Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ninavutiwa na Watu Wasiofaa?

Kwa Nini Ninavutiwa na Watu Wasiofaa?

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Ninavutiwa na Watu Wasiofaa?

“Nilijua kwamba sikupaswa kumruhusu awe rafiki wa karibu sana, lakini sikuweza kujizuia. Sikuamini kwamba mwanamume angependezwa nami.”—Nancy. *

“Nilikuwa nikienda peke yangu kuteleza kwa viatu vya magurudumu, na nikaanza kushirikiana kwa ukawaida na ‘marafiki’ niliowapata huko. Punde si punde, nilikuwa nikiishi maisha ya ukosefu wa maadili.”—Dan.

MWANZONI wote wawili, Nancy na Dan walikuwa imara kiroho. Nancy alilelewa katika familia inayomwogopa Mungu na alianza kuwahubiria watu alipokuwa na umri wa miaka tisa. Dan alianza utumishi wa wakati wote alipokuwa tineja. Lakini, wote wawili walikabili magumu katika utumishi wao kwa Mungu. Kwa nini? Walishirikiana na watu wasiofaa.

Je, umewahi kuvutiwa bila kujua na mtu ambaye ulihisi anakuathiri vibaya? Huenda alikuwa mwanadarasa mwenzako ambaye mlipendezwa na mambo yaleyale, au hata mtu wa jinsia tofauti ambaye ulipendezwa naye kimahaba.

Huenda ulikumbuka shauri hili la Biblia: “Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Lakini je, watu wote wasiomtumikia Yehova ni mashirika mabaya? Vipi ikiwa wana sifa fulani nzuri, labda hata zenye kupendeza? Pia, vipi ikiwa mtu ni mwabudu mwenzetu lakini yeye si mfano mzuri kiroho? Kabla ya kujibu maswali hayo, acheni tuchunguze ni jinsi gani na kwa nini upendezi huo hutokea.

Kinamchofanya Mtu Avutiwe

Kwa kuwa wanadamu wote wameumbwa kwa mfano wa Mungu, inatazamiwa kwamba wengine wasiomjua Yehova watakuwa na sifa nzuri. Kwa hiyo, huenda ukaona kuwa watu fulani wanaheshimika, labda hata wanapendeza, ingawa hawamwabudu Mungu wa kweli. Je, unapaswa kuwapuuza kabisa watu kama hao kwa kuwa tu hawafahamu kweli za Biblia? La hasha. Biblia inapotushauri “tuwatendee wote mema,” hilo linatia ndani wale ambao hawana imani ya Kikristo kama yako. (Wagalatia 6:10) Kwa hiyo kuwa mwangalifu unapochagua washiriki wa karibu hakumaanishi unapaswa kutenda kana kwamba wewe ni bora kuliko wengine. (Methali 8:13; Wagalatia 6:3) Mwenendo kama huo haupatani na imani yako ya Kikristo.

Hata hivyo, vijana fulani Wakristo wamefanya mengi zaidi ya kuwa marafiki tu; wamefanya urafiki wa karibu sana na watu ambao wanapendezwa kidogo au wasiopendezwa hata kidogo na mambo ya kiroho. Dan, aliyetajwa awali, alikuwa stadi wa kuteleza kwa viatu vya magurudumu. Watu ambao alishirikiana nao kwa ukawaida katika mchezo huo hawakuwa Wakristo. Mwishowe, Dan alijiunga na “rafiki” zake wapya katika ukosefu wa maadili na kutumia dawa za kulevya. Alipotambua kuwa maisha yake hayapatani na Ukristo, Dan aliacha kuhubiri na kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Ilimchukua miaka kadhaa kabla ya kupata nguvu za kufanya mabadiliko yaliyohitajika ili arudie ibada ya kweli.

Melanie alivutiwa na mwamini mwenzake aliyekuwa dhaifu kiroho. Melanie alieleza: “Niliambiwa alihitaji kutiwa moyo kwa hiyo nikaanza kushirikiana naye.” Bila shaka, Biblia huwatia moyo Wakristo ‘wawategemeze walio dhaifu.’ (1 Wathesalonike 5:14) Lakini Melanie alianza kwenda kwenye baa pamoja na rafiki yake mpya, ambako marafiki wengine walimwingiza katika mwenendo mbaya.

Daraka la Familia

Hali ya familia inaweza kuamua utavutiwa na nani. Michelle aliwaza kuhusu sababu iliyomfanya apendezwe na wavulana wenye matatizo ya kihisia na wasiojali. Aliamua ni kwa sababu walimkumbusha kuhusu baba yake, ambaye hakuwa na uhusiano wa karibu naye na hakumjali. Anaamini kuwa kujaribu kutafuta upendo kutoka kwa baba yake ambaye hakumwonyesha hisia zozote kwa muda mrefu kulimfanya apendezwe na mahusiano kama hayo.

Tofauti na hilo, kijana aliyelelewa na wazazi Wakristo anaweza kuwa na udadisi kuhusu jinsi wengine huishi, na kuhisi kwamba wazazi wake ni wagumu kupita kiasi. Iwe ni hivyo au la, je, suluhisho ni kufanya “urafiki na ulimwengu?” (Yakobo 4:4) Fikiria kilichompata Bill.

Ingawa alifundishwa Maandiko na mama yake tangu utotoni, Bill aliamua kutojiweka wakfu kwa Yehova, akihisi kwamba kufanya hivyo kungemzuia afanye analotaka. Akitaka kujua jinsi maisha ya mtu asiye Mkristo wa kweli yalivyo, alianza kushirikiana na genge lililomwingiza katika dawa za kulevya, jeuri, na uhalifu. Alikimbizwa na polisi, akaumia na kupoteza fahamu kwa miezi kadhaa. Madaktari waliona kwamba angekufa. Kwa furaha, Bill alipona. Lakini hawezi kuona na amelemaa. Alijifunza kutokana na magumu yaliyompata naye sasa ni Mkristo aliyejiweka wakfu. Lakini pia Bill amegundua kwamba kujifunza kupitia magumu kunaweza kutokeza madhara ya kudumu.

Uvutano Mwingine

Nyakati nyingine vyombo vya habari huathiri maoni ya vijana kuhusu rafiki anayefaa. Kwa mfano, si ajabu kuona vitabu, vipindi vya televisheni, sinema, na video za muziki zikionyesha shujaa ambaye mwanzoni huonekana kuwa mkali au mwenye mtazamo mbaya lakini baadaye anaonyeshwa akiwa na huruma. Wazo ambalo hutolewa ni kwamba watu wanaoonekana kuwa wasiojali au wenye kujifikiria wanaweza kuwa na hisia na wenye kujali. Kwa kuongezea, wazo linaloweza kupitishwa ni kwamba rafiki mzuri, na mara nyingi yule wa jinsia tofauti, ndiye anayehitajika ili kutokeza sifa hizo nzuri. Wazo hilo hufanya hadithi hizo zivutie. Lakini, unafikiri mambo hayo hutukia hivyo mara ngapi? Kwa kusikitisha, vijana fulani wamedanganyika na kufanya urafiki, au hata kumwoa, mtu mwenye ubinafsi na mjeuri, kisha wakasubiri “ageuke” bila mafanikio na kuwa mtu mwenye kujali.

Fikiria sababu nyingine ambayo huwafanya watu fulani wavutiwe na watu wasiofaa: Wao huona kuwa hawapendezi kwa hiyo humkubali mtu yeyote tu atakayeonyesha anapendezwa nao. Nancy, aliyetajwa awali, alijua kwamba Biblia inasema mtu anapaswa kuoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Lakini alihisi kuwa havutii na hivyo alifurahi mfanyakazi mwenzake asiye na imani moja naye, alipopendezwa naye kimahaba. Alianza kushirikiana naye na karibu aingie katika ukosefu wa maadili.

Kama masimulizi yaliyotajwa yanavyoonyesha, kuna sababu nyingi zinazoweza kumfanya kijana Mkristo avutiwe na watu wanaoweza kumwathiri vibaya, na inaonekana kuna njia nyingi sana za kupunguza uzito wa kufanya urafiki nao. Lakini, urafiki wa aina hiyo hutokeza mambo yenye kuhuzunisha na hata madhara. Kwa nini?

Uvutano wa Marafiki

Jambo hakika ni kwamba, mtu hutenda kama rafiki zake. Kwa hiyo wale tunaoshirikiana sana nao hutuathiri sana. Methali 13:20 inaonyesha kwamba uvutano huo unaweza kusaidia au kudhuru: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wajinga atapatwa na mabaya.” Marafiki wa karibu, kama watu wawili walio katika gari moja, huelekea upande mmoja na kufika mahali pamoja. Kwa hiyo jiulize: ‘Je, barabara ambayo rafiki yangu anatumia inaongoza ninakotaka kwenda? Je, itanielekeza karibu na miradi na matarajio yangu ya kiroho?’

Kwa kweli, inaweza kuwa vigumu kujichunguza kwa unyoofu. Huenda hisia zenye nguvu zikahusika. Lakini je, tunapaswa kuchagua marafiki kwa kuongozwa tu na hisia? Labda umesikia shauri hili ambalo hutolewa mara nyingi, “Fuata moyo wako.” Lakini Methali 28:26 inasema: “Anayetegemea moyo wake mwenyewe ni mjinga.” Kwa nini? Kwa sababu “moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9; Hesabu 15:39) Kuwa mwenye hila ni kukosa ushikamanifu, kudanganya, au kuwa msaliti. Je, unaweza kumtumaini mtu anayejulikana kuwa mwongo na msaliti? Moyo wetu wa mfano unaweza kuwa wenye hila. Hivyo, si lazima uhusiano uwe mzuri eti tu kwa sababu unahisi uko sawa.

Mwongozo unaotegemeka zaidi ni Neno la Mungu. Tofauti na moyo wako usio mkamilifu, kanuni za Biblia hazitakupotosha au kukukatisha tamaa. Kanuni za Biblia zinaweza kukusaidiaje kuamua ikiwa mtu fulani atakuwa rafiki mzuri? Na unawezaje kuepuka kufanya uchaguzi mbaya unapochagua rafiki wa kudumu, yaani, mwenzi wa ndoa? Maswali hayo yatazungumziwa katika makala ya wakati ujao.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Vyombo vya habari vinaweza kuathiri maoni yetu kuhusu rafiki anayefaa