Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kujifunza Mimi ni mwalimu, na nimemaliza tu kusoma makala zenye kichwa, “Vijana na Wazee Mnaweza Kufurahia Kujifunza.” (Agosti 8, 2004) Mara nyingi mimi hutaka kujua jinsi mnavyoandika makala zilizo sahihi, wazi, na zinazofaa sana. Kwa kweli, mimi huvutiwa na bidii yenu ya kuwatia moyo watu wa umri wote wajifunze.

F. S., Italia

Nilipokuwa katikati ya masomo yangu ya sekondari, nilichukizwa sana na shule hivi kwamba wazazi wangu waliniruhusu nijifunze mwenyewe nyumbani. Sasa nina umri wa miaka 20, na ninafurahia kujifunza tena. Kusoma makala hizo ni kikumbusho kwamba watu wote wanaweza kujifunza, hata hali zao ziweje.

N. G., Marekani

Ninasumbuliwa na mwana wangu mkubwa, ambaye ana umri wa miaka saba. Hapendi kusoma vitabu, kufanya kazi ya shule, na kujifunza katika mikutano ya Kikristo. Ninanuia kutumia mashauri yaliyo katika makala hizo.

M. O., Japani

Kati ya mambo yaliyopendekezwa katika makala hiyo ni kufanya pitio fupi baada ya kujifunza, kwa kuwa ni jambo la kawaida kusahau mambo ambayo umetoka tu kujifunza. Mimi na mke wangu tunajifunza Kihindi ili tuwahubirie Wahindi wanaoishi katika eneo letu. Mimi huona inanufaisha kuandika maneno mapya kwenye karatasi. Baadaye, ninapopata nafasi, mimi huangalia maneno hayo. Hilo hunisaidia kukumbuka mambo ambayo nimejifunza.

E. T., Marekani

Nina umri wa miaka 56, na kikundi cha lugha ya ishara kilianzishwa katika kutaniko letu. Ingawa sina uwezo mkubwa, nilijiunga na kikundi hicho kwa sababu nilitaka kusaidia. Nilipokuwa nikijiuliza kama nitaweza kujifunza lugha hiyo, nilisoma mfululizo huo. Nilitiwa moyo sana na habari iliyo chini ya kichwa kidogo, “Hata Wazee Wanaweza Kujifunza” na pia makala ya mwisho. Nilipata ujasiri tena wa kuendelea kulingana na uwezo wangu na kushirikiana na kikundi cha lugha ya ishara.

R. N., Japani

Magazeti Maridadi Niliona makala yenye kichwa, “Magazeti Yanayowavutia Watu” kuwa yenye kuchochea fikira! (Agosti 8, 2004) Sikujua jinsi magazeti hayo yanavyoweza kumwathiri mtu. Nilifurahia ile hoja ya kwamba kumwona mtu bila kukutana naye kunaweza kuathiri hisia za watu wakati mtu ambaye hawajakutana naye anapokufa. Pindi moja niliathiriwa kwa njia hiyo! Sasa binti yangu anapendezwa na magazeti fulani. Nitazungumzia makala hiyo pamoja naye.

S. M., Marekani

Sura Ningependa kuwashukuru kwa makala, “Kuhangaikia Sura Kupita Kiasi.” (Julai 22, 2004) Ni kana kwamba makala hiyo iliandikwa kwa ajili yangu. Nina umri wa miaka 19, na jambo la kusikitisha ni kwamba, nimekuwa na matatizo ya kula kwa muda mrefu. Si rahisi kutibu ugonjwa huo. Asanteni kwa makala zinazozungumzia habari kama hizo. Makala hizo hufanya nifikirie jambo hilo kwa uzito, na ninatumaini kwamba zitanisaidia kutatua tatizo langu.

G. L., Italia

Fumbo la Maneno Asanteni sana kwa makala nzuri zenye mafumbo ya maneno. Makala hizo hunisaidia kumjua Yehova Mungu na Biblia vizuri zaidi. Nina umri wa miaka tisa.

I. C., Ujerumani

“Amkeni!” linajibu: Maswali ya Biblia, “Je, Wajua?” huchapishwa katika matoleo ya lugha fulani za “Amkeni!” ambayo hayana fumbo la maneno.