Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuacha Kuiba Vitu Dukani

Jinsi ya Kuacha Kuiba Vitu Dukani

Jinsi ya Kuacha Kuiba Vitu Dukani

“Kupunguza wizi si tatizo lako peke yako, ni tatizo la jamii nzima; kila mtu hunufaika wizi unapokomeshwa.”—“EVERY RETAILER’S GUIDE TO LOSS PREVENTION.”

KAMA mazoea mengine mabaya, kuiba vitu dukani huathiri jinsi mtu anavyofikiri na kumfanya ajitetee. Kwa hiyo, kama vile mkulima hung’oa magugu pamoja na mizizi yake, yeyote anayetaka kuacha zoea la kuiba vitu dukani anapaswa kung’oa mawazo mabaya. Kwenye Waroma 12:2, Biblia inatushauri ‘tufanye upya akili yetu.’ Nalo andiko la 1 Petro 1:14 linatuhimiza hivi: “Acheni kufanyizwa kulingana na tamaa mlizokuwa nazo hapo zamani.” Mambo matano yafuatayo yanaweza kumsaidia mtu ambaye huiba vitu dukani abadili akili yake kuhusu kuiba.

Misaada ya Kurekebisha Kufikiri Kwetu

▪ Kwanza, ni kinyume cha sheria kuiba vitu dukani. Kuiba kunaweza kuwa jambo la kawaida mahali ambapo mtu anaishi, na huenda asikamatwe; lakini bado mtu anayeiba vitu dukani anavunja sheria.—Waroma 13:1.

Ni nini hutokea watu wengi wanapovunja sheria? Kulingana na Biblia, “sheria hufa ganzi.” (Habakuki 1:3, 4) Yaani, manufaa inayotokana na sheria zilizowekwa hupotea, na utengemano hukosekana katika jamii. Kila wakati mtu anapoiba vitu dukani, anadhoofisha msingi wa jamii inayotii sheria. Hilo linapotokea, kila mtu huumia.

▪ Pili, kuiba vitu dukani hufanya watu wakose kutumainiana. Mazoea hayo yasiyo ya unyoofu huharibu mahusiano ya kibinadamu na kufanya iwe vigumu kwa watu kuelewana na kutendeana kwa haki.—Methali 16:28.

“Udhaifu wangu mkubwa ni kuwatumaini watu kupita kiasi.” Ndivyo alivyosema mtu mmoja mwenye duka la nguo baada ya wezi kumfilisi. Aliamini kwamba wateja na wafanyakazi wake hawawezi kumwibia. Sasa anahisi kwamba hakupaswa kuwatumaini watu hao.

Mtu anapomdanganya mwingine, hilo hupunguza heshima ambayo mwenzake humpa. Lakini wezi hufanya wenye duka wamshuku kila mtu anayeingia katika duka lao. Hufanya watu wanyoofu washukiwe kuwa wezi. Hakuna mtu anayepaswa kufanya hivyo.

▪ Tatu, zoea la kuiba vitu dukani linaweza kumfanya mtu atende uhalifu mkubwa zaidi. Baada ya muda, huenda watu wanaoiba vitu dukani wakafanya mambo mabaya zaidi.—2 Timotheo 3:13.

Mwisho wa Kuiba Vitu Dukani

▪ Jambo la nne lililo muhimu zaidi ni kwamba mtu anayeiba vitu dukani anapingana na Mungu Mweza Yote. Neno lake humwambia mwizi “asiibe tena,” nalo huonya kuhusu hukumu dhidi ya wale wanaokosa kumtii. (Waefeso 4:28; Zaburi 37:9, 17, 20) Lakini Yehova huwasamehe wezi wanaojirekebisha. Wanaweza kuwa na amani pamoja na Mungu.—Methali 1:33.

▪ Tano, kama uhalifu wote mwingine, hivi karibuni kuiba vitu dukani kutakomeshwa. Kama Biblia inavyoahidi, Ufalme wa Mungu utakapotawala dunia kwa ukamili, wanadamu watatendeana kwa utimilifu na kwa unyoofu. Hilo litakomesha madhara yanayosababishwa na kuiba vitu dukani.—Methali 2:21, 22; Mika 4:4.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

NJIA RAHISI ZA KUZUIA WIZI

Huenda watu fulani wenye biashara ndogo wasiwe na uwezo wa kununua mifumo ghali ya ulinzi. Lakini hilo halimaanishi kwamba hawawezi kukabiliana na watu wanaoiba vitu dukani. Mara nyingi, wafanyabiashara wanaweza kulinda bidhaa zao kwa kuchukua hatua fulani rahisi.

Katika kichapo walichoandika pamoja, wapelelezi Michael Brough na Derek Brown wanakazia uhitaji wa kuwatazama wateja kwa makini: “Mtazame kila mtu. . . . Wewe na wafanyakazi wako ndio mnaoweza kulinda vitu kwa njia bora zaidi.” Wanapendekeza umwendee mtu unayeshuku kwamba ameiba na kumwambia hivi: “Je, umepata kitu ulichokuwa unatafuta? Tafadhali kipeleke kwa keshia, naye atakuambia bei yake.” “Ungependa nikufungie kitu hicho?” “Je, fulana hiyo inakutoshea?” “Ungependa nikupe kikapu?” Wapelelezi hao wanasema: “Hilo hufanya wateja wanyoofu na vilevile wezi watambue kwamba umewaona na kwamba unapendezwa nao.”

Wanasema hivi kuhusu kupanga vitu: “Hakikisha bidhaa zimejaa na zimepangwa vizuri kila wakati. Kuchunguza bidhaa mara nyingi kutafanya uzifahamu vizuri, na zinapopangwa vizuri inakuwa rahisi zaidi kugundua ikiwa kitu fulani kimeguswa au kuondolewa.”—Every Retailer’s Guide to Loss Prevention.

Kachero Russell Bintliff anadokeza: “Safu zisizokuwa na vizuizi na rafu zilizojaa zitawasaidia wafanyakazi kuona kile ambacho wateja wanafanya. Mfanyakazi anapotembea kwenye safu ambapo mtu fulani anashukiwa kuwa mwizi, anaweza kutambua ni nini kinachokosekana, kisha anaweza kujifanya kwamba anaangalia bidhaa na kuona ni nini kiko ndani ya kikapu cha mteja. . . . Watu wanaoiba vitu watajua ni nini kinachoendelea; lakini mteja mnyoofu hatatambua kwamba mfanyakazi huyo anamtazama.” Anasema hivi kuhusu mpangilio wa safu: “Safu zinapaswa kupangwa katika njia ambayo [mwenye duka] pamoja na wafanyakazi wanaweza kuona wateja wanafanya nini.”—Crimeproofing Your Business—301 Low-Cost, No-Cost Ways to Protect Your Office, Store, or Business.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Unyoofu hufanya watu watumainiane na wawe marafiki