Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tulionywa kwa Kusoma Amkeni!

Tulionywa kwa Kusoma Amkeni!

Tulionywa kwa Kusoma Amkeni!

WATU ambao husoma Amkeni! kwa ukawaida huelewa thamani ya makala hizo. Lakini wenzi wa ndoa kutoka Ujerumani ambao walikuwa wameenda likizo huko Khao Lak, Thailand, Desemba mwaka jana, walithamini sana makala yenye kichwa “Mawimbi Yanayofisha—Hekaya na Ukweli,” katika toleo la Februari 8, 2001.

Gazeti la Ujerumani Frankenpost (Selber Tagblatt) liliripoti hivi simulizi la wenzi hao wa ndoa: “‘Tulikuwa tukiogelea,’ akumbuka Roswitha Gesell. Baada ya kuogelea baharini, wenzi hao walienda hotelini kubadili mavazi. Reiner Gesell anaeleza jambo lisilo la kawaida ambalo waliona baada ya kurudi kwenye ufuo: ‘Tuliporudi ufuoni dakika kumi baadaye, bahari haikuwepo.’ Tuliona tu sakafu ya bahari na tumbawe lililokuwa umbali wa kilometa saba hivi kutoka pwani. ‘Waogeleaji wote ambao bado walikuwa majini walikuwa wamevutwa baharini.’ Wenzi hao waliokoka kwa sababu ya makala fulani ya gazeti la Amkeni!” Makala hiyo ilieleza kwamba mara nyingi kabla ya tsunami kutokea, maji hupwa isivyo kawaida.

“Wenzi hao walipoona wimbi kubwa kwa mbali, waligeuka na kuanza kukimbia. Reiner Gesell anakumbuka kwamba ukuta wa maji ulionekana kuwa na urefu wa meta 12 hadi 15. Jambo analokumbuka kwa majonzi ni kwamba watalii wengine waliokuwa ufuoni walitazama tu bahari kwa mshangao. ‘Hawakusonga. Niliwaambia kwa sauti kubwa wakimbilie mahali salama, lakini hakuna aliyefanya chochote.’ Hakuna aliyeokoka.”

Ikizungumza kuhusu Gesell na mkewe, makala ya gazeti hilo ilisema hivi pia: “Kwa kuwa walikuwa Mashahidi wa Yehova, wakati wa likizo yao walishirikiana na kutaniko lililokuwa karibu, ambalo lilikuwa umbali wa kilometa 140 kutoka Khao Lak. Waamini wenzao walipopata habari kuhusu msiba huo, kutaniko zima lilienda Khao Lak kuwatafuta.”

Wenzi hao ambao sasa wamerudi Ujerumani wakiwa salama, wanashukuru sana kwa ajili ya habari muhimu iliyokuwa katika gazeti la Amkeni! Wanawashukuru sana watu wa Thailand waliowasaidia, hasa ndugu zao wa kiroho ambao walidhihirisha upendo wa kweli wa Kikristo.