Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Kuutazama Ulimwengu

Madawa ya Vitamini na Kansa

Uchunguzi 14 tofauti-tofauti uliohusisha watu 170,000 unadokeza kuwa madawa ya vitamini hayawezi kuzuia kansa ya koo, tumbo, ini, na kongosho. Kulingana na gazeti la kitiba Deutsches Ärzteblatt, sawa na madawa ya beta carotene na vitamini A, C, na E hayana faida bali huenda yakaongeza kwa kiasi kidogo hatari ya kupatwa na kansa. Dakt. Richard Sullivan wa Kituo cha Utafiti wa Kansa nchini Uingereza anasema hivi: “Hakuna njia fupi ya kuzuia kansa ya utumbo mpana. Ikiwa unatumia vitamini kujilinda na ugonjwa huo, unapoteza pesa.” Anaongeza hivi: “Njia bora ya kupunguza hatari ni kula vyakula vinavyofaa na kutovuta sigara.”

Je, Una Wasiwasi Kuhusu Viini?

Makala moja katika gazeti The New York Times inasema: “Ni upumbavu kufikiria eti unaweza kuwa na nyumba isiyo na viini kwani haiwezekani. Isipokuwa uwe unaishi na mtu mzee sana, mchanga sana (mwenye umri wa chini ya miezi 6), au mgonjwa sana, bakteria chache zilizo juu ya meza, komeo la mlango, au kijiko haziwezi kukudhuru.” Ni kweli kwamba chakula kinachoweza kuharibika kikiachwa juu ya meza kwa saa kadhaa kinaweza kuwa na bakteria na kumfanya mtu aharishe. Ili kuzuia jambo hilo, weka chakula hicho ndani ya friji. Ili ujilinde na bakteria, si lazima utumie dawa za kuua bakteria. Gazeti hilo linasema: “Nawa mikono yako kwa sabuni na maji mara kadhaa kwa siku na usiwe na wasiwasi.”

Tumaini Linapungua

Gazeti la Hispania El País linaripoti: “Wahispania wengi wana tumaini dogo au hawatumaini kabisa mashirika yanayoongoza maisha yao.” Kulingana na Kituo cha Uchunguzi wa Masuala ya Kijamii, zaidi tu ya nusu ya watu 2,500 waliohojiwa walisema hawatumaini serikali, asilimia 56.2 hawatumaini benki, na asilimia 57.7 hawatumaini vyama vya wafanyakazi. Nchi hiyo ambayo karibu watu asilimia 75 hudai kuwa Wakatoliki, zaidi ya asilimia 61 walisema wana “tumaini dogo au hawalitumaini kabisa Kanisa Katoliki.” Tahariri ya gazeti Diario 16 ilisema hivi kuhusu jambo hilo: “Wahispania wengi husema waziwazi kwamba wao ni Wakatoliki lakini wengi wao si waumini wenye bidii wala hawakubali mafundisho yake.”

Kusoma Huboresha Kumbukumbu

Unaweza kuboreshaje kumbukumbu lako? Gazeti Folha Online la Brazili linasema: “Usitazamie muujiza. Siri ni kufanyiza akili yako kazi.” Mojawapo ya njia bora za kuchochea akili ni kusoma. Jinsi gani? Mtaalamu wa mfumo wa neva Ivan Izquierdo anasema: “Mtu anaposoma neno ‘mti,’ yeye hukumbuka miti yote ambayo amejua maishani katika muda mfupi sana.” Izquierdo anasema “hilo hutukia bila mtu kujua.” Anaamini kuwa njia hiyo ya kufanyiza akili kazi hufanya iwe vigumu kwa ubongo kupata ugonjwa kama vile Alzheimer. Mtaalamu wa mfumo wa neva, Wagner Gattaz wa Kituo cha Utafiti wa Matatizo ya Kumbukumbu huko São Paulo, Brazili, anasema: “Kadiri tunavyotumia kumbukumbu letu, ndivyo tunavyolihifadhi.”

Ujumbe Mfupi wa Simu Unaongezeka

Gazeti International Herald Tribune linaripoti kwamba “ujumbe zaidi ya bilioni 360 hutumwa kila mwaka ulimwenguni pote. Hiyo ni karibu ujumbe mfupi bilioni moja kwa siku.” Ujumbe mfupi wa simu unatumiwa zaidi sasa. Kampuni nyingi zinawatumia wateja ujumbe mfupi ili kuuza bidhaa zao. Kwa mfano, watu waliojiandikisha wanaweza kuomba watumiwe sala za papa kwenye simu zao za mkononi. Polisi nchini Uholanzi hutuma ujumbe mfupi kwenye simu zilizoibwa ili kuwatahadharisha watu wanaotaka kuzinunua kuwa simu hizo zimeibiwa. Na nchi zilizo na sheria ya kidini ambazo humruhusu mtu kumtaliki mke wake baada ya kumwambia mara tatu “nimekutaliki,” zimeidhinisha talaka kupitia ujumbe mfupi wa simu.

Matumizi ya Intaneti Nchini Uholanzi

Uchunguzi ulioripotiwa katika gazeti la Uholanzi Algemeen Dagblad unasema hivi: “Mtoto 1 kati ya 5 wenye umri wa miaka 11 na 12 amesumbuliwa kwa kutumiwa habari za ngono na mtu asiyemjua alipokuwa akitumia Intaneti.” Kulingana na orodha ya maswali iliyotumwa kwa wazazi 660 na watoto 220 wenye umri kati ya miaka 8 na 12, zaidi ya nusu ya watoto wanaotumia Intaneti wamewahi kujikuta katika “hali isiyopendeza” kwa kutumiwa “barua-pepe yenye kuudhi” au picha za ngono au habari nyingine isiyofaa. Wengi wa watoto hao waliwaambia wazazi jambo hilo. Pia uchunguzi huo unaonyesha kuwa wazazi 8 kati ya 10 wanaogopa hatari zinazoweza kuwapata watoto wao wanapotumia Intaneti, karibu nusu ya wazazi walisema wangependa kuwasimamia watoto wao wanapotumia Intaneti, asilimia 60 ya wazazi huweka kompyuta sebuleni ili kuwachunguza watoto wao, na kwamba watoto hutumia Intaneti kwa saa nzima hivi kila siku kucheza, kutuma barua-pepe, na kuwasiliana.

Shauri Wanalopendelea

Gazeti The Times la London linasema: “Uchunguzi fulani unaonyesha kuwa thuluthi mbili hivi ya wakurugenzi wa kampuni mashuhuri hupendelea kushauriwa na wenzi wao kuliko kushauriwa na wakurugenzi au wafanyakazi wenzao wanapokabili tatizo gumu kazini.” Bob Arnold ambaye kampuni yake ya ushauri ilifanya utafiti huo, anasema kwamba sifa inayowavutia wakurugenzi katika washauri si ustadi bali ni kutumainika. Anaeleza hivi: “Kwa kawaida, watu ambao huwashauri wakurugenzi hawapaswi kuathiriwa na maoni ya wengine, wanapaswa kuwa na busara na uzoefu,” lakini kwa kuwa kutumainika ndiyo sifa muhimu zaidi, wakurugenzi hupendelea kushauriwa na wake zao.

Huenda Hundi Zikaacha Kutumiwa

Gazeti U.S.News & World Report linasema: “Katika miaka 20 hivi ijayo huenda hundi zisitumiwe sana.” Kulipa kwa kutumia hundi kumepungua sana tangu kuanzishwa kwa “njia rahisi na za haraka zaidi kama vile kutumia kadi za mkopo na kulipa kwa kutumia kompyuta.” Mambo mengine yanayochangia hilo ni kuweka pesa kwenye benki kwa kutumia kompyuta na pia kulipa bili, ambayo ni njia inayowaruhusu wadeni watoe pesa kutoka kwenye akaunti ya benki ya wateja ili kulipia bili za kila mwezi. Benki zinadai kuwa kutotumia hundi za karatasi kutazuia kuibiwa kwa habari za wengine za siri. Hata hivyo, wataalamu fulani wa kuchunguza ulaghai wana wasiwasi kwamba kutumia hundi za kompyuta kutazidisha visa vya kuibiwa kwa habari za watu za siri na mbinu za kuwalaghai watu.