Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Naazimia Kufikia Mradi Wangu

Naazimia Kufikia Mradi Wangu

Naazimia Kufikia Mradi Wangu

SIMULIZI LA MARTHA CHÁVEZ SERNA

Siku moja nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilipoteza fahamu nilipokuwa nikifanya kazi nyumbani. Niliporudiwa na fahamu, nilijikuta kitandani. Nikiwa nimechanganyikiwa na kuumwa sana na kichwa, singeweza kuona au kusikia kwa dakika kadhaa. Niliogopa sana. Nilikuwa nimepatwa na nini?

WAKIWA na wasiwasi, wazazi wangu walinipeleka kwa daktari, ambaye alipendekeza nitumie vidonge vya vitamini. Alisema kwamba nilizimia kwa sababu ya kukosa usingizi. Miezi kadhaa baadaye, nilizimia tena mara mbili. Tulimwona daktari mwingine, ambaye alidhani kwamba nina tatizo la neva na akanipa dawa za kutuliza akili.

Hata hivyo, niliendelea kuzimia mara nyingi sana. Ningepoteza fahamu kisha ningeanguka na kujiumiza. Nyakati nyingine nilijiuma ulimi na pia ndani ya mdomo. Niliporudiwa na fahamu, niliumwa sana na kichwa na kuhisi kichefuchefu. Mwili wangu wote ulikuwa na maumivu, na mara nyingi sikuweza kukumbuka kilichotokea kabla ya kuzimia. Ili nipate nafuu, ilinibidi kupumzika kitandani kwa siku moja au mbili. Hata hivyo, nilidhani kwamba tatizo hilo lilikuwa la muda tu nami ningepona baada ya muda.

Miradi Yangu Yaathiriwa

Nilipokuwa mchanga, familia yetu ilianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Tulifunzwa na wenzi waliokuwa mapainia wa pekee, au wahudumu wa wakati wote ambao hutumia saa nyingi kila mwezi kuwafundisha watu kweli za Biblia. Niliona kwamba huduma ya mapainia hao iliwafanya wawe na shangwe. Nilipozungumza na mwalimu na wanafunzi wenzangu kuhusu ahadi za Biblia, nilianza kuwa na shangwe pia.

Muda mfupi baadaye, washiriki wengi wa familia yetu wakawa Mashahidi wa Yehova. Nilifurahia sana kuhubiri habari njema. Kufikia wakati nilipokuwa na umri wa miaka saba, nilikuwa nimeweka mradi wa kuwa painia wa pekee. Nilipokuwa na umri wa miaka 16, nilibatizwa na hivyo kuchukua hatua kubwa ili kutimiza mradi huo. Kisha nikaanza kuzimia tena.

Utumishi wa Painia

Licha ya matatizo yangu ya afya, nilihisi kwamba ningeweza kuwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova. Lakini kwa kuwa nilikuwa nikizimia mara mbili hivi kwa juma, wengine kutanikoni walionelea kwamba sipaswi kuchukua daraka hilo zito. Nilihuzunika na kuvunjika moyo. Hata hivyo, baada ya muda, wenzi wa ndoa waliokuwa wakitumika katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Mexico walihamia kutaniko letu. Walisikia kuhusu tamaa yangu ya kuwa painia na wakanitia moyo sana. Walinisadikisha kwamba ugonjwa wangu haupaswi kunizuia kufanya upainia.

Kwa hiyo, Septemba 1, 1988, niliwekwa rasmi kuwa painia wa kawaida katika mji wa kwetu wa San Andrés Chiautla, Mexico. Nilihubiri habari njema kwa saa nyingi kila mwezi. Wakati ambapo sikuweza kwenda mahubiri kwa sababu ya kuzimia, niliandikia watu walioishi katika eneo hilo barua zilizokuwa na habari za Biblia na hivyo kuwatia moyo wajifunze Biblia.

Ugonjwa Wangu Wagunduliwa

Wakati huo wazazi wangu walitumia pesa nyingi sana kunipeleka kwa mtaalamu wa mfumo wa neva. Aliponifanyia uchunguzi, daktari huyo aligundua kwamba nina kifafa. Kwa sababu ya matibabu niliyopokea wakati huo, hali yangu ilitulia. Wakati huohuo, niliweza kuhudhuria Shule ya Utumishi wa Painia, nami nikapata kitia moyo kilichochochea tamaa yangu ya kuhubiri maeneo ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa wa wahubiri.

Wazazi wangu walijua jinsi nilivyotamani kupanua huduma yangu. Kwa kuwa ugonjwa wangu ulikuwa umetulia kwa kiasi fulani, waliniruhusu kwenda Zitácuaro, katika Jimbo la Michoacán, mji uliokuwa kilometa 200 hivi kutoka nyumbani. Kushirikiana na mapainia wengine katika mgawo huo kulinisaidia nithamini hata zaidi utumishi wa wakati wote.

Hata hivyo, baada ya kukaa Zitácuaro kwa miaka miwili, nilianza kuzimia tena. Nikiwa nimefadhaika na kuhuzunika, nilirudi kwa wazazi wangu ili kupata matibabu. Nilimwona mtaalamu wa mfumo wa neva ambaye aligundua kwamba dawa nilizokuwa nikitumia zilikuwa zikiharibu ini langu. Nilianza kutafuta matibabu mengine kwa kuwa hatungeweza tena kumlipa mtaalamu huyo. Hali yangu ilikuwa inazorota, ikabidi niache upainia. Kila mara nilipozimia, nilivunjika moyo. Lakini niliposoma Zaburi na kusali kwa Yehova, nilifarijika na kuhisi nguvu zake.—Zaburi 94:17-19.

Nafikia Mradi Wangu

Hali yangu ilipokuwa mbaya sana, nilizimia mara mbili kwa siku. Kisha kukawa na mabadiliko makubwa. Daktari fulani alinipa matibabu hususa ya kifafa, nami nikaanza kuhisi nafuu kwa vipindi virefu zaidi. Kwa hiyo, Septemba 1, 1995, nilianza upainia tena. Afya yangu iliendelea kuwa nzuri, hivyo baada ya kukaa miaka miwili bila kupata kifafa, nikajaza ombi la kuwa painia wa pekee. Hilo lilimaanisha kwamba ningetumia wakati mwingi zaidi katika huduma na kutumika mahali popote nilipohitajika. Wazia furaha yangu nilipowekwa rasmi kuwa painia wa pekee! Nilifikia mradi nilioweka nikiwa mtoto.

Katika Aprili 1, 2001, nilianza mgawo wangu mpya katika kijiji kidogo kwenye milima ya Jimbo la Hidalgo. Sasa ninatumika katika mji mdogo kwenye Jimbo la Guanajuato. Lazima nitumie dawa kwa ukawaida na kupumzika vya kutosha. Mimi huwa mwangalifu kuhusu vyakula ninavyotumia, hasa mafuta, kafeini, na vyakula vya mikebe. Pia, mimi hujaribu kuepuka kuonyesha hisia nyingi, kama vile hasira au kuwa na wasiwasi kupita kiasi. Lakini nimenufaika kwa kuwa mwangalifu. Nimepata kifafa mara moja tu nikiwa painia wa pekee.

Kwa kuwa mimi bado ni mseja na sina madaraka ya familia, ninafurahia kutumika nikiwa painia wa pekee. Ninafarijika kujua kwamba ‘Yehova hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yetu na upendo tunaoonyesha kwa ajili ya jina lake.’ Yeye ni mwenye upendo sana kwa kuwa hatarajii tumpe mengi kuliko yale tunayoweza. Kukubali ukweli huo kumefanya niwe na maoni yaliyosawazika, kwa kuwa ikiwa afya mbaya itafanya niache upainia tena, ninajua kwamba bado Yehova atapendezwa na utumishi wangu wa nafsi yote.—Waebrania 6:10; Wakolosai 3:23.

Bila shaka, kuwaeleza wengine kuhusu imani yangu kila siku huniimarisha. Pia hunifanya nikazie akilini baraka za wakati ujao ambazo Mungu ametuahidi. Biblia inaahidi kwamba katika ulimwengu mpya, hakutakuwa na magonjwa, “wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani [yatakuwa] yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4; Isaya 33:24; 2 Petro 3:13.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Nikiwa na umri wa miaka 7 hivi (juu); nikiwa na umri wa miaka 16 hivi muda mfupi baada ya kubatizwa

[Picha katika ukurasa wa 27]

Nikihubiri pamoja na rafiki