Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kudumisha Kazi Yako

Jinsi ya Kudumisha Kazi Yako

Jinsi ya Kudumisha Kazi Yako

“Je, umemwona mtu stadi katika kazi yake? Yeye atasimama mbele ya wafalme.”—Methali 22:29.

KAMA andiko hilo la Biblia linavyoonyesha, mara nyingi, wafanyakazi stadi huthaminiwa sana. Waajiri huthamini stadi na sifa gani za wafanyakazi wao? George, mkurugenzi wa wafanyakazi katika kampuni moja yenye wafanyakazi 700, alimwambia hivi mwandishi wa Amkeni!: “Sisi huthamini mfanyakazi aliye na uwezo wa kuwasiliana vizuri na anayeshirikiana na wengine.” Biblia ina mashauri mazuri yanayoweza kukusaidia kuboresha stadi hizo, na hivyo kudumisha kazi yako. Fikiria mifano michache.

Wasiliana Vizuri

Mwandishi wa Biblia Yakobo, anaonyesha kwamba mtu anayejua kuwasiliana vizuri huanza kufanya hivyo hata kabla hajafungua kinywa chake. Yakobo aliandika kwamba mtu anapaswa kuwa “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.” (Yakobo 1:19) Kwa nini shauri hilo linafaa? Sulemani aliandika hivi: “Yeyote anapojibu jambo kabla ya kulisikia, huo ni upumbavu na aibu kwake.” (Methali 18:13) Kwa kweli, kumsikiliza mwajiri wako na wafanyakazi wenzako kwa makini kunaweza kuzuia kutoelewana na kukuzuia usifanye makosa ya kipumbavu.

Zingatia pia jinsi unavyozungumza. Ukizungumza waziwazi na kwa sauti ya kutosha, yaelekea utaeleweka na huenda msikilizaji wako akaheshimu sana mambo unayosema. Brian, mshauri wa kazi aliyetajwa katika makala iliyotangulia anasema: “Huenda ukashangaa kujua ni watu wangapi hupoteza kazi zao si kwa sababu hawana ustadi wa kazi bali kwa sababu ya kukosa uwezo wa kuwasiliana vizuri.”

Shirikiana na Wengine

Bila shaka utawajua wafanyakazi wenzako vizuri sana kwa kuwa utatumia wakati mwingi pamoja nao. Kwa sababu hiyo, huenda ukashawishiwa kuwasengenya kwa kutaja makosa na kasoro zao. Hata hivyo, Biblia inashauri hivi: ‘Fanya iwe shabaha yako kuishi kwa utulivu na kukazia akili mambo yako mwenyewe.’ (1 Wathesalonike 4:11) Kwa kufanya hivyo, utaepuka kuwa na sifa ya “kujiingiza katika mambo ya watu wengine.” (1 Petro 4:15) Isitoshe, utaepuka kupoteza wakati na kuzozana na wafanyakazi wenzako bila sababu.

Ukiombwa ufanye kazi fulani, kumbuka shauri hili la Yesu lenye hekima: “Mtu fulani aliye na mamlaka akikulazimisha uingie katika utumishi wa kilometa moja, nenda pamoja naye kilometa mbili.” (Mathayo 5:41) Yesu alikuwa akizungumzia mamlaka ya kiserikali lakini bila shaka kanuni hiyo inaweza kutumiwa kazini. Ukijulikana kuwa mfanyakazi mwenye bidii ambaye hufanya kazi ya ziada, yaelekea utadumisha kazi yako. Bila shaka, kuna mipaka ya mambo ambayo mwajiri wako anaweza kukuomba ufanye. Yesu alisema mtu anapaswa kumlipa “Kaisari vitu vya Kaisari, lakini Mungu vitu vya Mungu.” (Mathayo 22:21) Kanuni ambayo Yesu anataja hapa inaonyesha kwamba hupaswi kuwaruhusu wale walio na mamlaka wavuruge mambo muhimu zaidi kama vile kumwabudu Mungu.

Uwe Mnyoofu

Uchunguzi mmoja uliofanyiwa kampuni zaidi ya 1,400 ulionyesha kwamba waajiri wengi “walivutiwa sana na watu waliokuwa wakitafuta kazi ambao ni wanyoofu na waaminifu.” Bila shaka, kuwa mnyoofu kunatia ndani kutoiba pesa au vifaa vya mwajiri wako. Pia kunamaanisha kutoiba wakati. Uchunguzi uliofanywa na shirika moja la kuwasaidia watu kupata kazi ulionyesha kwamba mfanyakazi mmoja aliiba wastani wa saa 4 na dakika 15 kila juma. Kati ya mambo ambayo wezi hao wa wakati walifanya ni kuchelewa kufika kazini kila mara, kutoka kazini mapema, na kuzungumza na wafanyakazi wengine saa za kazi.

Biblia inashauri hivi: “Mwizi asiibe tena, bali afanye kazi ya bidii, akifanya kwa mikono yake kazi iliyo njema, ili awe na kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.” (Waefeso 4:28) Isitoshe, Neno la Mungu huwatia moyo Wakristo wafanye kazi kwa bidii hata ikiwa hawatazamwi na wasimamizi wao. Mtume Paulo aliandika hivi: “Watiini katika kila jambo wale ambao ni mabwana zenu katika maana ya kimwili, si kwa matendo ya utumishi wa macho, kama wenye kupendeza wanadamu, bali kwa unyoofu wa moyo, kwa kumwogopa Yehova.” (Wakolosai 3:22) Ikiwa unajulikana kuwa mfanyakazi mwenye bidii hata wakati ambapo husimamiwi, wewe ni mfanyakazi anayeweza kutumainika.

Uwe Mwenye Usawaziko

Biblia ilitabiri kwa usahihi kwamba nyakati zetu zingekuwa hatari na ngumu kushughulika nazo. (2 Timotheo 3:1) Bila shaka, misukosuko na machafuko ya kisiasa na kijamii yangetokeza mahangaiko ya kiuchumi. (Mathayo 24:3-8) Kwa hiyo, hata ukifuata mapendekezo yaliyotajwa katika makala hii, huenda bado ukapoteza kazi yako.

Hata hivyo, kufuata kanuni za Biblia kunaweza kukusaidia upunguze mahangaiko wakati ambapo huna kazi. Yesu alisema: “Basi, ikiwa Mungu huivika hivyo mimea ya shambani, ambayo ipo hapa leo na kesho hutupwa ndani ya jiko, je, yeye hataona ni afadhali zaidi awavike, ninyi wenye imani kidogo? Kwa hiyo msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ . . . Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.”—Mathayo 6:30-32.

Kama tu watu wengine wengi ulimwenguni pote, Ericka, aliyetajwa awali ameona ukweli wa maneno yaliyotajwa juu. Anasema hivi kwa ufupi: “Ninafurahia sana kazi ninayofanya sasa. Lakini ninajua kwamba mambo hubadilika. Ingawa hivyo, kwa kufuata kanuni za Biblia na kumtumaini Yehova, nimejifunza jinsi ya kupunguza mahangaiko nisipokuwa na kazi na pia jinsi ya kuridhika na kazi ninayopata.”

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kutosikiliza mikutanoni kunaweza kufanya upoteze kazi yako