Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimtendeeje Msichana Anayependezwa Nami?

Nimtendeeje Msichana Anayependezwa Nami?

Vijana Huuliza . . .

Nimtendeeje Msichana Anayependezwa Nami?

“Susan alichukua hatua ya kwanza, nami sikuona ubaya wowote. Kufanya hivyo kulinifaidi.”—James. *

“Ikiwa mwanamume anatenda kwa hila anaposhughulika na wanawake, hilo linaweza kutokeza madhara makubwa.”—Roberto.

HIVI majuzi msichana mmoja alikuambia angependa kukuuliza swali. Mmekuwa pamoja mara nyingi mkiwa na marafiki, na inafurahisha kuzungumza na kufanya mambo pamoja naye. Lakini jambo alilotaja limekushtua. Angependa mwanze uchumba na angetaka kujua ikiwa wewe unahisi hivyo.

Unaweza kushangazwa na hilo ikiwa unafikiri mwanamume ndiye anayepaswa kuanzisha uchumba. Ingawa mara nyingi inakuwa hivyo, kumbuka kuwa hakuvunja kanuni za Biblia kwa kufanya hivyo. * Kukumbuka hilo kutakusaidia ujibu kwa njia inayofaa.

Baada ya kufikiria jambo hilo, huenda ukaamua kwamba wewe ni mchanga kuanzisha uchumba au sasa hivi msichana huyo hakupendezi. Huenda pia ukahisi una hatia na kuwazia kwamba labda ulimwonyesha kuwa unapendezwa naye kwa njia fulani. Unapaswa kufanya nini? Kwanza, unapaswa kufikiria jinsi atakavyohisi.

Fikiria Hisia Zake

Fikiri jinsi msichana huhisi anapokuwa katika hali hiyo. Kwa kuwa anataka sana kukuvutia, huenda ametayarisha kwa siku nyingi maneno atakayosema. Baada ya kufikiria vizuri maneno atakayosema na tabasamu inayofaa, huenda amefikiria uwezekano wa wewe kumkataa. Mwishowe, baada ya kujipa ujasiri, alishinda wasiwasi na kukuambia yaliyo moyoni mwake.

Kwa nini alijitesa hivyo? Labda upendo umempumbaza. Au huenda amevutiwa na sifa zako nzuri ambazo wengine hawaoni. Labda anakusifu kwa njia isiyo ya moja kwa moja, jambo ambalo kwa kawaida wengine hawafanyi.

Tunataja mambo hayo, si ili tukuamulie, bali ili kukukumbusha umuhimu wa kutenda kwa fadhili. Msichana anayeitwa Julie anasema: “Hata ingawa huenda mwanamume asivutiwe na msichana huyo, anapaswa kufurahi kwamba mtu fulani amependezwa naye. Kwa hiyo, badala ya kusema tu hapana, anapaswa kumtendea kwa wororo.” Acha tufikirie kifupi kwamba unataka kufanya hivyo, yaani, “kumtendea kwa wororo,” au kumwambia humtaki kwa wororo.

Vipi ikiwa ulimkataa wakati uliopita? Huenda ukahisi kuwa wakati huu unapaswa kumwambia kwa ukali. Jizuie usifanye hivyo. Methali 12:18 inasema hivi: “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.” Unawezaje kusema kwa “ulimi wa mwenye hekima”?

Mshukuru kwa kukuambia jinsi anavyohisi na kwa kupendezwa nawe. Omba msamaha ikiwa ulimpotosha bila kujua. Mwambie waziwazi lakini kwa fadhili kwamba wewe huhisi hivyo. Ikiwa hakuelewi na unahitaji kuzungumza kwa uthabiti zaidi, bado epuka kusema kwa ukali na kwa maneno machungu. Hisia zake nyororo zinahusika kwa hiyo uwe na subira. Ikiwa wewe ndiwe ungekuwa unamwuliza, ungependa akutendee kwa wororo, sivyo?

Hata hivyo, anaweza kusisitiza kwamba ulimpotosha. Anaweza kutaja mambo yaliyofanya awe na hisia hizo. Huenda akasema, ‘Unakumbuka uliponipa ua?’ au ‘Kumbuka ulichoniambia tulipotembea pamoja mwezi uliopita?’ Sasa lazima ujichunguze kwa uangalifu.

Kubali Ukweli

Wasafiri wa kale waliona maeneo waliyogundua kuwa vitu vya kujishindia na kutumiwa walivyotaka, na hivyo ndivyo wanaume fulani wanavyowaona wanawake. Wanapenda kuwa na mahusiano ya kimahaba lakini hawataki kufunga ndoa. Bila kutaka kuwa na daraka lolote, wao hujaribu kuwavutia wanawake kwa kuchezea hisia zao. Mwanamume kama huyo huvutia hisia za mwanamke kwa hila. Mzee mmoja Mkristo anasema: “Vijana fulani huwachezea wasichana, wakitoka kwa mmoja hadi mwingine. Si vizuri kuchezea hisia za mwanamke hivyo.” Ubinafsi kama huo hutokeza nini?

“Kama mtu mwenye wazimu anayetupa silaha za moto, mishale na kifo, ndivyo alivyo mtu ambaye amemdanganya mwenzake na kusema: ‘Je, sikuwa nikifanya mzaha tu?’” (Methali 26:18, 19) Mwanamume anapoanzisha uhusiano na mwanamke bila kufikiria hisia zake, mwanamke atatambua hilo. Kisha ataumia sana moyoni kwa sababu ya hila hiyo, kama simulizi lifuatalo linavyoonyesha.

Kijana mmoja alianzisha uhusiano wa kimahaba na mwanamke fulani lakini hakutaka kumwoa. Alimpeleka kwenye hoteli nzuri, nao walikwenda kwenye karamu pamoja. Kijana alifurahia kuwa pamoja naye, na msichana aliamini kwamba anamchumbia. Alipogundua kwamba alipendezwa tu kuwa pamoja naye, aliumia sana.

Unapaswa kufanya nini ikiwa umempotosha bila kujua msichana ambaye amekuja kwako? Kujaribu kujitetea kutamfanya tu awe na uchungu. Fikiria kanuni hii ya Biblia: “Anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” (Methali 28:13) Kwa hiyo, sema kweli. Kubali ulilofanya ndiposa akakuelewa vibaya. Ikiwa ulichezea hisia zake kimakusudi, kubali ulifanya kosa zito. Omba msamaha kikweli.

Hata hivyo, usifikiri kwamba kuomba msamaha kutamaliza mambo. Huenda msichana huyo akakasirika kwa muda fulani. Huenda ukahitaji kuwaeleza wazazi wake kwa nini ulitenda hivyo. Na unaweza kukabili madhara mengine. Andiko la Wagalatia 6:7 linasema: “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.” Lakini kuomba msamaha na kufanya yote unayoweza kusahihisha kosa lako, kutamsaidia atulie. Na kisa hicho kitasaidia ‘kulinda midomo yako isiseme udanganyifu’ katika mambo yote maishani kutia ndani mambo yanayohusu watu wa jinsia tofauti.—Zaburi 34:13.

Fikiri kwa Uzito Kabla ya Kujibu

Lakini vipi ikiwa ungependa kumfahamu msichana huyo vizuri zaidi? Ikiwa ni hivyo, unapaswa kukumbuka kwamba uchumba si jambo tu la kujifurahisha. Hisia zenye nguvu ambazo watu wanaochumbiana hupata huwaelekeza kufunga ndoa. Wanapofunga ndoa, hisia hizo huwaunganisha pamoja kama mume na mke. Kujua hilo kunaweza kukuathirije?

Unapofikiri kuhusu msichana huyo, huenda ukatambua kwamba anapendeza katika njia mbalimbali. Amefungua mlango na ungependa kuuacha wazi. Lakini badala tu ya kukimbilia uchumba kwa kishindo, chukua hatua zitakazowalinda msiumie baadaye.

Baada ya muda fulani, huenda ukataka kuzungumza na watu fulani wakomavu wanaomjua. Mwambie afanye vivyo hivyo na watu fulani wanaokujua. Nyote mnapaswa kuwauliza watu hao wakomavu kuhusu sifa zenu nzuri na udhaifu wenu. Pia, unaweza kuwauliza wazee Wakristo maoni yao. Ni vizuri kujua ikiwa yule mtu unayependezwa naye kimahaba anaheshimiwa katika kutaniko la Kikristo.

Lakini huenda ukasema, ‘Kwa nini niwahusishe wengine katika maisha yangu ya kibinafsi?’ Ukweli ni kwamba hata katika jambo la kibinafsi kama uchumba, ni jambo la hekima kupata maoni ya wengine. Kwa kweli, hilo linapatana na Biblia kwani Methali 15:22 inasema: “Katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” Watu wazima utakaozungumza nao hawatakuamulia. Lakini huenda “shauri la nafsi” wanalotoa likafunua mambo yako na ya mtu huyo mwingine, ambayo huoni.—Methali 27:9.

James, aliyenukuliwa mwanzoni, alifanya hivyo. Ingawa alikuwa akiishi peke yake, alizungumza na wazazi wake kuhusu Susan. Kisha wote wawili wakabadilishana majina ya watu wengine wakomavu ambao wangewapa maoni kuhusu kama wanafaana. Baada ya kupata ripoti nzuri kuhusu kila mmoja wao, James na Susan walianza kuchumbiana ili waone ikiwa wangeweza kuoana. Ukichukua hatua kama hizo kabla ya kupendezwa sana na mtu mwingine, utajihisi ukiwa salama utakapofanya uamuzi.

Zaidi ya yote, sali kwa Yehova. Kwa kuwa uchumba ni hatua inayoongoza kwenye ndoa, mwombe Mungu akusaidie uone ikiwa kuanzisha uhusiano na msichana huyo kutakuwezesha kufanya hivyo. La muhimu zaidi, mwombe Mungu awasaidie nyote kufanya maamuzi yatakayowaleta karibu naye. Mkifanya hivyo, nyote wawili mnaweza kupata furaha ya kweli.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 6 Makala za “Vijana Huuliza” katika magazeti ya Amkeni! ya Oktoba 22, 2004, na Desemba 22, 2004, yanazungumzia jinsi mwanamke anavyoweza kumwendea mwanamume ili kuanzisha uchumba.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Ikiwa kwa kweli hupendezwi, uwe mwangalifu usimpotoshe bila kujua