Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Ubaguzi Asanteni kwa mfululizo wenye kichwa, “Je, Ubaguzi Utakwisha?” (Septemba 8, 2004) Nilipokuwa nikisoma makala hizo, nilitambua kwamba kwa kiasi fulani mimi mwenyewe nina ubaguzi. Jambo hilo lilinishangaza kwa sababu mara nyingi mimi hukasirishwa na watu wenye ubaguzi. Ninajua kwamba gazeti hilo litanisaidia.

M. U., Marekani

Ingawa ninaishi mbali na nchi nilikozaliwa, mimi sihisi kwamba ninabaguliwa. Lakini makala hizo zilinisaidia kuwahurumia wale wanaobaguliwa. Tunafurahi kwamba hivi karibuni Yehova atakomesha tatizo hilo!

T. G., Norway

Ninawapongeza kwa nia yenu ya kuwafanya watu wafikirie tatizo la ubaguzi. Hata hivyo, nafikiri kwamba hata ninyi mlionyesha ubaguzi kwenye ukurasa wa 8 na 9. Katika kurasa hizo mlieleza kuhusu wapita-njia wawili Wayahudi ambao hawakutaka kumsaidia mtu aliyejeruhiwa. Kwa nini mlichagua Wayahudi?

H. H., Marekani

“Amkeni!” linajibu: Hadithi hiyo kuhusu Msamaria mwenye ujirani ilisimuliwa na Yesu, ambaye alikuwa Myahudi. Katika siku za Yesu, Wayahudi wengi waliwabagua Wasamaria. Kwa hiyo, kwa kuonyesha kwamba mtu wa kabila lingine angeweza kuwa jirani mwema kwa Myahudi, Yesu alikuwa akiwafundisha wasikilizaji wake Wayahudi somo muhimu sana.

Magonjwa ya Akili Asanteni kwa makala yenye kichwa “Mpendwa Wako Anapokuwa na Ugonjwa wa Akili.” (Septemba 8, 2004) Mama yangu ameugua ugonjwa wa akili kwa miaka mingi. Sasa naelewa kwamba ninapaswa kumtia moyo atafute msaada na hapaswi kuona aibu kufanya hivyo.

M. P., Ukrainia

Nina umri wa miaka 16 tu, lakini nimekuwa na mshuko wa moyo kwa miaka mingi. Asanteni sana kwa kuandika makala hiyo nzuri ambayo imenisaidia sana kukabiliana na nyakati ngumu. Nina hakika kwamba wengine pia watanufaishwa na makala hiyo.

K. J., Ujerumani

Endeleeni kuandika makala kama hizo! Zinatusaidia sisi sote kutambua uhitaji wa kuwa na subira na upendo zaidi na kutafuta msaada tunaohitaji. Tunatamani sana kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu ambao hautakuwa na ugonjwa kama huo wenye kufadhaisha!

K. F., Marekani

Vijana Nina umri wa miaka 15, nami mara nyingi nimewahubiria walimu na wanafunzi wenzangu. Makala hiyo yenye kichwa “Vijana Wanaotetea Imani Yao,” (Septemba 8, 2004) ilisema kweli—kuhubiri shuleni ni ulinzi. Endeleeni kuandika makala hizo nzuri!

R. B., Ujerumani

Paradiso Nilifurahia kusoma makala yenye kichwa “Paradiso Ndogo.” (Septemba 8, 2004) Sikuwa nimewahi kusikia kuhusu wanyama wengi waliotajwa katika makala hiyo. Kuanzia sasa na kuendelea nitajaribu kusoma kila toleo la Amkeni!

W. C., Ufaransa

Asanteni sana kwa makala hiyo. Mara nyingi mimi husafiri tu ndani ya kijiji ninamoishi, lakini kupitia makala za Amkeni! mimi huweza “kusafiri” sehemu za mbali kwa ukawaida. Uzuri wa uumbaji wa Yehova hutustaajabisha na kutukumbusha upendo wake mkubwa.

D. H., Marekani

Kitu Bora Niliguswa moyo sana na simulizi la maisha la Charles Sinutko lililochapishwa katika makala “Kitu Bora Kuliko Umashuhuri wa Ulimwengu.” (Agosti 22, 2004) Ndugu Sinutko aliacha kazi yake, umashuhuri, na mali ili kumtumikia Yehova. Yeye na mke wake waliridhika na maisha rahisi. Imani yao yenye nguvu ilifanya nilie na pia ilinichochea nimtumaini Yehova. Nilitiwa moyo nijitahidi sana katika huduma yangu. Asanteni kwa simulizi hilo la maisha lenye kutia moyo.

I. B., Poland