Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kujaribu Kulisha Watu Bilioni Moja

Kujaribu Kulisha Watu Bilioni Moja

Kujaribu Kulisha Watu Bilioni Moja

KILA siku watu bilioni moja hawapati chakula cha kuwatosha. Hata hivyo, kulingana na Umoja wa Mataifa hali hiyo yenye kusikitisha haipaswi kuwapo.

“Mmesema kwamba mnataka kumaliza kabisa umaskini.” Ndivyo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Kofi Annan alivyowaambia wanaume na wanawake mashuhuri zaidi ulimwenguni mnamo Septemba 8, 2000. Walikuwa wamekusanyika pamoja kwa ajili ya Kongamano la Milenia la Umoja wa Mataifa, ambapo viongozi hao walisema waziwazi kuhusu matatizo yanayowakabili watu maskini ulimwenguni. Makamu wa rais wa Brazili alisema: “Kuwa maskini hohehahe ni fedheha kwa binadamu.” Waziri mkuu wa Uingereza aliongezea kwamba, “inasikitisha kuwa nchi zilizoendelea zimeshindwa kusaidia bara la Afrika na hilo linashangaza na kutuaibisha tukiwa jamii yenye ustaarabu.”

Watu hao wawili walisema waziwazi kwamba mataifa yamejiaibisha kwa kushindwa kufanya yawezayo ili kuwalisha watu wenye njaa. Ili kuthibitisha tamaa yao ya kuboresha hali za wanadamu duniani, viongozi waliohudhuria kongamano hilo waliahidi kuchukua hatua na kutoa azimio lenye sehemu nane lililotia ndani yafuatayo: “Tutafanya yote tuwezayo kuwakomboa wanaume, wanawake na watoto wenzetu kutoka katika utumwa wa umaskini, hali inayowakabili watu zaidi ya bilioni moja. . . . Isitoshe tunaazimia kwamba: Kufikia mwaka wa 2015, tutapunguza kwa asilimia 50 idadi ya watu ambao hupokea chini ya dola moja kwa siku na ya watu wasiopata chakula cha kutosha ulimwenguni.”

Kumekuwa na maendeleo gani tangu mradi huo mzuri ulipotangazwa Septemba 2000?

Matendo Huwa na Matokeo Kuliko Maneno

Mnamo 2003, Mradi wa Usimamizi wa Ulimwengu wa Kongamano la Uchumi la Kimataifa ulianza kuchunguza mambo yaliyokuwa yamefanywa ili kutimiza miradi ya Kongamano la Milenia la Umoja wa Mataifa. Ripoti rasmi iliyotolewa Januari 15, 2004, inasema: “Ulimwengu umeshindwa kabisa kujitahidi inavyohitajiwa ili kutimiza miradi yake iliyo muhimu zaidi.” Ripoti hiyo inasema hivi kuhusu njaa: “Upungufu mkubwa wa chakula silo tatizo la ulimwengu—kuna chakula cha kuwatosha watu wote. Tatizo ni kwamba watu wasio na pesa hawapati chakula hicho chenye lishe bora.”

Ripoti hiyo inasema hivi kuhusu tatizo la umaskini: “Serikali, zenye utajiri na zilizo maskini, ndizo zinazopaswa kulaumiwa kwa kuwa na uzembe wa kutekeleza ahadi hizo. Lakini mfumo wa uchumi wa kimataifa uliobuniwa na nchi zenye utajiri hauwafaidi maskini. Nchi tajiri hutoa ahadi nyingi, lakini haziko tayari kubadili mfumo huo wa uchumi au kuwasaidia maskini.” Licha ya hali hiyo, wanasiasa wanaendelea kujadiliana badala ya kutenda, na kila serikali inaelekeza mambo kwa hila ili kujifaidi. Wakati huohuo, watu maskini ulimwenguni wanaendelea kukosa chakula.

Hati ya Kongamano la Uchumi wa Ulimwengu yenye kichwa “Kuacha Kuahidi na Kuanza Kutenda,” ilionya kwamba “ikiwa sera za uchumi za kimataifa hazitabadilishwa, mataifa hayatakuwa na sera za kumaliza ukosefu wa chakula, na ikiwa jitihada hazitazidishwa, watu wengi sana watazidi kukabili njaa.” Na ni nani anayepaswa kutunga sera bora na kuanzisha “jitihada zitakazofanikiwa”? Ni serikali zilezile ambazo mwaka wa 2000 zilitangaza azimio lao la kuboresha maisha ya wanadamu.

Ahadi moja isiyotimizwa huvunja moyo; ahadi kadhaa zisizotimizwa hukatisha tamaa. Watu wamepoteza tumaini lao katika serikali kwa sababu zimeshindwa kutimiza ahadi yao ya kuwatunza maskini. Mama mmoja mwenye watoto watano katika nchi maskini ya Karibea anaweza kuandalia familia yake mlo mmoja tu kwa siku. Anasema hivi: “Mimi huhangaikia tu kupata chakula. Sijali ni nani anayetawala. Hatujawahi kupata msaada wowote kutoka kwa mtawala yeyote.”

Mwandikaji wa Biblia Yeremia alisema hivi: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Kushindwa kwa serikali za wanadamu kuwasaidia maskini kunathibitisha ukweli wa maneno hayo ya Biblia.

Hata hivyo, kuna Mtawala aliye na uwezo na anayetaka kutatua matatizo ya wanadamu, na Biblia inamtambulisha. Mtawala huyo atakapochukua mamlaka, hakuna mtu atakayekosa chakula.

Msingi wa Tumaini

“Macho ya wote yanakutazama yakiwa na tumaini, nawe unawapa chakula chao katika majira yake.” (Zaburi 145:15) Ni nani huyo anayehangaikia uhitaji wa wanadamu wa kupata chakula? Ni Muumba wetu, Yehova Mungu. Ingawa wanadamu wameteseka kutokana na ukosefu wa chakula na matatizo mengine kwa maelfu ya miaka, sikuzote Yehova anapendezwa nao. Ameona kwamba serikali za wanadamu zimeshindwa, na Biblia, Neno lake linalotegemeka linaonyesha kwamba karibuni ataziondoa na kuleta serikali yake mwenyewe.

Yehova anasema: “Mimi, naam, mimi nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu.” (Zaburi 2:6) Tangazo hilo kutoka kwa mamlaka iliyo kuu zaidi ulimwenguni inatupa sababu ya kuwa na tumaini. Mara nyingi watawala wa kibinadamu wameshindwa kuwasaidia raia zao, Yesu Kristo akiwa Mfalme aliyechaguliwa na Mungu atawaletea baraka ambazo watu maskini duniani hawajawahi kupata.

Kupitia Mfalme wake, Yehova atawalisha watu wote wenye njaa. “Yehova wa majeshi hakika atavifanyia vikundi vyote vya watu, . . karamu ya vyakula vinono,” linasema andiko la Isaya 25:6. Chini ya Ufalme wa Mungu mikononi mwa Kristo, watu hawatakosa chakula kizuri, haidhuru wanaishi wapi. Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.”—Zaburi 145:16.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

“Inasikitisha kuwa nchi zilizoendelea zimeshindwa kusaidia bara la Afrika na hilo linashangaza na kutuaibisha tukiwa jamii yenye ustaarabu.”—Waziri Mkuu wa Uingereza Tony Blair

[Picha katika ukurasa wa 12]

ETHIOPIA: Katika nchi hii karibu watu milioni 13 hutegemea chakula cha msaada. Mtoto aliye hapo juu ni mmoja wao

[Picha katika ukurasa wa 12]

INDIA: Wanafunzi hawa hupata chakula shuleni

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 12]

Top: © Sven Torfinn/Panos Pictures; bottom: © Sean Sprague/Panos Pictures