Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Katika Lugha Yetu Hakuna Matusi”

“Katika Lugha Yetu Hakuna Matusi”

“Katika Lugha Yetu Hakuna Matusi”

MATUSI ni nini? Ni “maneno machafu ya kumuudhi mtu; kutukana.” (Kamusi ya Kiswahili Sanifu—Toleo la Pili) Kwa kusikitisha, watu katika nchi nyingi hutumia matusi kwa ukawaida. Ingawa zamani ilikuwa kawaida kwa wanaume peke yao kutumia matusi, leo ni kawaida kuwasikia wanawake wakitumia matusi. Hata hivyo katika utamaduni fulani matusi hayakuwa yakitumiwa. Kwa mfano, fikiria maneno ya Mwenyeji wa Asili wa Amerika James Kaywaykla.

James alizaliwa karibu mwaka wa 1873, huko New Mexico, Marekani. Katika miaka yake ya baadaye, alipokuwa na umri wa miaka 90 hivi, alisema yafuatayo:

“Asubuhi moja niliamshwa na sauti ya babu yangu. Alikuwa ameketi kwenye bustani yetu, akitazama jua lililokuwa likichomoza, na kuimba Wimbo wa Asubuhi. Huu ni wimbo wa Ussen . . . kumshukuru kwa ajili ya mojawapo ya zawadi yake kuu, yaani, upendo uliopo kati ya mwanamume na mwanamke, kwani hicho ni kitu kitakatifu kwa Wenyeji wa Asili wa Amerika. * Wao hawafanyi mizaha michafu kuhusu ngono wala hawawezi kuelewa kwa nini Macho Meupe [Wazungu] hufanya mzaha kuhusu kutunga mimba na kuzaa. Kwao, kufanya mzaha kuhusu ngono, ni sawa na kudharau jina la Mungu. Ninajivunia sana kwamba katika lugha yetu hakuna matusi. Tunamshukuru Muumba wa Uhai kwa pendeleo la kushiriki katika kuumba uhai mpya.”—Native Heritage, kilichohaririwa na Arlene Hirschfelder.

Karibu miaka 2,000 iliyopita, Paulo mtume Mkristo aliandika hivi: “Neno lililooza na lisitoke kinywani mwenu, bali neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga kulingana na uhitaji, ili liwape wasikiaji lile linalofaa.” Aliandika hivi pia: “Uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa visitajwe hata kidogo katikati yenu, kama inavyowafaa watu watakatifu; wala mwenendo wa aibu wala maneno ya kipumbavu wala mizaha michafu, mambo yasiyofaa, lakini badala ya hayo, utoaji wa shukrani.”—Waefeso 4:29; 5:3, 4.

Matusi na mizaha michafu inaweza kuondolewaje katika moyo, akili, na kinywa? Shauri la Paulo kwa Wafilipi linaweza kutusaidia sisi sote: “Akina ndugu, mambo yoyote yaliyo ya kweli, mambo yoyote yaliyo ya hangaiko zito, mambo yoyote yaliyo ya uadilifu, mambo yoyote yaliyo safi kiadili, mambo yoyote yaliyo ya kupendeka, mambo yoyote yanayosemwa vema, wema wa adili wowote ulioko na jambo lolote la kustahili sifa lililoko, endeleeni kuyafikiria mambo hayo.”—Wafilipi 4:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Kulingana na imani ya Wenyeji wa Asili wa Amerika, Ussen ndiye muumba wa uhai.

[Picha katika ukurasa wa 31 zimeandaliwa na]

All photos: Library of Congress, Prints & Photographs Division; Apache symbol: Dover Publications, Inc.