Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kutoka kwa Wasomaji Wetu

Kunenepa Kupita Kiasi Ningependa kuwapongeza kwa mfululizo wa makala zenye kichwa “Ni Nini Suluhisho la Kunenepa Kupita Kiasi?” (Novemba 8, 2004) Nimepunguza uzito wangu kwa kilo 50 kwa kuwa na mazoea mazuri ya kula na kufanya mazoezi kila siku. Baada ya kupunguza uzito huo, sasa ninaweza kufanya mengi zaidi, hivi kwamba ninaweza kutumia muda mrefu zaidi katika huduma pasipo kuchoka sana.

M. E., Marekani

Nina umri wa makamo nami nimeanza kuhangaikia zaidi afya yangu, hata hivyo sikujali sana unene wangu wa kupita kiasi. Sasa nimeazimia kupunguza uzito. Nilianza mara moja. Mfululizo huo ulinihakikishia kwamba Yehova anamjali kila mmoja wetu.

H. S., Japani

Asanteni kwa habari sahihi kuhusu kunenepa kupita kiasi. Leo nimeanza programu yangu ya kufanya mazoezi na kubadili mazoea yangu ya kula. Nimekuwa nikisoma magazeti yenu kwa zaidi ya miaka 30, nami nimefaidika sana maishani mwangu kutokana nayo!

N. J., Marekani

Nina uzito wa kilo 160, kulingana na chati iliyo kwenye ukurasa wa 5, napaswa kuwa na uzito wa kilo 76. Nina kibarua kikubwa cha kupunguza uzito wangu. Najua kwamba makala hiyo na maelezo ya watu wanaotajwa humo yatanisaidia.

W. O., Marekani

Nafurahi kujua kwamba Yehova na tengenezo lake wanajali afya yetu. Hata hivyo, jambo moja lililonishangaza ni ile chati iliyo kwenye ukurasa wa 5. Madaktari fulani hutumia chati inayoonyesha uzito wa chini na wa juu kulingana na umbo la mtu. Mimi nina umbo kubwa, kwa hiyo uzito wangu unapaswa kuwa tofauti na wa mtu mwenye umbo dogo.

C. S., Marekani

“Amkeni!” lajibu: Asante kwa habari hiyo. Chati iliyo kwenye ukurasa wa 5 ni mojawapo ya chati zinazoweza kumsaidia mtu kutambua uzito unaomfaa. Hatukunuia kudokeza kwamba njia nyinginezo haziwezi kutumika.

Mfululizo huo ulionyesha maoni ya watu wengi kwamba tofauti na mtu mnene, mtu mwembamba hufanikiwa maishani. Je, kuwa kwangu mnene kwamaanisha kwamba mimi ni mvivu, mzembe, na mtu asiyefaa kitu?

I. J., Ujerumani

Naona kwamba hamkuzungumzia jinsi tatizo hilo linavyomwathiri mtu kiakili. Nakubali kwamba ni muhimu kukabiliana na unene wa kupita kiasi, lakini vipi mtu akishindwa kupunguza uzito? Atahisije?

Y. Z., Urusi

Huenda wasomaji fulani wakadhani kwamba Yehova hupenda watu wembamba tu au kwamba watu wenye uzito “wa kawaida” ndio wanaoruhusiwa kuwa Mashahidi wa Yehova.

R. B., Ujerumani

“Amkeni!” lajibu: Wasomaji hao watatu wanatoa hoja ambazo hazikuzungumziwa katika makala hizo. Ni kweli kwamba unene wa kupita kiasi husababishwa na mambo mbalimbali mbali na kula kupita kiasi. Kwa mfano, dawa fulani zaweza kumfanya mtu aongeze uzito. Maumbile aliyorithi mtu yaweza kufanya iwe vigumu zaidi kwake kupunguza uzito. Vyovyote vile, hatukumaanisha kwamba watu wenye uzito unaofaa ndio wanaokubalika machoni pa Mungu. Tunatumaini kwamba mfululizo wa makala zetu ulimchochea na kumpa mapendekezo yeyote ambaye angependa kufuata programu fulani ya kuwa na mazoea mazuri ya kula na kufanya mazoezi na kupunguza uzito wake kwa kufanya hivyo. Programu hizo huokoa uhai. Tunasikitika kwa kutoeleweka kokote kulikozuka kutokana na suala hilo.