kusema kwamba hayo ni mabishano yasiyo na maana yoyote.

Lakini kuzungumzia mambo yanayoonyeshwa na kusikiwa katika sinema si mabishano yasiyo na maana. Mambo hayo ni muhimu kwa wazazi na wote wanaothamini sana viwango vya maadili. Mwanamke mmoja kijana alilalamika hivi: “Ninapopuuza dhamiri yangu na kurudi kutazama sinema fulani, mimi huhisi vibaya sana. Mimi huona aibu kwa ajili ya wale waliotengeneza sinema hiyo mbovu na kwa ajili yangu mwenyewe kwa kuitazama. Ni kana kwamba kutazama sinema hiyo kumenishushia heshima.”

Kuweka Viwango

Kuhangaikia mambo yanayoonyeshwa katika sinema si jambo jipya. Wakati sinema zilipoanza kutengenezwa, watu walikasirika sana walipoona sinema zilizokazia ngono na uhalifu. Hatimaye, katika miaka ya 1930, sheria ambazo ziliweka mipaka kuhusu mambo ambayo yangeweza kuonyeshwa katika sinema zilitungwa nchini Marekani.

Kulingana na kichapo The New Encyclopædia Britannica, sheria hizo mpya “zilikandamiza sana, na kuzuia kuonyeshwa kwa jambo lolote ambalo linahusiana na mambo ambayo hufanywa na watu wazima. Zilikataza kuonyeshwa kwa ‘mambo yoyote ya kimahaba’ na uzinzi, ngono haramu, utongozi, na ubakaji wala mambo hayo hayakupaswa kutajwa isipokuwa tu iwe ni lazima kabisa kwa sababu yalihusiana na hadithi inayosimuliwa, na waliofanya mambo hayo waadhibiwe kufikia mwisho wa sinema hiyo.”

Kuhusiana na jeuri, filamu “hazikupaswa kuonyesha au kuzungumzia silaha zilizokuwa zikitumika wakati huo, kuonyesha uhalifu ukitendeka, polisi wakiuawa na wahalifu, ukatili au uchinjaji mwingi, au kuonyesha uuaji kimakusudi au kujiua, isipokuwa mambo hayo yawe ya lazima kwa hadithi hiyo. . . . Haikuruhusiwa kuonyesha kwamba uhalifu ulifaa chini ya hali zozote zile.” Kwa ufupi, sheria hizo zilisema kwamba “hakuna picha itakayoonyeshwa ambayo itashusha viwango vya maadili vya wale wanaoitazama.”

Viwango Vyachukua Mahali pa Sheria

Kufikia miaka ya 1950, watayarishaji wengi huko Hollywood walikuwa wakipuuza sheria hizo wakihisi kwamba zilikuwa zimepitwa na wakati. Hivyo, mnamo 1968, sheria hizo ziliondolewa na badala yake viwango vya sinema vikawekwa. * Kwa sababu ya viwango hivyo, sinema ingeweza kuonyesha wazi mambo yasiyofaa, lakini ingetiwa alama kuwaonya watu kwamba inapaswa kutazamwa tu na “watu wazima.” Jack Valenti aliyekuwa rais wa Shirika la Sinema la Marekani kwa miaka 40 hivi, alisema kwamba lengo lilikuwa “kuwaonya wazazi kimbele ili waweze kuamua sinema ambazo watoto wao wangeweza kutazama na zile ambazo hawakupaswa.”

Mfumo huo ulipoanzishwa, vizuizi viliondolewa. Sinema nyingi zilizotengenezwa Hollywood zilionyesha ngono, jeuri, na lugha chafu. Uhuru huo mpya ambao watengenezaji wa sinema walipata ulitokeza nafasi ya kuonyesha jambo lolote bila kuzuiwa. Hata hivyo, kupitia mfumo wa kuweka viwango, watu wangeweza kuonywa kimbele. Lakini je, viwango hivyo vinaweza kukuambia kila kitu unachohitaji kujua?

Mambo Ambayo Viwango Haviwezi Kufunua

Watu fulani wanahisi kwamba viwango hivyo vinapunguzwa kadiri miaka inavyopita. Uchunguzi uliofanywa na Shule ya Afya ya Umma ya Harvard unaunga mkono maoni hayo, kwa kuwa ulionyesha kwamba sinema zinazoonwa kuwa zinawafaa vijana wenye umri mdogo leo zina jeuri na ngono nyingi zaidi kuliko zile zilizoonyeshwa miaka kumi tu iliyopita. Uchunguzi huo ulimalizia kwa kusema kwamba “sinema zenye viwango vilevile zinaweza kutofautiana sana katika mambo yanayoonwa kuwa ya kuchukiza” na kwamba “viwango vinavyotegemea umri peke yake havina habari kamili kuhusu jeuri, ngono, lugha chafu, na mambo mengine yanayoonyeshwa katika sinema hiyo.” *

Wazazi ambao huwaruhusu bila kujali watoto wao waende kutazama sinema huenda wasijue ni sinema za aina gani zinazoonwa kuwa zinafaa leo. Kwa mfano, mchambuzi mmoja wa sinema alisema kwamba katika sinema moja huko Marekani ambayo ilionwa kuwa inawafaa vijana. Mwigizaji mkuu alikuwa “msichana mwenye umri wa miaka 17 ambaye alikuwa na uhuru wa kufanya chochote alichotaka, kila siku alilewa, alitumia dawa za kulevya, na kushiriki katika karamu za ukosefu wa adili na ngono za kupita kiasi na mvulana ambaye alikuwa tu amekutana naye.” Sinema nyingi huonyesha mambo kama hayo. Kwa kweli, gazeti The Washington Post Magazine linasema kwamba kutajwa kwa ngono ya kinywa kunaonekana kuwa “jambo linalokubaliwa kwa ukawaida” katika sinema zinazoonwa kuwa zinawafaa vijana. Kwa wazi, kiwango cha sinema hakipaswi kuwa jambo pekee linaloamua mambo yanayoonyeshwa katika filamu. Je, kuna mwongozo bora zaidi?

“Chukieni Yaliyo Mabaya”

Mfumo wa kuweka viwango hauwezi kuchukua mahali pa dhamiri iliyozoezwa na Biblia. Wanapofanya maamuzi yoyote kutia ndani yale yanayohusiana na vitumbuizo, Wakristo hujitahidi kufuata himizo la Biblia linalopatikana katika Zaburi 97:10: “Chukieni yaliyo mabaya.” Mtu anayechukia yaliyo mabaya ataona kuwa ni kosa kutumbuizwa na mambo ambayo Mungu huchukia.

Wazazi hasa wanapaswa kuwa waangalifu kuhusu sinema ambazo wanawaruhusu watoto wao kutazama. Lingekuwa jambo la kipumbavu kutazama tu kiwango cha sinema. Huenda sinema inayoonwa kuwa inamfaa mtoto wako mwenye umri fulani ikakazia maadili ambayo wewe ukiwa mzazi hukubali. Jambo hilo haliwashangazi Wakristo hata kidogo kwa kuwa ulimwengu hufikiri na kutenda kinyume na viwango vya Mungu. *Waefeso 4:17, 18; 1 Yohana 2:15-17.

Hiyo haimaanishi kwamba sinema zote ni mbaya. Lakini tunapaswa kuwa waangalifu. Kuhusiana na hilo, toleo la Amkeni! la Mei 22, 1997 lilisema hivi: “Kila mtu anapaswa kuchanganua mambo kwa uangalifu na kufanya maamuzi ambayo yatamwacha akiwa na dhamiri safi mbele ya Mungu na mwanadamu.”—1 Wakorintho 10:31-33.

Jinsi ya Kupata Vitumbuizo Vinavyofaa

Wazazi wanawezaje kuwa wateuzi wanapochagua sinema ambazo familia zao zitatazama? Fikiria maelezo yafuatayo kutoka kwa wazazi ulimwenguni pote. Huenda maelezo yao yakakusaidia kutafuta vitumbuizo vinavyofaa familia yako.—Ona pia sanduku “Tafrija za Aina Nyingine,” kwenye ukurasa wa 14.

“Sikuzote mimi au mke wangu tuliambatana na watoto wetu kwenda kutazama sinema walipokuwa wachanga,” asema Juan anayeishi Hispania. “Hawakwenda peke yao kamwe au kuambatana na vijana wengine. Sasa, wakiwa vijana, hawaendi kutazama sinema inapoonyeshwa mara ya kwanza; badala yake, sisi huonelea wasubiri hadi tusome maoni ya wachambuzi wa sinema au tusikie maoni ya watu tunaowatumaini. Kisha tukiwa familia tunaamua kama tutatazama sinema hiyo.”

Mark, anayeishi Afrika Kusini, humtia moyo kijana wake aeleze maoni yake kuhusu sinema zinazoonyeshwa katika majumba ya sinema. Mark anasema: “Mimi na mke wangu huanzisha mazungumzo kuhusu sinema fulani na kumwuliza mwana wetu maoni yake. Jambo hilo hutuwezesha kusikiliza maoni yake na kumtolea sababu. Kwa njia hiyo, tunaweza kuchagua sinema ambazo sisi sote tunaweza kufurahia.”

Rogerio, anayeishi Brazili, pia hutumia wakati pamoja na watoto wake kuchanganua filamu wanazotaka kutazama. Anasema: “Tukiwa pamoja, sisi husoma maoni ya wachambuzi. Mimi huambatana nao kwenye maduka ya video ili kuwafundisha jinsi ya kutazama jalada la video kuona kama huenda filamu isifae.”

Matthew anayeishi Uingereza huona kwamba inanufaisha kuzungumza na watoto wake kuhusu sinema wanazotaka kutazama. Anasema: “Tangu wakiwa wachanga, tuliwahusisha watoto wetu katika mazungumzo kuhusu filamu ambazo zingetupendeza tukiwa familia. Ikiwa tungeamua kutoitazama filamu fulani, mimi na mke wangu tungewaeleza sababu badala ya kuwakataza tu.”

Kwa kuongezea, wazazi fulani wameona kwamba inafaa kufanya utafiti kwenye Intaneti kuhusu sinema. Kuna vituo vingi vya Intaneti vinavyotoa habari nyingi kuhusu filamu. Habari hizo zinaweza kutumiwa kuelewa vizuri mambo yanayokaziwa na sinema fulani.

Manufaa ya Dhamiri Iliyozoezwa

Biblia huzungumza kuhusu wale ambao “nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Waebrania 5:14) Kwa hiyo, lengo la wazazi linapaswa kuwa kukazia viwango ambavyo vitawasaidia watoto wao kufanya maamuzi yenye hekima watakapokuwa na uhuru wa kuchagua vitumbuizo vyao.

Kuhusiana na jambo hilo, vijana wengi ambao ni Mashahidi wa Yehova wamezoezwa vizuri na wazazi wao. Kwa mfano, Bill na Cherie, wanaoishi Marekani hufurahia kwenda kutazama sinema pamoja na wavulana wao wawili. Bill anasema, “baada ya kutazama sinema hiyo, mara nyingi sisi huzungumza kuhusu filamu hiyo, ilifundisha maadili gani na ikiwa tunakubaliana na maadili hayo au la.” Bila shaka, Bill na Cherie wanatambua umuhimu wa kuwa wateuzi. Bill anasema, “Sisi hufanya uchunguzi kuhusu filamu hiyo kabla ya kuitazama, na hatuoni aibu kutoka kwenye jumba la sinema ikiwa kuna jambo lisilofaa ambalo hatukuwa tumetarajia.” Kwa kuwahusisha watoto wao kufanya maamuzi mazito, Bill na Cherie wanahisi kwamba wanawasaidia wana wao kusitawisha mtazamo unaofaa kuhusu mema na mabaya. Bill anasema, “wanafanya maamuzi ya hekima zaidi wanapochagua filamu watakazotazama.”

Kama Bill na Cherie, wazazi wengi wamewasaidia watoto wao kuzoeza nguvu zao za ufahamu kuhusiana na vitumbuizo. Ni kweli kwamba sinema nyingi ambazo watayarishaji wa filamu hutokeza hazifai. Kwa upande mwingine, wanapoongozwa na kanuni za Biblia, Wakristo wanaweza kufurahia vitumbuizo vinavyofaa na kuburudisha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Nchi nyingi ulimwenguni zina mfumo kama huo ambao alama fulani hutiwa kuonyesha sinema fulani inapaswa kutazamwa na watu wa umri fulani.

^ fu. 12 Kwa kuongezea, huenda viwango vya sinema vikatofautiana katika nchi mbalimbali. Huenda sinema inayoonwa kuwa haiwafai vijana katika nchi moja ikaonekana kuwa inafaa katika nchi nyingine.

^ fu. 16 Wakristo wanapaswa pia kukumbuka kwamba huenda sinema za watoto na vijana zikawa na mambo yanayohusiana na uchawi, kuwasiliana na pepo, au mambo mengine ya kishetani.—1 Wakorintho 10:21.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12]

‘SISI HUFANYA MAAMUZI PAMOJA’

“Nilipokuwa mdogo, tulienda kwenye sinema tukiwa familia. Kwa kuwa sasa nina umri mkubwa, ninaruhusiwa kwenda peke yangu. Hata hivyo, kabla ya kuniruhusu kwenda, wazazi wangu hutaka kujua kichwa cha filamu hiyo na habari inayozungumziwa. Ikiwa hawajui jambo lolote kuhusu sinema hiyo, wao husoma maoni ya wachambuzi au kutazama sehemu ndogo ya sinema hiyo inapoonyeshwa kwenye televisheni. Pia wao hutafuta habari kuhusu sinema hiyo kwenye Intaneti. Wakihisi kwamba sinema hiyo haifai, wao hutoa sababu. Vilevile wao huniruhusu nitoe maoni yangu. Sisi hujieleza waziwazi na kufanya maamuzi pamoja.—Héloïse, mwenye umri wa miaka 19, anayeishi Ufaransa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 13]

ZUNGUMZIENI MAMBO HAYO!

“Wazazi wakiwakataza watoto wao vitumbuizo fulani na kukosa kuwapa vitumbuizo vinavyofaa, huenda watoto hao wakajaribu kutosheleza tamaa zao kwa siri. Kwa hiyo, watoto wanapotaka kutazama sinema zisizofaa, wazazi fulani hawawakatazi moja kwa moja, wala kuwaruhusu. Badala yake, wao hungoja hali itulie. Bila kukasirika, wao huzungumzia mambo hayo kwa siku kadhaa, wakimwuliza kijana huyo sababu inayofanya ahisi kwamba sinema hiyo inafaa. Wanapozungumzia jambo hilo, mara nyingi vijana hukubaliana na wazazi wao na hata kuwashukuru. Kisha, wakiongozwa na wazazi wao, wao huchagua vitumbuizo vingine wanavyoweza kufurahia pamoja.”—Masaaki, mwangalizi asafiriye huko Japani.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]

TAFRIJA ZA AINA NYINGINE

▪ “Kwa kawaida, vijana hupenda kuwa pamoja na vijana wa rika lao, kwa hiyo sikuzote sisi hupanga binti yetu ashirikiane na watu wanaofaa chini ya usimamizi wetu. Kwa kuwa kutaniko letu lina vijana wengi wenye mfano mzuri, sisi humtia moyo binti yetu afanye urafiki nao.”— Elisa, Italia.

▪ “Sisi hujihusisha sana na tafrija za watoto wetu. Sisi huwapangia tafrija zinazofaa kama vile matembezi, kwenda kwenye karamu za aina mbalimbali pamoja na Wakristo wa umri wote. Kwa kufanya hivyo, watoto wetu hawaoni kwamba lazima wawe na marika wao ndio wafurahie tafrija.”—John, Uingereza.

▪ “Tumeona kwamba kukusanyika pamoja na Wakristo wenzetu huridhisha. Watoto wangu pia hupenda kucheza kandanda, kwa hiyo mara kwa mara sisi hupanga kucheza kandanda pamoja na wengine.”—Juan, Hispania.

▪ “Sisi huwatia moyo watoto wetu wafurahie kucheza ala za muziki. Pia sisi hufanya mambo mengi tunayopenda tukiwa pamoja kama vile kucheza tenisi, voliboli, kuendesha baiskeli, kusoma, na kukutana na marafiki.”—Mark, Uingereza.

▪ “Sisi hucheza kwa ukawaida mchezo wa kuvingirisha matufe tukiwa familia na pamoja na marafiki. Pia mara moja kwa mwezi, sisi hujaribu kupangia jambo fulani la pekee tukiwa familia. Ili kuepuka matatizo, wazazi wanahitaji kuwa waangalifu.”—Danilo, Filipino.

▪ “Kuhudhuria tamasha fulani husisimua zaidi kuliko kuketi tu na kutazama sinema. Sisi hutafuta habari kuhusu tamasha zitakazofanywa katika eneo letu kama vile maonyesho ya sanaa na ya magari, au tamasha za muziki. Kwenye tamasha hizo mara nyingi sisi hupata nafasi ya kuwa na mazungumzo. Pia tunakuwa waangalifu tusipange vitumbuizo vingi kupita kiasi. Kuwa na vitumbuizo vingi hupoteza wakati na pia hufanya visiwe vyenye kusisimua.”—Judith, Afrika Kusini.

▪ “Mimi hujaribu kuwasaidia watoto wangu waelewe kwamba si kila jambo ambalo watoto wengine hufanya linafaa. Wakati huohuo mimi na mume wangu hujaribu kuwapangia vitumbuizo vinavyofaa. Sisi hujaribu kuwafanya wasilalamike na kusema, ‘Hatuendi mahali popote. Hatufanyi jambo lolote.’ Tukiwa familia, sisi huenda kwenye bustani na kuwaalika washiriki wa kutaniko letu nyumbani kwetu.” *—Maria, Brazili.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 47 Kwa habari zaidi kuhusu vikusanyiko vya kirafiki, ona jarida letu lingine, Mnara wa Mlinzi, Agosti 15, 1992, ukurasa wa 15-20.

[Hisani]

James Hall Museum of Transport, Johannesburg, South Africa

[Picha katika ukurasa wa 11]

Chunguza maoni ya wachambuzi wa sinema KABLA ya kuamua

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Wazazi, fundisheni watoto wenu kuwa wateuzi