Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilivutwa kwa Muumba na Kweli Nzuri za Biblia

Nilivutwa kwa Muumba na Kweli Nzuri za Biblia

Nilivutwa kwa Muumba na Kweli Nzuri za Biblia

SIMULIZI LA TSUYOSHI FUJII

MIAKA kadhaa iliyopita nilipewa pendeleo lisilo la kawaida. Nikiwa msaidizi wa Senei Ikenobo, mwalimu mkuu wa shule ya Ikenobo ya kupanga maua, nilipaswa kupanga maua kwenye chumba chenye fahari katika Jumba la Kifalme huko Tokyo, Japani. Tulifanya kazi chini ya ulinzi mkali. Nikiwa na wasiwasi mwingi, nilikuwa mwangalifu sana nisimwage hata tone moja la maji. Hiyo ilikuwa mojawapo ya matukio muhimu katika kazi yangu ya kupanga maua. Acheni niwaeleze jinsi nilivyoanza kazi hiyo.

Nilizaliwa mwaka wa 1948 huko Nishiwaki City, kaskazini-magharibi ya Kobe, Japani. Tangu nilipokuwa mtoto nilivutiwa sana na mimea na uzuri wa maua mbalimbali yanayochanua wakati wa yale majira manne. Hata hivyo, nililelewa na nyanya yangu aliyekuwa Mbudha mwenye bidii, hivyo sikuwazia kamwe kwamba kuna Muumba.

Mama yangu alifundisha na angali anafundisha ikebana, au ufundi wa kupanga maua, katika mji wa kwetu. Huko Japani, ikebana, ambayo pia inajulikana kama kado (upangaji wa maua), ni taaluma inayoheshimiwa sana. Ingawa Mama hakunifundisha ufundi huo, alikuwa na uvutano mkubwa juu yangu. Wakati ulipofika wa kuamua jambo nitakalofanya maishani, nilitaka kusomea kazi ya ikebana. Mwalimu na mama yangu walipendekeza nijiunge na chuo kikuu, lakini bila kusita niliamua kujiunga na Chuo cha Ikenobo. Ikenobo ndiyo taaluma ya zamani zaidi ya ikebana nchini Japani. Nilipokubaliwa katika chuo hicho, nilijifunza kwa bidii ufundi wa kupanga maua.

Naanza Kujifunza Ikebana

Wasanii wa Ikebana, ambayo ndiyo sanaa ya kitamaduni ya Japani, hufanya vitu vionekane kuwa hai. Acha nieleze. Huenda maua yaliyo katika ndoo ndani ya duka la kuuza maua yakavutia, lakini yanatofautianaje na mimea midogo inayochanua katika kiwanja au miti inayochanua milimani? Katika mazingira ya asili, mimea humfanya mtu atambue kuna uhai na majira. Huo ndio wakati ambapo huenda ukaguswa moyo zaidi. Ikebana ni njia ya kuonyesha uzuri huo wa uumbaji kwa kutumia maua na mimea na kuyapanga kwa njia inayokugusa moyo sana.

Kwa mfano, tuseme unataka kuonyesha kipindi cha majira ya kupukutika kwa majani. Unaweza kufanya hivyo kwa kutumia maua yanayochanua katika majira hayo kama vile kikoroga-maziwa na patrinia, pamoja na majani yanayopukutika wakati huo. Je, ungependa kuwe na upepo mwanana? Unaweza kuongezea mashina machache ya mmea unaoitwa eulalia ambayo huyumbayumba kidogo na kufanya watazamaji wahisi upepo mwanana wa majira ya kupukutika kwa majani. Nilivutiwa sana na ikebana, na nilifurahia sana kuonyesha hisia zangu kwa kupanga maua na mimea katika chombo cha maua.

“Familia” Kubwa

Ufundi wa kupanga maua wa ikebana ulianza miaka 500 iliyopita. Shule za ikebana husimamiwa na mwalimu mkuu. Cheo cha mwalimu mkuu hurithiwa. Akiwa mrithi wa utamaduni huo, yeye huwa na mamlaka ya kuwa mzee wa “familia” kubwa ya wafuasi. Kupatana na utamaduni, anapaswa kufundisha kizazi kinachofuata mbinu mpya alizobuni katika kipindi ambacho ameishi.

Baada ya kuhitimu kutoka Chuo cha Ikenobo na kumaliza somo la kiufundi la kado lililochukua miaka miwili, nilianza kufanya kazi kwenye Taasisi ya Ikenobo kuanzia Januari 1971. Nilipanga “Maonyesho ya Ikebana ya Taasisi ya Ikenobo” kotekote nchini Japani. Pia nilisafiri nchini kote nikiwa mmoja wa watu waliomsaidia mwalimu mkuu kutokeza kazi zake za ufundi.

Bado ninakumbuka mara ya kwanza kabisa niliposimama kwenye jukwaa la Uwanja wa Michezo wa Fukuoka nikiwa msaidizi wa mwalimu mkuu alipokuwa akionyesha jinsi ya kupanga maua. Nilikuwa na wasiwasi mwingi kwani nilikuwa mbele ya maelfu ya watu. Nilipinda mashina na kukata matawi, mambo ambayo sikupaswa kufanya. Lakini mwalimu mkuu alifanya mzaha kuhusu makosa hayo huku akiueleza umati yale aliyokuwa akifanya. Hilo lilinisaidia kutulia.

Niliandamana na mwalimu mkuu alipopanga maua wakati wa sherehe za kitaifa zilizohudhuriwa na watu mashuhuri kutoka nchi nyingine. Kama nilivyotaja mwanzoni, mojawapo ya pindi hizo zilifanya nijikute katika chumba chenye fahari katika Jumba la Kifalme.

Baadaye, wakati Chuo cha Mazoezi cha Ikenobo kilipoanzishwa kwa kusudi la kufundisha upya walimu nchini kote, nilipewa kazi iliyohusiana na kufundisha, kutayarisha mtaala, na kusimamia utayarishaji wa vitabu vya mafundisho na filamu ambazo zingetumiwa na wahadhiri kuwafundisha wanafunzi 200,000 hivi katika matawi 300 nchini Japani. Nilisafiri nchini kote kusimamia mtaala huo. Ikenobo pia ina matawi katika nchi nyingine, nami nilienda Taiwan mara kadhaa kwa mwaka. Kwa hiyo mwalimu mkuu alinitumaini nami nilikuwa na cheo kikubwa.

Nilifurahia kazi yangu, lakini sikuridhika kabisa na maisha yangu. Ingawa kazi yangu ilihusisha vitu vizuri, kuna mambo yaliyonitamausha. Wanafunzi walioneana wivu na kuchongeana, na mara nyingi walimu waliniomba mashauri. Lakini katika shirika lililoongozwa na utamaduni na mamlaka za kale, mambo mengi yalizidi uwezo wangu. Kwa kuwa wengi walipenda ikebana kikweli na walichukua masomo yao kwa uzito, nilijitahidi kadiri nilivyoweza kuwafanya wafurahie masomo yao.

Napata Kweli Nzuri kwa Mara ya Kwanza

Nilichukia dini kwa sababu nilifikiri kwamba ingenipofusha akili. Isitoshe, nilikuwa nimeona unafiki mwingi sana kati ya watu wanaozungumza kuhusu amani na furaha. Kwa upande mwingine, mke wangu Keiko, alitafuta kweli tangu utotoni. Alipendezwa na dini mbalimbali na alisikiliza mafundisho yao, lakini hayakutosheleza njaa yake ya kiroho.

Kwa hiyo, Shahidi wa Yehova alipotutembelea nyumbani, Keiko alikubali kujifunza Biblia. Alikuwa akiniambia kila kitu alichojifunza na mambo yaliyomvutia. Mambo ambayo Keiko aliniambia yalisikika kuwa mazuri, lakini sikuwa na shauku kama yake.

Hata hivyo, Keiko aliendelea kunieleza kwa usadikisho mwingi mambo aliyokuwa akijifunza kutoka katika Biblia. Sikuzote alikuwa akiweka magazeti kadhaa yaliyozungumzia Biblia ndani ya mkoba wangu niliposafiri. Lakini nilikataa kuyasoma. Nilitaka kulinda kazi na mafanikio yaliyochukua miaka mingi kupata. Tulikuwa tu tumenunua nyumba, na nilidhani kwamba nikikubali mafundisho ya Biblia, ningelazimika kuacha nyumba hiyo. Wakati huohuo, Keiko alifanya maendeleo haraka na kufuata mambo aliyoamini. Nilihisi nikiwa mpweke na nimetengwa. Ingawa nilijua kwamba yale aliyoniambia yalikuwa kweli, nilianza kumpinga.

Napinga Ingawa Navutiwa

Nilikuwa nikifika nyumbani usiku kutoka kazini, lakini jioni ambazo Keiko alihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova, nilikuwa nikichelewa hata zaidi kimakusudi. Hata niliporudi nyumbani saa nane au saa tisa za usiku, Keiko alikuwa akinisubiri ili anieleze mambo yaliyotendeka siku hiyo, na hivyo kuonyesha kwamba ananijali. Lakini sikuweza kuvumilia kuona familia yangu ikitoka nyumbani kwa saa kadhaa ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Nilizidi kumpinga mke wangu na kumwambia kwamba nitamtaliki. Hata hivyo, Keiko aliendelea kuwa imara.

Ilikuwa vigumu kuelewa tabia ya Keiko. Licha ya mkazo uliokuwa katika ndoa yetu na kwamba alikuwa na ugonjwa wa pumu, alifurahia kila jambo alilofanya. Nilivutiwa na Keiko hapo mwanzoni kwa sababu ya unyoofu na upole wake. Hiyo ndiyo sababu iliyonifanya niwe na wasiwasi kwamba angedanganywa alipoanza kujifunza Biblia.

Hata hivyo, Keiko alitumia yale aliyokuwa akijifunza na alijaribu kuwa mke na mama mzuri. Ingawa nilimpinga, aliponiomba nihudhurie mikutano na makusanyiko ya Kikristo, nilifanya hivyo mara kwa mara, labda kwa sababu nilijivunia Keiko.

Wakati huohuo, nilimwonea Yehova wivu. Nilipoona Keiko akijaribu kufanya mabadiliko, nilijiuliza kwa nini mafundisho ya Biblia yalikuwa na uvutano mkubwa hivyo juu ya watu. Niliwaza: ‘Kwa nini mke wangu yuko tayari kupatwa na magumu yote hayo kwa ajili ya Yehova?’

Baada ya muda, baadhi ya ndugu Wakristo katika kutaniko la Keiko walitaka kunitembelea nyumbani. Sikutaka kukutana nao. Hata hivyo, nilitaka kujua kilichomfanya Keiko awe na amani ya akili. Mwishowe, udadisi wangu ulifanya nikubali kujifunza Biblia. Nilipoanza kuwa na uhusiano wa karibu zaidi na watu walionitembelea, niliwaona kuwa wenye kuburudisha. Kupitia funzo la kila juma, kweli ya Biblia ilianza kupenya moyoni mwangu hatua kwa hatua na maoni yangu yakapanuka.

Uzuri wa Uumbaji na wa Kweli

Nilipojaribu kuonyesha uzuri na nguvu za uumbaji kupitia ikebana, nilikuwa na wasiwasi kuhusu jinsi ya kuonyesha fahari yake. Lakini nilielewa fahari hiyo nilipojifunza kwamba Yehova ndiye aliyeumba maajabu ya uumbaji. Mwanadamu duni anawezaje kushindana na uwezo wa kubuni wa Muumba? Yehova ndiye Msanii Mkuu Zaidi! Hata hivyo kwa kujaribu kumwiga, nilianza kupanga maua kwa njia bora zaidi. Kwa kweli, baada ya kuanza kujifunza Biblia, watu walianza kuniambia kwamba kazi yangu ilibadilika kwani kazi zangu zilionyesha uanana.

Kweli za Biblia zilinisaidia kuelewa mambo mengi kwa mara ya kwanza. Nilipojifunza kwamba mtawala wa ulimwengu huu, Shetani Ibilisi ndiye anayefanya watu wateseke na kwamba moyo wetu ni wenye hila kwa sababu ya dhambi tuliyorithi kutoka kwa Adamu, nilielewa maana halisi ya mambo yanayotukia ulimwenguni. (Yeremia 17:9; 1 Yohana 5:19) Nilijifunza kwamba Yehova ni Mungu wa amani, ana upendo, haki, nguvu, na hekima nyingi (Kumbukumbu la Torati 32:4; Waroma 11:33; 1 Yohana 4:8; Ufunuo 11:17); kwamba Mungu alichochewa na upendo kumtuma Yesu afe kwa ajili yetu (Yohana 3:16; 2 Wakorintho 5:14); na kwamba kuna wakati ambapo hakutakuwa na kuteseka au kifo (Ufunuo 21:4). Nilivutiwa na uzuri wa kweli hizo. Kwa kuongezea, Mashahidi wa Yehova hufuata fundisho la Yesu la ‘kumpenda jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Kujionea mwenyewe jambo hilo kulinihakikishia kwamba hiyo ndiyo dini ya kweli.—Mathayo 22:39.

Kukabiliana na Kizuizi

Ukweli ulipoanza kutia mizizi moyoni mwangu, nilikabili kizuizi. Mwalimu mkuu aliposhindwa kuhudhuria mazishi, mara nyingi nilimwakilisha katika mila za Wabudha. Hilo lilikuwa jaribu kwangu nilipotaka kujiweka wakfu kwa Yehova. Niliamua kwamba sitashiriki katika mila za Wabudha. (1 Wakorintho 10:21) Kwa heshima, nilimweleza mwalimu mkuu kwamba nilinuia kubatizwa karibuni na nilikuwa nimeamua kwamba sitashiriki katika ibada nyingine yoyote hata kama kazi yangu ingehusisha kufanya hivyo. Aliniambia kwamba hapingi uamuzi wangu wa kuwa Mkristo na kwamba ningeshughulikia mambo ya kidini kwa njia yangu mwenyewe. Jibu hilo lilinishangaza kwani nilifikiri kwamba ningeadhibiwa na kupoteza kazi yangu.

Niliposhinda kizuizi hicho, nilibatizwa ili kuonyesha wakfu wangu kwa Yehova katika kusanyiko la Kikristo mnamo Juni 1983, mwaka mmoja baada ya kuanza kujifunza Biblia. Nilipotoka katika kidimbwi cha ubatizo, nilikaribishwa na Keiko aliyetokwa na machozi na kutabasamu. Nikitokwa pia na machozi, tulimshukuru Yehova pamoja kwa ajili ya furaha tuliyokuwa nayo.

Naamua Kuacha Kazi

Mwalimu mkuu alikuwa ameonyesha kwamba alielewa kabisa msimamo wangu nikiwa Mkristo. Nilijaribu kufanya kazi yangu kwa makini kuliko awali. Hata hivyo, nilijaribu kudumisha usawaziko kati ya kazi yangu na maisha yangu ya Kikristo. Kwa miaka saba niliongeza utendaji wangu katika huduma ya Kikristo miezi kadhaa kila mwaka.

Hata hivyo, ilinibidi kufikiria kwa uzito hali ya kiroho ya mwana wangu wa pekee na afya ya Keiko iliyokuwa ikizorota. Nilijiambia, ‘Ninapaswa kutumia wakati mwingi zaidi na familia yangu.’ Pia nilitaka kutanguliza mambo ya Ufalme maishani mwangu. Tamaa na mahitaji hayo yalinichochea nisali kwa Yehova kuhusu kuacha kazi yangu ya ikebana. Mwalimu mkuu alitambua kwamba nilikuwa nimefanya uamuzi, na mwishowe nilifaulu kustaafu bila matatizo yoyote Julai 1990, nikiwa na umri wa miaka 42.

Kuwasaidia Wengine Waone Uzuri wa Ukweli

Muda mfupi baada ya kustaafu, nilianza huduma ya wakati wote ili kuwasaidia wengine wapate kweli. Kwa sasa, mimi hutumia siku moja kwa juma kuwafundisha watu kazi ya kupanga maua, bila kufuata mtindo wa Ikenobo. Nina pendeleo la kutumikia nikiwa mzee katika kutaniko, naye Keiko ni painia na sasa yeye hupatwa na ugonjwa wa pumu mara chache zaidi kuliko awali. Mwana wetu ambaye sasa ameoa ni mtumishi wa huduma katika kutaniko lililo karibu. Sote tunafurahia sana pendeleo kubwa la kumtumikia Yehova tukiwa familia!

Chini ya utawala wa Ufalme wa Yesu Kristo, ninatazamia kuchuma maua ambayo nitapanda kwenye bustani yangu na kuyapanga kwa njia maridadi. Tamaa yangu kubwa pamoja na familia yangu ninayoipenda ni kulisifu milele jina tukufu la Yehova, Muumba wa vitu vyote vizuri.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Nikiwa pamoja na mke wangu, mwana wangu, na familia yake

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kupitia ikebana, unaweza kuonyesha hisia zako kuhusu uzuri wa uumbaji