Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Ni Hatari Kuchumbiana Kwenye Intaneti?

Je, Kweli Ni Hatari Kuchumbiana Kwenye Intaneti?

Vijana Huuliza . . .

Je, Kweli Ni Hatari Kuchumbiana Kwenye Intaneti?

“Kwenye Intaneti huwezi kujua kabisa unawasiliana na nani.”—Dan, 17. *

“Kwenye Intaneti watu wanaweza kudanganya. Ni rahisi kujifanya jinsi usivyo kwa kweli.”—George, 26.

ULIMWENGUNI kote kuchumbiana kupitia Intaneti kunazidi kuwa maarufu. Kama makala ya kwanza katika mfululizo huu ilivyoonyesha, uchumba unaofanywa kupitia Intaneti unaweza kusitawi haraka lakini mara nyingi unakwisha haraka wakati watu hao wanapojuana kikweli. * Hata hivyo, kukatishwa tamaa silo jambo pekee linalohangaisha. Kufanya uchumba kupitia Intaneti kunaweza kutokeza madhara makubwa zaidi, kimwili, kihisia, au hata kiroho.

Kompyuta iliyo ndani ya nyumba yako, inayoonekana kuwa salama na isiyoweza kutokeza madhara, inawezaje kuwa hatari? Baadhi ya hatari zinahusiana na kanuni fulani muhimu ya Biblia. Mtume Paulo aliandika hivi: “Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Hilo halimaanishi kwamba kutumia Intaneti si jambo la unyoofu wala haimaanishi utaacha kuwa mnyoofu ukitumia Intaneti. Hata hivyo, tunapaswa kutambua kwamba watu wengine si wanyoofu nyakati zote na kama maelezo yaliyonukuliwa mwanzoni mwa makala hii yanavyoonyesha, Intaneti hufanya iwe rahisi kuendeleza udanganyifu wa aina fulani na isiwe rahisi kutambuliwa. Na uhusiano wa kimahaba unapohusika, udanganyifu unaweza kuleta hatari kubwa sana.

Kwa mfano, ona aina ya udanganyifu unaofafanuliwa katika mstari huu wa Biblia: “Sikuketi na watu wasiosema kweli; wala siingii pamoja na wale wanaoficha jinsi walivyo.” (Zaburi 26:4) Ni nini kinachomaanishwa na “wale wanaoficha jinsi walivyo”? Tafsiri fulani za Biblia husema “wanafiki.” Kitabu kimoja cha marejeo kinaeleza kuwa maneno hayo yanaweza kutumika kwa “wale wanaoficha wengine makusudi yao, au wanaoficha utu wao na nia yao.” Udanganyifu huo hufanywaje katika Intaneti? Na ni hatari zipi zinazotokezwa kwa wale wanaotafuta mahaba?

Mbwa-mwitu Katika Mavazi ya Kondoo

Baba anayeitwa Michael alishtuka kujifunza katika semina fulani kuwa watoto wengi hawatii sheria za wazazi wao kuhusu kutochunguza vituo hatari vya Intaneti. Anasema hivi: “Jambo lililoniogopesha hata zaidi ni kujua kwamba watu wanaofanya ngono na watoto wanaweza kutumia Intaneti kuwashawishi watoto wadogo wafanye ngono zisizofaa.” Vijana wanapotumia Intaneti kukutana na watu wasiowajua, wanaweza kukabili hatari kubwa kuliko wanavyofikiri.

Kumekuwa na ripoti za habari kuhusu watu wazima wanaotaka kufanya ngono na vijana ambao hujifanya kuwa vijana na kuwavizia kwa kutumia Intaneti. Kulingana na uchunguzi mmoja, “kijana mmoja kati ya watano wanaotumia Intaneti ameombwa afanye ngono.” Gazeti moja pia lilisema kwamba mtoto 1 kati ya 33 aliye na umri kati ya miaka 10 na 17 “alisumbuliwa isivyofaa” kupitia mazungumzo ya kompyuta.

Vijana wengine wameshangaa kugundua kwamba “kijana” waliyekuwa wakisitawisha uhusiano wa kimahaba naye kwenye Intaneti alikuwa mfungwa aliye mtu mzima. Bila kujua vijana wengine wamejihusisha na watu wanaowavizia kingono. Kwanza watu hao waovu “huwatayarisha” wale watakaowakamata, na kuwafanya wawatumaini kupitia mazungumzo ya kirafiki kwenye Intaneti. Lakini muda unapopita wao hujaribu kukutana na mtu huyo ili watimize tamaa zao zilizopotoka. Kwa kuhuzunisha, vijana wamepigwa, wakanajisiwa, na hata kuuawa kwa sababu ya hilo.

Kwa kweli, watu waovu ‘huficha jinsi walivyo’ ili wapate watu wa kuwadhulumu kwenye Intaneti. Watu hao wanaovizia wanaweza kukukumbusha mfano wa Yesu kuhusu manabii wa uwongo ambao “wanakuja kwenu katika mavazi ya kondoo” lakini kwa kweli wao ni kama “mbwa-mwitu wenye kunyafua.” (Mathayo 7:15) Mtu anaweza kujificha kabisa anapowasiliana kupitia Intaneti hivi kwamba inaweza kuwa vigumu sana kutambua kwamba anakudanganya. George, aliyetajwa awali anasema hivi: “Unapozungumza na mtu uso kwa uso unaweza kujifunza mambo kutokana na ishara zake za uso na kupitia sauti yake. Lakini katika Intaneti huwezi kujua mambo hayo. Ni rahisi kudanganywa.”

Kwa kweli, shauri hili la Biblia ni lenye hekima: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha, lakini wasio na uzoefu wameendelea mbele nao lazima waumie.” (Methali 22:3) Si watu wote unaowasiliana nao kwenye Intaneti walio wabaya. Hata hivyo, kuna njia nyingine ambayo watu hutumia ili ‘kuficha jinsi walivyo.’

Hatari za Kudanganya na Kuweka Siri

Haishangazi kwamba ni jambo la kawaida kati ya watu wanaotafuta mahaba kwenye Intaneti kutilia chumvi au kujifanya kuwa wana sifa nzuri na kuficha kasoro nzito. Kwa kuongezea, gazeti The Washington Post lilinukuu maneno ya mwandishi fulani aliyesema: “Linaweza kuwa jambo baya kuchumbiana kupitia Intaneti kwa kuwa watu hudanganywa.” Linaongeza hivi: “Mara nyingi watu hujifanya kuwa wa jinsia nyingine. . . . Mapato yao, . . . jamii, rekodi za uhalifu, rekodi kuhusu matatizo ya akili na ikiwa wamefunga ndoa hazifunuliwi kwa muda mrefu kadiri uhusiano huo unavyoendelea.” Ili kuwaonya watu, wengi wameripoti jinsi walivyojikuta katika hali zenye kuhuzunisha kwa sababu ya kudanganywa na watu waliokutana nao kwenye Intaneti.

Je, watu wanaweza kudanganya kuhusu jambo muhimu kama vile hali yao ya kiroho? Kwa kuhuzunisha, ndiyo. Wengine hudai kuwa Wakristo wa kweli na kumbe sivyo ilivyo. Kwa nini wadanganye? Kwa mara nyingine tena, ni kwa sababu Intaneti hufanya iwe rahisi kwao kudanganya. Kijana mmoja huko Ireland, anayeitwa Sean, anakubali kwamba, “Ni rahisi sana kudanganya unapotumia kompyuta.”

Watu wengi hawaoni hilo kuwa jambo zito kwani wao husema ni kawaida mtu kudanganya kidogo anapoanza uchumba. Lakini, kumbuka kwamba Mungu huchukia uwongo. (Methali 6:16-19) Naye ana sababu nzuri ya kuuchukia. Uchungu na huzuni nyingi iliyopo ulimwenguni hutokana na kusema uwongo. (Yohana 8:44) Uwongo ndio msingi mbaya zaidi wa kuanza uhusiano, hasa uhusiano unaofikiriwa kuendelea kwa muda mrefu. Jambo baya hata zaidi ni kwamba kusema uwongo huharibu uhusiano wa mtu na Yehova Mungu.

Jambo la kusikitisha ni kwamba vijana wengine wamehusika katika aina nyingine ya udanganyifu. Wamefanya uchumba kupitia Intaneti na wamewaficha wazazi wao jambo hilo. Kwa mfano, wazazi wa kijana mmoja walishangaa wakati msichana fulani ambaye hakuwa na imani moja na familia yao alipowasili nyumbani kwao baada ya kusafiri zaidi ya kilometa 1,500. Mwana wao alikuwa akimchumbia kwenye Intaneti kwa miezi sita, lakini hawakujua jambo lolote kuhusu uchumba huo hadi msichana huyo alipofika!

Wazazi hao walijiuliza, “Hilo linawezekanaje?” Walijiambia kwamba, ‘Mwana wetu hangeweza kupendezwa na mtu ambaye hajawahi kukutana naye.’ Lakini kwa kweli, alikuwa akiwadanganya, yaani, akificha jinsi alivyo kwa kweli. Je, hukubali kwamba uwongo kama huo ni msingi mbaya wa uchumba?

Afadhali Mtu Unayemfahamu Kuliko Unayemwazia

Kufanya uchumba kupitia Intaneti kunaweza kutokeza hatari nyingine. Katika hali fulani, mtu unayezungumza naye kwenye Intaneti anaweza kuonekana kuwa halisi zaidi kuliko watu unaowaona kila siku. Familia, marafiki, na madaraka yako yanaweza kukosa umuhimu. Msichana mmoja anayeitwa Monika, huko Austria anasema: “Nilianza kupuuza mahusiano muhimu kwa sababu nilitumia wakati mwingi kwenye kompyuta na watu niliokutana nao kwenye Intaneti.” Alipogundua jambo hilo, alisikitishwa na kuamua kuacha kutumia njia hiyo ya kuwasiliana.

Bila shaka, watu wengi hutumia Intaneti kwa usawaziko. Kutuma barua pepe kunaweza kuwa njia muhimu sana ya kuwasiliana na marafiki na wapendwa wetu. Lakini utakubali kwamba kuwasiliana uso kwa uso ndiyo njia bora zaidi. Ikiwa “umepita upeo wa ujana,” yaani, wakati ambapo tamaa za ngono huwa nyingi, na unataka kufunga ndoa, basi unakabili mojawapo ya maamuzi muhimu zaidi maishani. (1 Wakorintho 7:36) Kwa hiyo, fanya uamuzi kwa uangalifu.

Biblia hutoa shauri hili: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.” (Methali 14:15) Badala ya kuamini mambo yote ambayo unaandikiwa na mtu ambaye hujawahi kukutana naye, fikiria hatua zako kwa uangalifu. Ni jambo la hekima zaidi kukutana na kufanya urafiki na mtu uso kwa uso. Chunguza ikiwa kweli mnapatana, hasa kuhusiana na miradi yenu ya kiroho na maadili. Uchumba wa aina hiyo unaweza kuongoza kwenye ndoa yenye furaha kwelikweli.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina fulani yamebadilishwa.

^ fu. 5 Ona makala yenye kichwa “Vijana Huuliza . . . ‘Je, Nitafute Mchumba Kwenye Intaneti?’” katika toleo la Amkeni! la Aprili 22, 2005.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Je, kweli unajua ni nani unayewasiliana naye kwenye Intaneti?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Unapofanya uchumba, jambo bora zaidi ni kuwasiliana uso kwa uso