Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Misiba Yote Itakoma Hivi Karibuni

Misiba Yote Itakoma Hivi Karibuni

Misiba Yote Itakoma Hivi Karibuni

“Watoto na wajukuu. Sikilizeni! . . . Muda si muda, mlima huu utawaka moto. Lakini kabla ya hilo kutukia, kutakuwa na mingurumo, kelele, na matetemeko. Moshi, miale na radi itatemwa, na hewa itatetema na kunguruma. Kimbia wakati uwezapo . . . Ukiupuuza, ukiona vitu na mali kuwa vyenye thamani zaidi kuliko uhai wako, mlima utakuadhibu kwa sababu ya kutojali na pupa. Usijishughulishe na nyumba yako, kimbia bila kusitasita.”

ONYO hilo lililonukuliwa katika kitabu Earth Shock, cha Andrew Robinson, lilikuwa limeandikwa kwenye jiwe la ukumbusho huko Portici, mji ulio chini ya Mlima Vesuvius huko Italia, baada ya volkano hiyo kulipuka mwaka wa 1631 W.K. Mlipuko huo uliua watu zaidi ya 4,000. Robinson anasema, “bila kutazamiwa, mlipuko huo wa mwaka wa 1631 ndio uliofanya Mlima Vesuvius ujulikane sana.” Jinsi gani? Kujengwa upya kwa Portici ndiko kulifanya majiji ya Herculaneum na Pompeii yavumbuliwe. Majiji hayo yaliharibiwa kabisa Mlima Vesuvius ulipolipuka mnamo 79 W.K.

Plini Mchanga, Mroma aliyeokoka msiba huo na ambaye baadaye akawa gavana, aliandika kuhusu matetemeko yasiyo ya kawaida ambayo yalitoa onyo. Yeye, mama yake, na wengine walitii onyo hilo na kuokoka.

Ishara ya Kuonya ya Wakati Wetu

Leo tunakaribia sana mwisho wa mifumo ya kiuchumi, kijamii, na kisiasa ya ulimwengu huu. Tunajuaje? Kwa sababu Yesu Kristo alitabiri mfululizo wa matukio ya ulimwengu ambayo yangekuwa ishara ya kwamba siku ya hukumu ya Mungu imekaribia. Kama volkano inayonguruma, kutoa moshi, na vipande vya lava, ishara hiyo yenye mambo mengi inatia ndani vita vikubwa, matetemeko ya nchi, njaa, na tauni, mambo hayo yote yameukumba ulimwengu kwa kiwango kisicho na kifani tangu 1914.—Mathayo 24:3-8; Luka 21:10, 11; Ufunuo 6:1-8.

Lakini ishara ya kuonya ya Yesu pia inatia ndani ujumbe wa tumaini. Alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Ona kwamba Yesu aliuita ujumbe wa Ufalme “habari njema.” Kwa kweli, ni habari njema kwa sababu Ufalme wa Mungu, ambao ni serikali ya kimbingu ambayo mfalme wake ni Kristo Yesu, itaondoa madhara yote ambayo wanadamu wamesababisha. Isitoshe, itakomesha misiba ya asili.—Luka 4:43; Ufunuo 21:3, 4.

Kwa kweli, Yesu alipokuwa mwanadamu duniani, alionyesha nguvu zake za kudhibiti hali ya hewa kwa kutuliza dhoruba iliyohatarisha uhai. Wanafunzi wake wenye woga walisema hivi kwa mshangao: “Kwa kweli huyu ni nani, kwa maana anaagiza hata pepo na maji, nazo zinamtii?” (Luka 8:22-25) Leo, Yesu si mwanadamu duni, bali ni kiumbe wa roho mwenye nguvu. Kwa hiyo, hatakuwa na tatizo lolote la kudhibiti nguvu za asili ili zisiwadhuru raia zake!—Zaburi 2:6-9; Ufunuo 11:15.

Huenda wengine wakaona kuwa jambo hilo ni ndoto tu. Lakini kumbuka kwamba tofauti na ahadi na utabiri wa wanadamu, unabii wa Biblia, kutia ndani unabii mbalimbali ambao tumeona ukitimizwa tangu 1914, umetimia kikamili. (Isaya 46:10; 55:10, 11) Naam, wakati ujao wenye amani duniani ni jambo hakika. Tunahakikishiwa wakati wetu ujao utakuwa hivyo iwapo tutatii Neno la Mungu na onyo lake lenye upendo kuhusu matukio yenye kutetemesha dunia yatakayotukia hivi karibuni.—Mathayo 24:42, 44; Yohana 17:3.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]

KUNA TUMAINI GANI KWA WAPENDWA WETU WALIOKUFA?

TUNAWEZA kulemewa na huzuni mpendwa wetu anapokufa. Biblia inatuambia kuwa Yesu alilia rafiki yake mpendwa Lazaro alipokufa. Hata hivyo, dakika chache baadaye Yesu alifanya muujiza wenye kushangaza, kwa kumfufua Lazaro! (Yohana 11:32-44) Kwa kufanya hivyo, aliwapa wanadamu wote msingi thabiti wa kuamini ahadi nzuri aliyokuwa ametoa mapema katika huduma yake aliposema: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Tumaini zuri la kufufuliwa na kuishi kwenye dunia paradiso na liwafariji wote ambao wamefiwa na wapendwa wao.—Matendo 24:15.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je, unatambua onyo la kwamba hizi ndizo siku za mwisho za ulimwengu huu?

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

USGS, David A. Johnston, Cascades Volcano Observatory