Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Watu Huiba Vitu Dukani?

Kwa Nini Watu Huiba Vitu Dukani?

Kwa Nini Watu Huiba Vitu Dukani?

“Sioni kuiba vitu dukani kuwa jambo baya. Mimi huona jambo hilo kuwa sawa na kuwagawia wenye uhitaji vitu.”—KASISI WA KANISA LA ANGLIKANA.

IKIWA hekaya husema kweli, Robin Hood hakuona ubaya wowote kuiba. Hekaya za Waingereza zinasema kwamba aliwaibia matajiri ili kuwapa maskini. Kasisi aliyenukuliwa juu pia anaamini kwamba umaskini ni sababu nzuri ya kuiba. Anasema hivi kuhusu watu wanaoiba vitu dukani: “Ninawasikitikia sana, kwa kweli ninafikiri wana sababu nzuri kabisa za kuiba.” Anadokeza kwamba mara moja kwa mwaka, maduka makubwa yanapaswa kuwaruhusu maskini wachukue chochote wanachotaka bila kulipa.

Hata hivyo, wengi huchochewa kuiba vitu dukani na sababu nyingine mbali na umaskini. Nchini Japani, polisi waliwakamata polisi wenzao wawili kwa kuiba vitu dukani. Nchini Marekani, mkurugenzi mmoja wa shirika la chakula lisilo la kibiashara alikamatwa akiiba katika duka la shirika hilo. Mara nyingi matineja wenye pesa huiba vitu wasivyohitaji. Ni nini huwachochea watu hao kuiba?

‘Kunasisimua’

Msisimuko. Woga. Uwezo. Kama wale wasichana wawili waliotajwa katika makala iliyotangulia, watu fulani ambao huiba vitu dukani hupata hisia kama hizo, na tamaa ya kuhisi hivyo huwafanya waibe tena na tena. Baada ya kuiba kwa mara ya kwanza, mwanamke mmoja alisema hivi: “Nilisisimuka. Sikukamatwa na hilo lilinisisimua!” Alisema hivi kuhusu jinsi alivyohisi baada ya kuiba kwa kipindi fulani: “Niliaibika lakini pia nilisisimuka. Nilichangamka kwelikweli. Kuiba na kukosa kukamatwa kulifanya nihisi kuwa na uwezo mkubwa sana.”

Kijana mmoja anayeitwa Hector anasema kwamba baada ya kuacha kuiba vitu dukani kwa miezi kadhaa, alihisi tamaa ya kuiba tena. * “Niliendelea kuhisi hivyo na tamaa hiyo ikawa kama uraibu. Ningetembea madukani na kuona redio kwenye dirisha la duka na kujiambia, ‘Ni rahisi sana kuiba redio hii. Ninaweza kuiiba na nisikamatwe.’”

Wale ambao huiba ili kupata msisimuko hawahitaji vitu wanavyoiba. Gazeti moja la India linasema: “Wanasaikolojia wanasema kwamba watu hao huchochewa na msisimuko wa kufanya mambo waliyokatazwa. . . . Baadhi yao hata hurudisha vitu walivyoiba.”

Sababu Nyingine

Mamilioni ya watu hupatwa na mshuko moyo. Nyakati nyingine watu walioshuka moyo huonyesha dalili hizo kupitia tabia mbaya kama vile kuiba vitu dukani.

Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 14 alilelewa katika familia tajiri isiyo na matatizo. Licha ya hayo, msichana huyo alikata tamaa. Alisema: “Singeweza kuondoa hisia hizo.” Alianza kutumia kileo na dawa za kulevya. Kisha siku moja akakamatwa akiiba dukani. Baadaye alijaribu kujiua mara mbili.

Kijana mwenye tabia nzuri akianza ghafula kuiba vitu dukani, wazazi wanapaswa kufikiria ikiwa ana matatizo ya kihisia. Dakt. Richard MacKenzie, ambaye ni mtaalamu wa magonjwa ya vijana, alisema: “Ninaamini kwamba mtoto wako anapoanza kuonyesha tabia yoyote isiyo ya kawaida unapaswa kufikiria uwezekano wa kwamba ameshuka moyo mpaka uchunguzi uonyeshe sivyo ilivyo.”

Vijana fulani huchochewa na rafiki zao kuiba vitu dukani na huenda wakalazimika kufanya hivyo ili wakubaliwe na rafiki zao. Huenda wengine wakaiba vitu dukani kwa sababu hawana jambo la kufanya. Wezi stadi hujiruzuku kwa kuiba vitu dukani. Hata sababu iwe nini, wezi huiba vitu vyenye thamani ya mamilioni ya dola kutoka madukani kila siku. Lazima mtu fulani alipie vitu hivyo.

[Maelezo ya dnini]

^ fu. 7 Baadhi ya majina katika makala hizi yamebadilishwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 5]

KLEPTOMANIA

Maria anasema hivi: “Tangu nilipokuwa tineja, nimekuwa nikiiba vitu dukani. Tamaa hiyo iliendelea kuwa mbaya zaidi hadi nikaanza kuiba vitu vyenye thamani ya dola 500 hivi kwa siku.

“Sina nia ya kuiba, lakini tamaa ya kufanya hivyo inakuwa yenye nguvu. Kwa kweli ningependa kubadilika.” Kwa kuwa ni vigumu sana kudhibiti tamaa hiyo, Maria anafikiri kwamba ana kleptomania.

Neno “kleptomania” humaanisha “tatizo la akili ambalo humfanya mtu awe na hamu kubwa ya kuiba bila kuwa na nia ya kujifaidi kifedha.” Tatizo hilo si uraibu wa kawaida tu, linatokana na matatizo makubwa sana ya kihisia.

Watu wengine husema kwamba mtu ambaye ana zoea la kuiba ana tatizo hilo, lakini madaktari wanaamini kwamba tatizo hilo la akili si la kawaida. Kulingana na Shirika la Marekani la Magonjwa ya Akili, watu wanaoiba vitu dukani ambao wana tatizo hilo hawafiki asilimia 5. Kwa hiyo, tunahitaji kuwa waangalifu kabla ya kusema kwamba mtu mwenye zoea la kuiba vitu dukani ana tatizo la akili. Huenda kukawa na sababu nyingine zinazomfanya aibe.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Wazazi wanaojali hujitahidi kuelewa sababu ambayo hufanya mtoto aibe vitu dukani